NA VERONICA ROMWALD, DAR ES SALAAM
KUNA watu huwa hawana desturi ya kuugua mara kwa mara, tofauti na wengine ambao maradhi kwao ni kawaida.
Ili kuepuka maradhi ya mara kwa mara, kuna mambo mengi ambayo
binadamu anapaswa kuyazingatia.
Leo tutazungumzia siri nane ambazo watu
wasiougua mara kwa mara huzingatia.
1. Pata mapumziko ya kutosha
Matokeo ya tafiti nyingi zilizofanyika katika sehemu mbalimbali
duniani yanaonyesha kwamba, watu wanaopata usingizi wa kutosha huwa na
furaha na afya bora.
Tafiti zinaonyesha kwamba kupumzika na kupata usingizi kwa saa nane
na zaidi ni muhimu katika kudumisha afya, kuzuia magonjwa na kukupa
furaha.
Kukosa usingizi na kutokupata mapumziko ya kutosha huchangia
kupandisha kiasi cha homoni zinazosababisha msongo wa mawazo na matatizo
chungu nzima ya kiafya.
2. Fanya mazoezi
Tafiti zinaonyesha kwamba kufanya mazoezi mara kwa mara huupa mwili
kinga ya maradhi mbalimbali. Tafiti zinaonyesha pia kwamba, kujumuika
kwa kushiriki katika michezo husaidia kuzuia tatizo la msongo wa mawazo
na matatizo mengine ya kiafya.
Mazoezi yana faida lukuki, ikiwa ni pamoja na kuzuia magonjwa sugu
kama vile kisukari na magonjwa ya moyo. Mazoezi pia huongeza kinga ya
mwili na kuongeza kiwango cha homoni zinazoleta hali ya furaha mwilini.
3. Epuka unywaji pombe kupindukia
Mvinyo na na aina nyingine ya pombe ni salama endapo tu zitatumika
katika kiwango kinachokubalika kiafya, tafiti zinaonyesha kwamba kiasi
kidogo cha mvinyo huimarisha afya ya moyo, mapafu na misuli hivyo
kumsaidia mnywaji kupata kinga na magonjwa sugu yasiyo ambukizi.
Watu wenye uwezo wa kudhibiti kiasi cha kilevi wanachotumia hufurahia vinywaji wavipendavyo huku wakizilinda afya zao.
Ikumbukwe kwamba, kiwango cha pombe kinachokubalika kiafya, kwa watu
wengi huweza kuonekana ni kidogo hivyo kuwafanya kunywa kupindukia.
Unywaji pombe kupita kiasi huweza kusababisha madhara mengi kwa afya na
hata kuhatarisha maisha yetu.
4. Jali unachokula
Chakula kinaweza kuwa dawa au sumu kwa maana ya kiasi na aina ya
chakula. Kula chakula bora ni kitu muhimu katika kudumisha afya bora.
Matokeo ya tafiti yanaonyesha kwamba watu wanaojali wanachokula kwa
kuzingatia kula chakula bora hujikinga na aina nyingi za magonjwa hivyo
kuwa na afya bora na furaha tele.
5. Kuwa na mitazamo chanya
Hufanya kazi kwa ufanisi na bidii wakati huo huo hukubaliana na matokeo.
Huwa na mategemeo ya mafanikio na furaha katika maisha. Hufurahia
maisha na kutokufungwa na makosa yanayotokea katika maisha.
Huchagua ubora juu ya kiasi na kuto jilinganisha au kujishindanisha na watu wengine.
6. Cheka mara kwa mara
Ziko tafiti nyingi zinazoonyesha umuhimu wa kutabasamu na kucheka
katika kudumisha afya. Watu wanaotabasamu na kucheka mara kwa mara
hujikinga na msongo wa mawazo hivyo kukaribisha furaha na afya katika
maisha yao.
Tafiti zinaonyesha pia kwamba, watu hawa huishi maisha marefu yaliyojawa na afya na furaha.
7. Lala na kuamka mapema
Kulala kwa muda wa kutosha peke yake haitoshi. Tafiti zinaonyesha
kwamba, kulala mapema na kuamka mapema ni muhimu katika kudumisha afya
na kuleta furaha maishani.
Baada ya kufanya kazi wakati wa mchana, kwa kawaida miili huwa imechoke hivyo
kuhitaji mapumziko. Lakini pia huwa na nguvu na ufanisi mkubwa wakati wa alfajiri.
Kwa maana hiyo, ni muhimu kulala mapema ili angalau kutimiza saa nane.
8. Nawa mikono mara kwa mara
Tabia ya kunawa mikono mara kwa mara husaidia kuzuia magonjwa mbalimbali.
Matokeo ya tafiti hizo yanaonyesha kwamba kunawa kwa kutumia sabuni
hutukinga na magonjwa kama vile kuharisha, mafua na magonjwa ya tumbo.
Ziko tafiti zilizowafuatilia watu wenye tabia ya kunawa mara kwa mara
na kuwalinganisha na wale wasio na tabia hiyo na kubaini kwamba wenye
tabia ya kunawa mikono mara kwa mara huwa na kinga ya magonjwa ya
mlipuko kwa asilimia mpaka tisini.
Wataalamu na wanasayansi wanatushauri kunawa kabla na baada ya kula
chochote, pia kunawa tunapotoka msalani na hata tunapotoka sehemu zenye
mikusanyiko ya watu.
Makala haya yameandaliwa kwa msaada wa mtandao wa Jamii Health.
Chapisha Maoni