NA
VERONICA ROMWALD – DAR ES SALAAM
RIPOTI ya utafiti uliofanywa na uwezo (iliyopo Twaweza)
imeeleza kwamba kuna uhusiano mkubwa kati ya matokeo ya kujifunza na utapiamlo.
Utafiti huo ulilenga kuangalia juu ya uhusiano uliopo kati ya lishe na matokeo ya kujifunza,ulifanyika kati
ya Oktoba na Desemba, mwaka jana.
Uwezo ilitoa matokeo ya utafiti huo Dar es Salaam jana katika
halfa iliyofanyika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM).
Akizungumza kuhusu utafiti huo, Mkurugenzi Mtendaji wa
Twaweza, Aidan Eyakuze alisema ulihusisha watoto 197,451 na kaya 68,588 nchini.
“Matokeo yanaonesha miongoni mwa watoto wenye miaka 10
mpaka 14, ambao walipimwa uwezo wa kusoma hadithi ya kingereza ya kiwango cha
darasa la pili, Watoto wenye utapiamlo walifaulu kwa kiwango cha asilimia 17.9,
wenye utapiamlo wa wastani asilimia 16.4 na wasio na utapiamlo walifaulu kwa
asilimia 25.8.
“Walipimwa pia uwezo wa kusoma hadithi ya Kiswahili ya
kiwango cha darasa la pili ambapo watoto wenye utapiamlo walifaulu kwa asilimia
46.3, watoto wenye utapiamlo wa wastani asilimia 51.3 walifaulu na wasio na
utapiamlo asilimia 65.8 walifaulu,” alisema.
Aliongeza “Walipimwa uwezo wa kufanya hesabu za kuzidisha
za kiwango cha darasa la pili, watoto wenye utapiamlo asilimia 35.5 walifaulu,
watoto wenye utapiamlo wa wastani asilimia 37.7 walifaulu na wasio na utapiamlo
asilimia 53.4 walifaulu.
“Matokeo haya yanaonesha watoto wasio na utapiamlo
wanafaulu zaidi kusoma masomo ya Kiswahili na Hisabati kuliko wale wenye
utapiamlo,” alisema.
Alisema takwimu zilizokusanywa zinaonesha kuwa, kwa ujumla
kitaifa, asilimia nne ya watoto wenye umri chini ya miaka mitano, asilimia 5.6
ya watoto wenye miaka kati ya mitano na tisa na asilimia 5.7 ya watoto wenye
miaka kati ya 10 hadi 14 wana utapiamlo.
“Hata hivyo kuna utofauti mkubwa kiwilaya, asilimia 23.9 ya
watoto wa Songea Mjini walio chini ya miaka mitano wana utapiamlo ukilinganisha
na asilimia 0.3 wilaya ya Tabora Mjini na Musoma Mjini,” alisema.
Alisema kwa wastani, asilimia 50 ya kaya zinamudu milo
mitatu kwa siku.
“Matokeo yanaonesha kuwa baadhi ya wilaya zina zaidi ya
asilimia 85 ya kaya zinazomudu milo mitatu kwa siku, Mbulu asilimia 97.6,
Kishapu asilimia 88.2, Mafinga Mjini asilimia 88, Tunduma asilimia 86.4, Moshi
Mjini asilimia 86. Lakini katika wilaya nyingine, kaya chini ya asilimia 40
ndizo zinazomudu milo mitatu kwa siku mfano Masasi asilimia 38.6, Tandahimba asilimia
35.5, Mtwara Vijijini asilimia 27.6 na Nanyumbu asilimia 23.1,” alisema.
Alisema kitaifa, ni
shule moja tu kati ya tano inayotoa huduma ya chakula cha mchana shuleni sawa
na asilimia 23.
Alisema kwa mkoa wa Kilimanjaro asilimia 79 ya shule zinatoa chakula cha mchana lakini
katika mkoa wa Geita, ni asilimia tano tu ya shule zinazomudu chakula cha
mchana kwa watoto.
“Utafiti huu umethibitisha kile ambacho wengi wetu tulikuwa
tunadhani, uwezo wa watoto kufanya vizuri shuleni unaathiriwa na jinsi
wanavyopata lishe nzuri.
“Katika awamu hii ya elimu bila malipo ya ada, suala la
utoaji wa chakula shuleni limeachwa njia panda. Halijaainishwa kwenye fedha za
ruzuku zinazotumwa moja kwa moja shuleni na serikali.
“Wazazi nao wameacha kutoa michango shuleni, kutokana na
matamko rasmi ya kufuta michango yote mashuleni. Tunajiuliza, Je, suala la
michango ya wazazi kwa ajili ya chakula cha watoto wao waki shuleni bado
halizungumziki? Si vibaya tukalijadili
hili pia, miongoni mwa jitihada nyingine sinazofanywa kuhakikisha watoto wetu
wanajifunza,” alisema.
Meneja wa Uwezo Tanzania, Zaida Mgalla, alisema takwimu
hizo zinaonesha taswira ya hali ya lishe ya watoto.
“Inaonekana wazi kwamba upo uhusiano mkubwa kati ya lishe
ya watoto na matokeo yao ya kujifunza, hivyo utoaji wa chakula shuleni inaweza
ikawa njia mojawapo ya kuwapa motisha wanafunzi kuhudhuria zaidi shuleni,”
alisema.
Chapisha Maoni