NA VERONICA ROMWALD – DAR ES SALAAM
MZAZI mchunge mwanao, ndiyo ujumbe mahususi unaopaswa kuusimamia kuelekea sikukuu ya christmass na mwaka mpya.
Unatakiwa kuwa makini kwani Jeshi la Polisi nchini limeonya kwamba litawachukulia hatua kwa kuwakamata na kuwashtaki wazazi wa watoto ambao watapotea na kufikishwa katika vituo vya polisi.
Msemaji wa Jeshi hilo, Kamishna Msaidizi, Advera Bulimba (pichani chini), ameeleza hivyo katika mkutano wake na waandishi wa habari alioufanya jana Dar es Salaam.
Amesema imekuwa ni kawaida kwa watoto wengi kufikishwa vituoni baada ya kupotea katika kipindi cha msimu wa sikukuu.
“Tutawaita wazazi watusaidie wakati watoto wanapotea wao walikuwa katika
mazingira gani, maana imekuwa ni kawaida kipindi cha sikukuu vituo vya
polisi vinajaa watoto waliookotwa katika maeneo mbalimbali, ikiwamo
fukwe za bahari,” alisema.
Aidha, aliwataka wananchi kuepuka kulewa kupita kiasi, hasa wale
wanaoendesha vyombo vya moto na kwamba wakikamatwa sheria itachukua
mkondo wake.
“Kwa ujumla wananchi wajue kwamba jeshi lao limejipanga kikamilifu
kuimarisha ulinzi nchini kwa kushirikiana na vyombo vingine vya usalama
kuelekea msimu huu wa sikukuu.
“Uzoefu unaonyesha sikukuu za mwisho wa mwaka huambatana na vitendo
vinavyohatarisha usalama wa raia na mali zao, utumiaji wa vilevi kupita
kiasi, utapeli, wizi, unyang’anyi na uendeshaji wa vyombo vya moto bila
kuzingatia sheria na kanuni za usalama barabarani, askari watafanya
doria wakati wote,” alisema.
Aliwataka pia watu wanaomiliki nyumba za kulala wageni na maduka
makubwa kama vile hoteli na ‘supermarket’ kufunga kamera za usalama.
“Wafunge kamera ili waweze kufuatilia kila kinachoendelea katika
maeneo yao, nani kaingia, nani katoka na anafanya nini,” alisema.
Pia, aliwaonya wafanyabiashara wanaomiliki kumbi za starehe, huku
likiwataka kuzingatia masharti ya leseni zao walizopewa hasa msimu huu
wa sikukuu.
Amewataka wamiliki wa kumbi za starehe wazingatie kiwango cha idadi
ya watu wanaoruhusiwa kuingia ukumbini na iwapo watagundulika kuzidisha
watachukuliwa hatua kali za kisheria.
“Tumegundua katika msimu wa sikukuu kuna baadhi ya watu hupenda kuitumia fursa hiyo kujipatia kipato kisicho halali.
“Tutapita hadi kwenye kumbi za starehe, tukikuta mtu ameruhusu watu
zaidi ya kiwango cha leseni yake tutamchukulia hatua za kisheria,”
alisema.
Chapisha Maoni