NA VERONICA ROMWALD, DAR ES SALAAM
DAKTARI bingwa wa magonjwa ya akili kwa watoto na vijana wa Hospitali
ya Taifa Muhimbili (MNH), Doroth Mushi, amesema tatizo la kukojoa
kitandani kwa watu wazima linatibika.
Akizungumza na MTANZANIA hospitalini hapo hivi karibuni, Dk. Mushi
alisema wamekuwa wakipokea vijana mbalimbali wanaokabiliwa na tatizo la
kutokwa na haja ndogo kitandani wakiwa usingizini na kuwapatia matibabu.
“Vijana wenye tatizo hili ni wengi, hasa wale waliofikia umri wa kuoa
au kuolewa, huwa wanakuja hapa tunawatibia. Kuna dawa huwa tunawapatia,
lakini pia tunawapa ushauri nasaha,” alisema Dk. Mushi.
Alisema Idara ya Magonjwa ya Akili hospitalini hapo ndiyo inayohusika
kutoa matibabu ya tatizo hilo ambalo linatajwa kuwa lipo katika kundi
la magonjwa ya akili.
“Kukojoa kitandani ni tatizo la kiakili, kawaida tatizo huanza
kujitokeza wakati wa ukuaji wa mtoto, lakini kwa kuwa wengi hawajui,
huchukulia kama ni hali ya kawaida na kwamba litaisha kadiri
anavyoendelea kukua,” alisema.
Alisema ingawa wapo ambao huacha kukojoa kitandani bila kwenda
hospitali, wengine hali hiyo huendelea nayo hadi wanapofikia umri wa
ujana kwa kukosa matibabu mapema.
“Kwa sababu wazazi wengi hawajui kwamba ni tatizo la akili, mtoto
akiendelea kupatwa na hali ya kutoa haja ndogo kitandani mara kwa mara
na wapo ambao hutoa hata haja kubwa, huishia kuwaadhibu badala ya
kuwafikisha hospitalini kwa uchunguzi na tiba,” alisema.
Alisema ni kweli wazazi wanayo haki ya kuwaadhibu watoto na vijana
wao, lakini hiyo si tiba sahihi, hivyo wanapaswa kuwafikisha hospitalini
iwapo hali hiyo inajitokeza mara kwa mara.
Daktari huyo ambaye pia ni mhadhiri katika Chuo cha Sayansi na Tiba
Muhimbili (MUHAS), alisema zipo sababu nyingi zinazochochea mtoto kupata
matatizo ya akili, ikiwamo mjamzito kukaa na uchungu kwa muda mrefu.
“Matatizo ya akili mengine hurithiwa kwa sababu yapo kwenye vinasaba.
Pia mtoto hupata tatizo iwapo mama akikaa na uchungu muda mrefu wakati
wa kujifungua, hali hiyo husababisha athari kwenye ubongo wa mtoto,
kwani hukosa oksijeni ya kutosha,” alisema.
Aliongeza kuwa yapo pia baadhi ya magonjwa ambayo mama akiugua katika
kipindi cha ujauzito huweza kumsababishia mtoto athari katika ubongo
wake, ndiyo maana wataalamu wa afya husisitiza mama afike kliniki
kipindi chote cha ujauzito.
Chapisha Maoni