Na Catherine Sungura, W. Afya
UJUMBE wa wawekezaji kutoka nchini Misri umewasili nchini na
kufanya mazungumzo na serikali ya Tanzania kwa nia ya kujenga viwanda
vya dawa za binadamu zikiwemo za majimaji pamoja na zile za antibiotic.
Ujumbe huo ulikutana jana na Waziri wa Afya, Maendeleo ya
Jamii, Jinsia,wazee na Watoto, Ummy Mwalimu pamoja na wawakilishi kutoka
wizara Viwanda, Biashara na Uwekezaji na Kituo cha Uwekezaji cha Taifa (TIC).
Kikao hicho kilifanyika katika ofisi ndogo ya wizara hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam.
Ujumbe huo ulisema watazalisha dawa za majimaji yaani “IV Fluids” pamoja na “antiobiotics”
za aina mbalimbali ikiwemo "Paracetamol IV” na dawa za kutibu Malaria.
Ulisisitiza lengo lao ni kujenga kiwanda kikubwa ambacho kitakuwa
na uwezo wa kuzalisha dawa ambazo zitawahudumia watanzania pamoja na
nchi za Afrika Mashariki na ya kati.
Katika mazungumzo
hayo,wawekezaji hao pia wanatarajia kusaidia Tanzania katika uzalishaji
wa chanjo ya ugonjwa wa homa ya Ini (Hepatics B na C ).
Waziri Ummy amewaahidi wawekezaji hao kuwasaidia katika mipango ya
ujenzi huo na kutoa ushirikiano wa dhati katika kufanikisha jambo hilo katika muda uliopangwa.
“Naelekeza kwa taasisi
zote zitakazoguswa na uanzishwaji wa viwanda hivi watoe ushirikiano wa
hali ya juu ili lengo hili lifikiwe, soko la dawa hapa nchini lipo naomba
niwahakikishie hili,”alisema waziri Ummy.
Waziri Ummy aliwaomba
wawekezaji hao kuharakisha ujenzi huo ndani ya
miezi kumi na nane kama walivyoahidi ili watanzania waanze kunufaika
mapema.
Chapisha Maoni