Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
WATALII kutoka nchi takatifu ya Israel wameonesha nia ya kuja kutembelea mbuga mbalimbali zilizopo nchini na kumuona faru fausta.
Faru huyo ndiye mwenye umri mkubwa kuliko wote barani Afrika na anapatikana nchini Tanzania pekee.
Hayo yameelezwa hivi karibuni na Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Utalii Tanzania
(TTB), Devota Mdachi alipokuwa akizungumza kuhusu ziara ya siku tatu waliyofanya nchini humo.
Katika ziara hiyo, Mdachi aliongozana na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya
Maliasili na Utalii, Dk. Aloyce Nzuki.
“Tunafahamu Waisraeli wanapenda kuangalia wanyamapori. Nilipokuwa
nikiwatajia wanayama tulio nao walionesha kufurahi hasa nilipowaeleza
kuwa faru Fausta (55) mwenye umri mkubwa kuliko wote barani Afrika yupo
katika ardhi ya Tanzania walionyesha kuvutiwa zaidi,” alisema Mdachi.
Alisema Bodi ya Utalii Israel imeahidi kushirikiana na Bodi ya Utalii
Tanzania (TTB) katika kutangaza vivutio vilivyopo na kukuza sekta ya
utalii nchini.
"Ziara imeleta mafanikio makubw akatika sekta ya utalii, lengo lilikuwa kukutana na wadau wa sekta ya utalii nchini humo wakiwamo mawakala wa utalii na wa sekta ya malazi," alisema.
Alisema Israel imeonesha shauku kubwa ya kushirikiana na TTB kuutangaza utalii wa Tanzania.
Kumbuka
*Hivi karibuni serikali ilitumia mamilioni ya fedha kumtibu Faru fausta alipougua jambo ambalo lilizua gumzo nchini.
*Kwa ujio huo wa watalii ni wazi kwamba faru huyo atasaidia nchi kupata fedha nyingi.
Chapisha Maoni