Kijana Abdallah akidhibitiwa na walinzi wa Muhimbili, muda mchache alipokamatwa kabla ya kupelekwa kituo cha polisi salenda (Picha na Veronica Romwald)
NA VERONICA ROMWALD – DAR ES SALAAM
UONGOZI wa Hospitali ya Taifa Muhimbili umewaonya watu wanaoingia ndani ya viunga vya hospitali na kujifanya madaktari 'vishoka' huku wakijua kuwa si kweli.
Umesisitiza kwamba iwapo watakamatwa hakuna msamaha wa aina yoyote utakaotolewa na kusisitiza watafikishwa kwenye vyombo vya dola wachukuliwe hatua kwa mujibu wa sheria.
Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano ya Umma na Huduma kwa Wateja Muhimbili, Aminiel Aligaesha amesema hayo alipozungumza na mtandao huu kuhusu tukio la kukamatwa kwa kijana Abdallah Athuman anayedaiwa kuwa ni daktari feki.
"Wapo watu ambao hutumia mtindo huo wakiwa na nia ya kuwadanganya wagonjwa ili kupata fedha kutoka kwao (rushwa) kwa madai kwamba watawasaidia kupata matibabu.
“Mtakumbuka miaka mitatu iliyopita, kulikuwa na matukio
mengi ya namna hii, tuliamua kuweka ulinzi madhubuti kila eneo la kutolea huduma
na si rahisi mtu kuwajua walinzi wetu, wakikukamata tutachukua hatua kwa mujibu
wa sheria,” amesema.
Ameongeza “Kijana huyu ni mfano kwa wengine, walinzi wetu walimkuta
akiwahoji wagonjwa, walishamuhisi na kumfuatilia nyendo zake siku nyingi,
walimfuata na kumuuliza maswali ya msingi hakuweza kujibu.
“Walimuuliza historia yake kimasomo akadai, amesoma kidato
cha kwanza hadi cha nne mwaka 1998 hadi 2012 na kidato cha tano na sita mwaka
2013 hadi 14, unaweza kuona anatudanganya kiasi gani,” amesema.
Amesisitiza “Muhimbili si mazingira ya watu kuja kufanya
utapeli kama wapo wengine, kupitia mfano huu tutawafikisha vyombo vya dola
sheria ichukue mkondo wake.
Kijana huyo alikamatwa juzi asubuhi na walinzi wa hospitali hiyo wakati walipokuwa wakifanya doria.
Akizungumza na mtandao huu, Mkuu wa Oparesheni wa
Kampuni ya Ulinzi Nge, Muhimbili, Vitus Kabonge amesema wamefanikiwa kumkamata
kijana huyo baada ya kuweka mitego yao.
“Tulipata taarifa zake siku nyingi, tukaanza kufuatilia
nyendo zake, tulimkuta akihoji mgonjwa, tukamuita ofisini kwetu ajieleze.
“Tulitaka atupe kitambulisho chake cha kazi na atueleze
yupo kitengo gani, hakutupa maelezo, tukamuweka chini ya ulinzi,” amesema.
Mwenyewe (Athuman) amesema alifika hospitalini hapo si kwa nia ya kufanya uhalifu bali kumsalimia
rafiki yake lakini ndipo akashangaa akikamatwa na walinzi hao.
“Nilikuwa pale maeneo ya benki ya damu (Maabara Kuu ya
hospitali), nilikuja kumsalimia rafiki yangu, nikakamatwa, hiki kifaa
nilichonacho shingoni si changu kuna daktari mwanafunzi alikuja akaniachia
nimshikie,” amesema.
Chapisha Maoni