NA VERONICA ROMWALD – DAR ES SALAAM
Anakueleza inabidi uendelee kusubiri wodini kwa siku kadhaa kwani wamelazimika kusogeza mbele tarehe yako ya kufanyiwa upasuaji kutokana na sababu zilizo nje ya uwezo wao.
Kwamba hospitali imepokea majeruhi wengi ambao wamepata ajali hivi punde na wanalazimika kuwahudumia haraka kuokoa maisha yao.
Anakueleza ingawa wanao uwezo wa kuwapa huduma majeruhi hao na wewe hata hivyo wanalazimika kuahirisha upasuaji wako kwa sababu hakuna damu ya kutosha.
Hapana shaka suala hilo litakusikitisha na kukukatisha tamaa, lakini utalazimika kukubaliana nalo huku ukizidi kumuomba Mwenyezi Mungu akusaidie uweze kufanyiwa upasuaji huo ili uwe na afya njema tena.
Mkurugenzi wa Huduma za Tiba Shirikishi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Dk Plaxeda Ogweyo anasema kuna wakati hulazimika kusubirisha wagonjwa wodini kutokana na uhaba wa damu.
“Inajulikana wazi, Muhimbili ni hospitali kubwa nchini ambayo inapokea wagonjwa wanaosumbuliwa na magonjwa yote na tunao uwezo wa kibingwa kuwahudumia wote,
“Lakini kuna wakati huwa tunalazimika kusubirisha wagonjwa wodini hasa wale ambao hawahitaji kuongezewa damu ili tuhudumie wale wanaokuwa na uhitaji kwa wakati huo tuweze kuokoa maisha yao,” anasema.
Dk Ogweyo (Mwenye shati jeupe anayemfafanulia jambo Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Sophia Mjema) anasema ili kutosheleza mahitaji ya hospitali hiyo kila siku wanahitaji kukusanya chupa za damu 100 hadi 120 hata hivyo huwa inakusanya chupa 60 hadi 70 pekee.
“Hii ni changamoto kwa kweli tunao uwezo wa kuhudumia wagonjwa wote lakini inabidi tuanze na wale wanaokuwa wanahitaji huduma ya dharura kwa mfano majeruhi wa ajali ambao huhitaji kuongezewa damu,” anasema.
Dk. Ogwola anasema ili kukabiliana na hali hiyo, huwa wanafanya kampeni za ukusanyaji damu kwa kupita katika shule mbalimbali, vyuo, ofisi za umma na binafsi kuhamaisha wananchi wajitolee damu.
Ofisa Mtoa Damu kutoka Mpango wa Taifa wa Damu Salama Peter Chami akiangalia wingi wa damu ya Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo Pedro Pallangyo ambayo aliitoa katika kituo cha kuchangia damu cha Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)
Hali ilivyo JKCI
Kaimu Mkurugenzi wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete, Dk. Peter Kisenge anasema uhitaji wa damu katika hospitali hiyo ni mkubwa.
Anasema mara nyingi kwa siku huwa wanafanya oparesheni mbili kubwa za moyo ili kufanikisha upasuaji huo huhitaji kutumia kati ya chupa tatu hadi tano za damu kwa mgonjwa mmoja.
“Damu ni muhimu katika mwili wa binadamu, ili mtu aweze kuishi anahitaji damu, yenyewe huhitajika kupeleka oksijeni na virutubisho mwilini mwake,” anasema.
Daktari huyo anasema ingawa suala la upatikanaji damu kutosheleza mahitaji ni tatizo, lakini changamoto kubwa ambao hukabiliana nayo ni upatikanaji wa damu ya watu waliopo kwenye kundi B- na B+.
“Kuna wakati tunapata wagonjwa waliopo katika kundi hili la
damu ingawa huwa si wengi, mara nyingi ni kati ya wawili au watatu inapotokea
tunakosa damu ya kuwaongezea huwa tunalazimika kuwapigia watu ambao
tunawafahamu wapo kundi hilo tunawaomba waje kujitolea damu kusaidia wagonjwa
hao, na kwa kuwa wapo tayari kujitolea huwa wanakuja,” anasema.
Anasema kuna kipindi uhitaji wa damu huwa mkubwa zaidi hasa
zinapotokea ajali kwani majeruhi huhitaji kuongezewa damu kuokoa maisha yao.
“Siku hizi ajali za bodaboda zimekuwa nyingi mno,
zinapotokea hivyo JKCI tunapata shida mno, unakuta tunalazimika kubadili ratiba
ya upasuaji ikiwa tulipanga kuwafanyia wagonjwa watano kwa wiki inabidi
tuwafanyie wagonjwa watatu tu,” anasema.
Hali halisi
Ukweli ni kwamba hali ya upatikanaji wa damu nchini bado hairidhishi, kiasi kinachokusanywa kwa mwaka hakitoshelezi mahitaji halisi.
Shirika la Afya Duniani (WHO) linapendekeza, kila nchi iwe
na hifadhi ya damu kwa kiwango cha asilimia moja ya idadi ya watu wake ili
kuweza kutosheleza mahitaji yake.
Kwa uwiano huo, Tanzania inapaswa kukusanya chupa za damu
500,000 kila mwaka, lakini Mpango wa Taifa wa Damu Salama nchini haijawahi
kufikia kiwango hicho cha ukusanyaji wa damu nchini.
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na
Watoto, Ummy Mwalimu anasema takwimu za ripoti ya mwaka 2016 pekee zinaonesha zilikusanywa
jumla ya chupa za damu 196,735 kwa kipindi cha Januari mpaka Desemba.
“Ingawa inaonesha kuongezeka kwa makusanyo ya damu zaidi ya
mara tatu ikilinganishwa na chupa za damu 65,000 ambazo zilikusanywa mwaka
2015, hata hivyo bado ni changamoto,” anasema.
Anasema mahitaji ya damu ni makubwa nchini hasa kwa kundi
la wanawake ambao wengi wamekuwa wakipoteza maisha kwa kuvuja damu nyingi hasa
wakati wa kujifungua.
“Iwapo kungekuwa na akiba ya
kutosha ya damu, wanawake wengi
wasigepoteza maisha yao kwa kukosa damu, kufariki kwa kukosa damu ni kifo ambacho kinaweza kuzuilika.
“Takwimu
za hivi karibuni zinaonyesha, takribani wanawake 556 kati ya vizazi hai 100,000
hufa kila mwaka kutokana na matatizo ya uzazi nchini, inakadiriwa asilimia 40
ya vifo hivyo vingeweza kuepukika kama kungekuwa na akiba ya kutosha ya damu
salama,” anasema.
Waziri Ummy (mwenye nguo ya kitenge) anasema Juni 14, kila mwaka dunia huadhimisha Siku ya Wachangiaji Damu Duniani kwa lengo la kuhamasisha jamii ijitolee damu kwa ajili ya kusaidia wengine.
“Siku ni ukumbusho wa siku ya kuzaliwa Karl Landsteiner, huyu ndiye aliyegundua mfumo wa makundi ya damu ambayo ni kundi A, B na O na alizawadiwa tuzo ya Nobel kutokana na ugunduzi huo,” anabainisha.
Waziri Ummy anasema maadhimisho ya mwaka huu yalipewa kauli mbiu isemayo, ‘Changia damu Changia sasa na Changia mara kwa mara.
“Kauli mbiu hiyo imelenga kuhamasisha uchangiaji damu ili kukabiliana na dharura inayoweza tokea ya uhitaji wa damu, kila mwananchi mwenye vigezo vya kuchangia damu anakumbushwa kujenga utamaduni wa kuchangia damu mara kwa mara ili Taifa liwe na akiba ya kutosha ya damu,” anasema.
Anasema Wizara kwa kutumia wataalamu wake itaendelea kuelimisha jamii kuhusu umuhimu wa kuchangia damu kwa hiari.
Anasema wizara itaendelea pia kutoa rasilimali watu na fedha ili Mpango wa Taifa wa Damu Salama uweze kutimiza majukumu yake na hatimaye kupunguza vifo ambavyo vinaweza kusababishwa na ukosefu wa damu.
“Serikali imeongeza kiwango cha fedha kwenye bajeti ya mwaka 2017/18, zimetengwa Sh. bilioni 5.5 kwa ajili ya Mpango Taifa wa Damu Salama kutoka Sh 4.5 bilioni zilizotengwa mwaka 2016/17,” anafafanua.
Agizo kwa halmashauri
Waziri Ummy anasema
pamoja na hatua hizo, ni vema Halmashauri zote nchini zitenge bajeti kwa ajili
ya kununulia vifaa vya kukusanyia damu.
Anasema kila mkoa na
halmashauri zinapaswa kuhakikisha hospitali zake zinakuwa na damu salama wakati
wote.
“Viongozi wa mikoa na halmashauri waweke utaratibu wa kukusanya damu kutoka kwa wachangia damu wa
hiari na kuacha tabia ya kutegemea
kupata damu toka kwa wachangia damu wanandugu ( Family replacement donors).
“Wanandugu kuchangia damu uwe ni utaratibu wa dharura ambao wakati
mwingine si salama kwani ndugu hulazimika kuchangia damu hata kama hawana
vigezo vya kuchangia damu,” anasema.
Anaongeza “Ili kuendelea kuhakikisha ubora wa damu ambayo inakusanywa
sampuli zote zitumwe katika vituo vya kanda vya mpango wa Taifa wa Damu salama
ili zipimwe katika ubora na viwango vinavyotakiwa ( Quality assured manner).
Umuhimu wa damu mwilini
Wanasayansi wanaeleza kwamba ili mnyama na binadamu waweze kuishi wanahitaji damu, damu ni tishu inayopatikana katika mwili wa binadamu na manyama ambayo huzunguka mwilini ndani ya mishipa ya damu ikisukumwa na moyo kwa lengo la kumuwezesha waishi.
Wanataja kazi kuu ya damu ni kupeleka lishe na hewa ya oksijeni katika seli za mwili na kutoa hewa ya kaboni daioksaidi pamoja na taka zingine kutoka kwenye seli hizo.
Wanafafanua kwamba ndani ya damu kuna ute-gili (plasma) na seli za damu nyeupe na nyekundu. Kazi kuu ya seli nyekundu za damu ni kubeba hewa ya oksijeni.
Wanasema kazi ya ute-gili ni kubeba hewa ya kaboni dioksaidi. Wakati seli hai nyeupe za damu zenyewe hufanya kazi kama walinzi wa mwili wa kupambana na magonjwa na zipo pia chembe sahani.
Chapisha Maoni