Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement

https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEgBJWNcyjI2X91jbmkoaBJN7krUG7V881jcVIiVOynHUPt8PVOB3NfWSxfzTn-28XDaLuYYB9GV9PU0LS_1LfWfxrD93zbA_X1jOm8NqI4IBR6Vio_W9vgtWMOucpgYEumH073f6f59r1o/s1600/Muhimbili.jpgNa Mwandishi Maalumu, Dar es Salaam


WATUMISHI wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) wakiwamo madaktari, wauguzi na wale wa kada nyinginezo wameanza upya kuhakikiwa taarifa zao.


Akizungumza na MTANZANIA jana, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano ya Umma na Huduma kwa Wateja wa Muhimbili, Aminiel Aligaesha alisema uhakiki huo unafanyika kufuatia agizo walilopokea kutoka serikalini.


“Ni kweli tulifanyiwa uhakiki, lakini tumepokea barua inayotaka tuhakiki tena watumishi na tayari tangazo limebandikwa katika mbao za matangazo na uhakiki umeanza,” alisema.


Aligaesha alisema baada ya kukamilika kwa uhakiki huo, taarifa za watumishi hao zitatumwa katika ngazi husika serikalini.


MTANZANIA lilipita katika moja ya mbao za matangazo iliyopo katika jengo la utawala na kuona tangazo hilo ambalo limesainiwa na Mkurugenzi wa Utumishi, Makwaia Makani.


Kupitia tangazo hilo, Makani alisema uhakiki huo utafanyika kwa watumishi wote kupitia taarifa za kitambulisho cha Taifa (NIDA) na taarifa zilizopo katika Mfumo Shirikishi wa Taarifa za Kiutumishi na Mishahara (HCMIS).


Alisema uhakiki huo utaanza rasmi Julai 18, mwaka huu hadi Agosti 15, mwaka huu.


“Muhimbili itaendesha zoezi la uhakiki wa wafanyakazi wake wote kwa kutumia taarifa zilizopo katika kitambulisho cha Taifa pamoja na taarifa zilizopo katika mfumo wa LAWSON, ikiwa ni kutekeleza agizo la serikali,” alisisitiza.


Aliongeza “Uhakiki huo utafanyika katika darasa la komputa lililopo katika jengo la utawala. Katika kuhakikisha uhakiki huo unafanikiwa wafanyakazi wote wanatakiwa kuzingatia yafuatayo: kila mmoja awe na kitambulisho cha Taifa au namba ya kitambulisho chake.


“Kila mfanyakazi awe na kitambulisho cha kazi, wafanyakazi wote waliopo likizo yoyote ndani ya nchi wahakikishe wanafika na kuhakikiwa taarifa zao,” alisema.


Makani alisisitiza ni lazima watumishi wazingatie suala la nidhamu katika kipindi chote cha uhakiki huo.


“Aidha, wakurugenzi wakuu wa idara, vitengo, wakuu wa majengo na wodi zote, wanatakiwa kuhakikisha wafanyakazi wote walio chini yao wanahakikiwa bila kukosa,” alisisitiza.


Uhakiki huo unafanyika ikiwa ni siku chache tangu Muhimbili, kupitia Ofisa Uhusiano wake, Neema Mwangomo kueleza kuwa watumishi saba wa hospitali hiyo ambao awali walitajwa kuwa miongoni mwa watumishi waliokutwa na vyeti feki kushinda rufaa zao.


Katika uhakiki wa awali, jumla ya watumishi 134 walibainika kuwa na vyeti feki vya kitaaluma ambao walitakiwa kujiondoa wenyewe kazini kabla ya Mei 15, mwaka huu.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement