NA VERONICA ROMWALD – DAR ES SALAAM
ILI binadamu aweze kutimiza majukumu yake ya kila siku
ni lazima awe na afya njema, inapotokea ameugua huhitaji kupata tiba dhidi ya
ugonjwa unaomsumbua.
Kwa msingi huo, matibabu ni haki ya kila mtu ili aweze
kuwa tena na afya njema lakini matibabu hayo anayopatiwa ni lazima yawe sahihi.
Miaka ya nyuma huduma za matibabu zilikuwa zikitolewa
zaidi katika vituo vya afya, zahanati na hospitali zinazomilikiwa na serikali.
Baadae tukashuhudia mashirika ya dini na taasisi
mbalimbali nazo zikipata kibali cha kuanzisha huduma hizo za matibabu na hata
watu binafsi.
Wakili wa Mahakama Kuu Tanzania, Maulid Kikondo anasema
hali hiyo imepelekea baadhi ya wamiliki kutoa matibabu kwa lengo la kufanya kibiashara
zaidi kuliko kutoa huduma.
“Kwa kawaida mtu anapopatiwa matibabu huwa ni kwa nia
njema, lakini kama ilivyo kwa mambo mengine ingawa ni jambo jema lakini kuna
wakati matatizo mbalimbali huweza kujitokeza,” anasema.
Anasema matatizo hayo mara nyingi hujitokeza kati ya
mtoa huduma na mpokea huduma.
“Hii ni kwa sababu wamiliki wengi (wa hospitali na
vituo vya afya), wanatoa matibabu kwa lengo la kufanya biashara kuliko huduma,
wanapokuwa na element ya biashara maana yake ni kwamba wanafikiria zaidi kupata
faida.
“Unapokuwa na mfumo wa biashara kwenye matibabu huwezi
kuwakwepa wajanja wajanja, kwa sababu siku zote, wafanyabiashara hutaka
kutengeneza faida na hapa ndipo ‘yanapozaliwa’ matatizo.
“Kwa mfano unakuta mtu amekwenda hospitalini anajikuta
anaandikiwa vipimo vingi ambavyo vingine wala havihitaji na kupewa dawa nyingi,
kwa sababu mmiliki anahitaji kupata faida,” anabainisha.
Anasema ingawa si wamiliki
wote wenye nia hiyo lakini kati ya wale walio waamini wanaofanya kazi kwa
kuzingatia maadili wapo ambao hufanya kinyume.
“Miaka ya nyuma madaktari
wengi walikuwa wakisoma hapa nchini na walikuwa rahisi hata kufahamiana na
kujuana, tofauti na leo hii wengine wanasoma nje ya nchi na wanarudi kufanya
kazi nyumbani,” anasema.
Anasema wakati walipokuwa
wachache ilikuwa rahisi kujua na kukosoana pale ambapo mwenzao anakuwa amefanya
makosa katika kutoa matibabu tofauti na sasa.
Anasema kutokana na hali hiyo ni muhimu sasa jamii
kuanza kujifunza, kuifahamu na kuielewa vema sheria ya matibabu.
“Kutokana na matatizo ya ki-matibabu yanayoweza
kujitokeza kati ya mtoa huduma na mpokea huduma, kilitengenezwa kipengele
maalumu cha sheria kwa lengo la kuyatatua,” anasema.
Wakili huyo anafafanua “Wataalamu wa sheria walitengeneza
‘Medical legal’ ambayo baadae ilitumika kutengeneza kipengele cha ‘medical
Negligence ambacho kazi yake ni kushughulika na haki za wagonjwa.
“Yaani inapotokea mgonjwa amepata madhara yoyote wakati
akipatiwa matibabu, kipengele hicho kinaeleza nani ambaye anawajibika kwa
madhara hayo,” anabainisha.
Anaongeza “Kipengele hicho cha sheria kilitengenezwa
makusudi, ili kulinda haki za mgonjwa, inaeleza wazi wakati gani daktari
anapaswa kuwajibika pale ambapo inatokea anatoa matibabu kinyume na taratibu
zilizowekwa.
Anasema hivyo sheria hiyo lengo lake kuu ni kusimamia
na kulinda haki za mgonjwa kuhakikisha kwamba anapatiwa matibabu sahihi
yanayostahili.
Jinsi
inavyofanya kazi
Anasema jambo ambalo kila mtu anapaswa kulijua ni
kwamba daktari anapaswa kupata idhini ya mgonjwa kabla ya kumpatia matibabu.
“Ili daktari awe na haki ya kutoa matibabu ni lazima
pawe na idhini ya mgonjwa, mgonjwa aridhie mwenyewe na kabla ya kuridhia
kutibiwa lazima pawe na majadiliano.
“Kwamba daktari anapaswa kumueleza kwa kina mgonjwa kwa
mfano juu ya faida na madhara ya matibabu (dawa) au sindano atakayochomwa,”
anasema.
Anaongeza “Lazima daktari amueleze mgonjwa ili aridhie
mwenyewe iwapo apatiwe matibabu kwa dawa au sindano ambayo (daktari)
amependekeza.
“Na mgonjwa anakuwa tayari anaelewa kwamba ingawa hiyo
anayopatiwa ni tiba lakini labda inaweza kumsababisha athari nyingine kwenye
mwili kwa mfano itapelekea figo zake kushindwa kufanya kazi baadae katika
maisha yake na mambo mengineyo,” anasema.
Anaongeza “Lakini hapa kwenye idhini ya mgonjwa wakati
mwingine huwa kuna utata, wapo watu ambao hudhani kwamba mgonjwa akisema sawa
huku akiwa hajaelezwa faida na madhara ya matibabu anayopewa ni sahihi jambo
ambalo si sawa.
“Sheria inataka lazima pawe na ‘informed concept’,
mgonjwa lazima aelezwe na aelewe hasa huduma anayokwenda kupatiwa ni ipi ili
atoe idhini yake,” anasema.
Anasema inapotokea kwa bahati mbaya kwamba mgonjwa
ndiye ambaye amesaini fomu ya matibabu na hakukuwa na majadiliano ya kutosha
kuelezwa juu ya kile anachokubaliana, iwapo atapata madhara moja kwa moja
daktari aliyempatia huduma anaweza kushtakiwa kwa mujibu wa sheria hiyo.
“Madaktari wanaifahamu vema sheria hii na wengi wapo
makini katika utendaji wao na ndiyo maana kabla ya kumuhudumia mgonjwa hufanya
majadiliano kwa sababu akienda kinyume anaweza kushtakiwa kwa sheria hii,”
anasema.
Anaongeza “Hata kabla
daktari hajakuchoma sindano lazima akueleweshe kwa kina juu ya matibabu hayo na
wewe mwenyewe uamue akutibu au la.
Anasema watu wengi
wamekuwa wakipatiwa matibabu yasiyo sahihi na kuishia kupata madhara hata hivyo
kwa kuwa hawana uelewa wowote kuhusu sheria hiyo wamekuwa wakiugulia majumbani
mwao.
“Uelewa wa watanzania kuhusu
sheria hii ni mdogo mno, wengi wanapata madhara na hawajui kwamba wanaweza
kupata haki yao kwa kushtaki mahakamani, kesi zinazokuja mahakamani ni chache
mno, mataifa yaliyoendelea wanaitumia sheria hii kudai haki zao,” anabainisha.
Lazima
uandaliwe kisaikolojia
Wakili maulid Kikondo anasema
ingawa sheria inatambua kwamba mgonjwa anapochukua uamuzi wa kukaa mbele ya
daktari ni hatua ya kuridhia pia lakini kuna matibabu ambayo daktari anapaswa
kumuandaa kisaikolojia mgonjwa kabla ya kumtibu.
“Kwa mfano mgonjwa ni wa
jinsi ya kike na daktari ni mwanamume ikiwa itabidi avue nguo kwa mfano ili
atibiwe ni lazima daktari amueleze mapema ili ajiandae kisaikolojia,” anasema.
Anasema kwa kuwa mgonjwa
ana haki na maisha yake ataamua mwenye iwapo apatiwe matibabu hayo au la na
kwamba daktari hapaswi kumlazimisha.
Matibabu
kwa mtoto
Anasema ni makosa daktari kumtibu mtoto aliye chini ya
umri wa miaka 18 kabla ya kupata idhini kutoka kwa wazazi au walezi wake.
“Ndiyo maana kabla ya kumfanyia matibabu yoyote mtoto
chini ya miaka 18 lazima wazazi wake waitwe, wao watatoa idhini kwa niaba
yake,” anafafanua.
Mgonjwa
aliyezidiwa
Wakili huyo anasema taaluma inampatia haki daktari
kumsaidia na kumuhudumia mgonjwa aliye katika hali mbaya ambayo inaweza
kupelekea kupoteza maisha bila kusubiri idhini yake.
“Yaani kwa mfano, mtu amepata ajali na kufikishwa
haraka hospitalini, daktari ana haki ya kumsaidia bila kusubiri majadiliano na
idhini ya mgonjwa, lakini anachopaswa kufanya (daktari) ni kutibu tatizo lilompelekea
mgonjwa kufikishwa hospitalini.
“Kwamba labda anajeraha linatoka damu nyingi, atatibu
jeraha hilo pekee ikiwa mgonjwa huyo ana tatizo jingine kwa mfano aliwahi kuumia
jicho lake huko miaka ya nyuma, daktari hana haki kumtibu kwa wakati huo kwa
sababu mgonjwa hajaridhia,” anasema.
Sheria
msumeno
Anasema wakati sheria hiyo
ikilinda haki za mgonjwa wakati mwingine pia hulinda haki za daktari
anayempatia matibabu.
“Kwa mfano, daktari
amepokea majeruhi wa ajali amempatia huduma lakini kwa bahati mbaya majeruhi
huyo akafariki dunia na ndugu wakalalamika kwamba daktari amesababisha kifo cha
ndugu yao.
“Tutasikiliza maelezo ya
pande zote mbili, ikiwa mgonjwa huyo alifariki wakati daktari akitimiza wajibu
wake wa kumsaidia kuokoa maisha kwa kutibu tatizo lililokuwa likihatarisha uhai
wake, basi daktari husika anakuwa huru.
“Lakini ikiwa mgonjwa
alifariki wakati daktari akitibu tatizo jingine ambalo halihusiani na ajali
hiyo, bila idhini ya mgonjwa hapo daktari anakuwa matatani na atahukumiwa kwa
mujibu wa sheria,” anafafanua.
Makala haya kwa mara ya kwanza yamechapishwa Agosti 31, mwaka huu kwenye gazeti la MTANZANIA
Makala haya kwa mara ya kwanza yamechapishwa Agosti 31, mwaka huu kwenye gazeti la MTANZANIA
Chapisha Maoni