Wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wametakiwa kufanya kazi kwa kujituma, kuongeza ufanisi na kutoa huduma bora kwa wagonjwa ili epukana na malalamiko yanayoweza kujitokeza.
Rai hiyo imetolewa leo
na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi hiyo Prof. Mohamed Janabi wakati akizungumza
katika kikao cha wafanyakazi kilichofanyika jijini Dar es Salaam.
Prof. Janabi pia aliwahimiza
wafanyakazi wa Taasisi hiyo kuendelea
kutunza vizuri kumbukumbu mbalimbali zikiwemo za wagonjwa na utendaji wa kazi zao
za kila siku ili pale zitakapohitajika zipatikane kwa haraka.
“Mjitahidi kujaza fomu ya
wazi ya mapitio na upimaji utendaji kazi (OPRAS) kwa wakati ili kusiwe na
malalamiko ya upandaji wa vyeo kwani ujazaji wa fomu hizo ndiyo unaowezesha mfanyakazi
kupimwa utendaji wake kwa kipindi cha mwaka mzima”, alihimiza Mkurugenzi
Mtendaji huyo.
Kwa upande wake
Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali Kuu na Afya (TUGHE) Godfrey
Tamba aliupongeza uongozi wa Taasisi hiyo kwa kazi wanayoifanya ya kuhakikisha wafanyakazi
wanafanya kazi zao katika mazingira bora.
Tamba alisisitiza, “Wafanyakazi
wenzangu tunaodai haki zetu tukumbuke kutimiza wajibu wetu wa kazi kwa wakati,
kwani uongozi wa TUGHE hautawatetea watu ambao hawatimizi wajibu wao ipasavyo”.
Hiki ni kikao cha pili
cha wafanyakazi wote kufanyika tangu kuanza kwa mwaka huu ambapo katika kikao hicho
mambo mbalimbali yalijadiliwa ikiwa ni pamoja na kuongeza ufanisi katika
utendaji wa kazi.
Chapisha Maoni