Picha na mtandao
NA VERONICA ROMWALD – DAR ES SALAAM
TANGU siku sifuri hadi miezi tisa ya ujauzito, mtoto
hutegemea kupokea vitu vyote muhimu kwa ajili ya ukuaji wake kuanzia chakula
(virutubisho), hewa, maji na vinginevyo kutoka kwa mama yake kupitia kondo la
nyuma.
Kisayansi kondo la
nyuma ndiyo kiunganishi pekee kinachowaunganisha mama na mtoto katika kipindi
chote cha ujauzito.
Wataalamu wa afya wanasema ni muhimu mno kwa mjamzito
kuhudhuria kliniki katika kipindi chote cha ujauzito wake.
Kliniki ndipo sehemu pekee ambako mjamzito hufanyiwa uchunguzi wa kina na wataalamu wa
afya kufuatilia maendeleo ya mtoto wake aliyepo tumboni mwake.
Aidha, huko hupatiwa matibabu na ushauri sahihi inapobidi
ili kumuwezesha kujifungua mtoto mwenye afya njema na uzito unaostahili.
Mara kadhaa imepata kutokea katika baadhi ya maeneo, watoto
kuzaliwa na kugundulika kuwa na maambukizi ya malaria kali, hali
inayowashangaza wengi.
Daktari Sigsbert Mkude ambaye pia ni Mkuu wa Kitengo cha Uchunguzi na
Matibabu, Mpango wa Taifa wa Kudhibiti Malaria nchini, na hapa anafafanua
kuhusu suala hilo katika makala haya (karibu, soma uelimike).
“Kisayansi mtoto anaweza kuzaliwa akiwa na ugonjwa wa
malaria kitaalamu inaitwa ‘congenital malaria’, lakini jambo hilo huwa ni nadra
sana kutokea,” anabainisha
Anasema ni nadra kutokea kwa sababu katika kondo la nyuma
la mama kuna njia mbalimbali za kinga za asili ambazo humkinga mtoto aliyepo
tumboni kupata ugonjwa huo.
“Mama anapokuwa na maambukizi kwenye kondo la nyuma, vimelea
vya malaria hutumia mwanya huo kwa kusafiri kupitia kondo la nyuma kutoka kwa
mama kwenda kwa mtoto,” anabainisha.
Anasema inapotokea hali hiyo ndipo pale mtoto huzaliwa
akiwa tayari ameambukizwa malaria kali.
“Ndiyo maana tunahamasisha kina mama wafike kliniki, hata
kama hana dalili tukimpima kwa kipimo cha MRDT tukakuta ana vimelea vya malaria
tunampatia dawa mapema ili kuzuia asimuambukize mtoto wake aliye tumboni,”
anafafanua.
Dk. Mkude (pichani) anasisitiza mjamzito anapowahi mapema kliniki tunampatia
chandarua chenye dawa ili kumkinga dhidi ya mbu waenezao malaria na
anapogundulika kuwa na malaria tunampa dawa ili kuangamiza vimelea vya malaria.
Baada
ya kuzaliwa
Anaongeza “Tunasisitiza mjamzito kuhudhuria kliniki kwa
matibabu kwa sababu katika kipindi cha mwezi wa kwanza tangu mtoto kuzaliwa
mara nyingi magonjwa anayoyapata huwa ni ya maambukizi na hupitia kwenye
kitovu.
“Katika ule mwezi wa kwanza ikitokea kwa bahati mbaya
kitovu chake kikachafua, kama kitovu hakijafunga vizuri kunakuwa na uhusiano mkubwa wa kitovu na mishipa
yake ya damu ikiwa atapata ugonjwa huugua mno,” anasema.
Anasema hata hivyo mara nyingi watoto wadogo huwa
hawaoneshi dalili ya homa na kwamba wakati mwingine huwa wanakuwa baridi au
hushindwa kunyonya.
“Akipata maambukizi kupitia kitovu mara nyingi wengine
hutokwa vipele katika eneo la shingoni, hivyo ni muhimu mama kuhudhuria
kliniki,” anasema.
Hali ipoje
nchini
Dk. Mkude anasema tafiti zinazoendelea kufanyika nchini
tangu mwaka 2000 hadi sasa zinaonesha kiwango cha maambukizi ya malaria
kinazidi kupungua.
“Tangu mwaka 2000 hadi sasa kiwango cha maambukizi ya
malaria kimepungua hadi asilimia 30, na idadi ya vifo imepungua kwa kiwango cha
asilimia 33 na 34 katika kipindi hicho,” anasema.
Anasema mahudhuria ya wagonjwa katika vituo vya kutolea
huduma za afya kwa mwaka ni kati ya wagonjwa milioni 10 hadi 12.
“Hawa ni wale ambao hufika kutibiwa na kuondoka nyumbani,
malaria husababisha vifo vya takriban watu 5,000 kila mwaka nchini sawa na
asilimia 30,” anabainisha.
Kundi
lililopo hatarini
Anasema tafiti zinaonesha wananchi wenye kipato cha chini
ndio ambao wengi hupata maambukizi ya ugonjwa huo kuliko wale ambao wana kipato
kizuri.
“Zaidi ya asilimia 90 wanaishi kwenye maeneo yenye
maambukizi ya malaria, ukitazama hali ya maambukizi ya ugonjwa huu kwa mfano kwenye
eneo kama Mikocheni unaweza kukuta mtoto mmoja kati ya watoto 100 anaugua
malaria lakini Vingunguti na Buguruni hali inakuwa kinyume chake,” anasema.
Anasema katika miaka ya hivi karibu takwimu zinaonesha
idadi ya vifo vya watoto walio chini ya miaka mitano kutokana na ugonjwa huo
zinaonekana kupungua.
“Katika kipindi cha mwaka 2006 hadi 2010 malaria ndiyo
ugonjwa ambao ulikuwa unaongoza kwa vifo lakini tangu mwaka 2010 hadi sasa kuna
magonjwa mengine yameibuka kwa mfano magonjwa ya njia ya hewa tunaona yamepiku
ugonjwa wa malaria.
“Mwaka 2015 NIMR walifanya utafiti ambao ulionesha kwamba
idadi ya vifo vitokanavyo na malaria vinapungua lakini bado ugonjwa huu ni miongoni mwa
magonjwa yanayosababisha vifo vya watu wengi,” anasema.
Mbu anayeeneza malaria
Idadi
ya maambukizi kimkoa
Dk. Mkude anaitaja mikoa yenye kiwango kikubwa cha Katavi,
Mwanza, Shinyanga, Tabora na Simiyu.
“Lakini kwa miaka 15 sasa kiwango vya maambukizi kimepungua
kwa asilimia zaidi ya 50 ingawa mikoa yenye maambukizi ya malaria inaonekana
kuongezeka,” anasema.
Anasema takwimu za mwaka 2016 zinaonesha asilimia 6.0 ya watu
maskini wapo katika maambukizi kuliko wenye uwezo mkubwa kifedha ambao kiwango
cha maambukizi ni asilimia 1.0.
“Hii inamaanisha kwamba makazi bora yaliyojengwa katika
mpangilio mzuri hasa katika miji mikubwa inasaidia kupunguza kiwango cha
maambukizi ya malaria kuliko maeneo yenye makazi duni,” anabainisha.
Anataja mikoa yenye kiwango kidogo cha maambukizi ni Dar es
Salaam, Iringa, Pwani, Kilimanjaro, Njombe, Songwe na Ruvuma.
Changamoto
Mkurugenzi wa Kitengo cha Udhibiti Mbu Waenezao Malaria wa
Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk. Charles
Mwalimu anasema ingawa chandarua ni njia rahisi na bora kujikinga dhidi ya mbu
waenezao malaria hata hivyo wapo watu kwenye jamii huogopa kuvitumia.
“Kuna imani potofu ambazo zimejengeka huko kwenye jamii,
baadhi ya wanaume wamekuwa wakikataa kulala kwenye vyandarua eti watapata
tatizo la upungufu wa nguvu za kiume,” anasema.
Anaongeza “Wengine wanaogopa kulala kwenye chandarua eti
wakilala wanaona ni kama wapo kwenye jeneza au wengine wakivihusisha na imani
za freemason, jambo ambalo halina uhusiano
hata kidogo.
“Hakuna utafiti wowote uliowahi kufanyika kuthibitisha
kwamba chandarua kinasababisha upungufu wa nguvu za kiume, kilichothibitishwa
ni kwamba humpatia mtu usingizi mnono kwa sababu mbu huwa hawamfikii na
kumsabishia usumbufu wa aina yoyote,” anabainisha.
Anasema vyandarua vinavyogawiwa kwa wananchi
vimethibitishwa na Shirika la Afya Duniani (WHO) na na Taasisi ya Usajili wa
Viuatilifu katika Kanda za Joto (TPRI) kuwa ni salama.
“Lengo la Serikali ni kuhakikisha inalinda afya za wananchi
wake na si kuwaangamiza,” anasisitiza.
Mtaalamu akipuliza dawa ukoko ndani ya nyumba (picha na mtandao)
Mkakati
maalumu
“Wizara tumejipanga kufanya kampeni nyingine kubwa ya
kusambaza vyandarua mapema mwakani katika mikoa yote 26 ili kuendeleza mapambano
dhidi ya ugonjwa wa malaria,” anasema.
Anaongeza “Tumeshapokea fedha kutoka, Mfuko wa Dunia wa
kukabiliana na Ukimwi, Malaria na Kifua Kikuu,
tutaanza na mikoa mikoa 11 ambako tutagawa vyandarua takriban milioni 15.
“Lengo letu ni kuhakikisha kila chandarua kimoja kinatumika
na angalau watu wawili ndani ya familia, tunawasihi wananchi tutakapokuwa
tunakwenda wawe tayari kuvipokea vyandarua hivyo na kuvitumia ili kwa pamoja
tuweze kutokomeza malaria nchini,” anatoa rai.
Unayopaswa kufahamu
Malaria
ni ugonjwa unaosababishwa na vimelea viitwavyo Plasmodia ambavyo hungia katika mfumo wa damu mwilini
baada ya mtu kuumwa na mbu jike aitwaye Anopheles
anayekuwa amebeba vimelea hivyo.
Wataalamu
wa afya wanaeleza kwamba vimelea hivyo vinapoingia mwilini, vimelea hivyo
huenda katika chembe za ini la binadamu na kuanza kuzaliana, wakati chembe za
ini zinapopasuka, huruhusu vimelea hivyo ambavyo huenda kushambulia chembe
nyekundu za damu yake.
Wanasema
huko vimelea hivyo huzidi kuongezeka na wakati chembe nyekundu za damu
zinapopasuka huruhusu vimelea ambavyo huenda hushambulia kwa wingi zaidi chembe
nyekundu za damu.
Wanasema
mzunguko wa chembe nyekundu za damu unapovamiwa na mipasuko hiyo huendelea hatimaye
mtu huanza kuonesha dalili za malaria kila baada ya chembe hizo kupasuka.
Kwa
mujibu wa wataalamu, mtu huuanza kuhisi homa, baridi, kutokwa jasho jingi,
maumivu ya kichwa na mwili, kichefuchefu na hata kutapika, dalili hizo huanza
kuonekana baada ya saa 48 hadi 72,
ikitegemea aina ya vimelea na muda
ambao mtu amekuwa na ugonjwa.
Shirika
la Afya Duniani (WHO) mwaka 2013 lilikadiria zaidi ya watu milioni 198,
waliambukizwa malaria na kwamba watu 584,000 walifariki dunia kutokana na
ugonjwa huo.
WHO
ilieleza karibu watu wanne hadi watano waliofariki dunia ni watoto walio chini
ya umri wa miaka mitano, ugonjwa huo unatishia mamia ya nchi na maeneo
mbalimbali ulimwenguni kwani watu bilioni 3.2 wanakabili hatari ya
kuambukizwa.
Jinsi
ya kujikinga
Kwa kuhakikisha unatumia chandarua kilichowekwa dawa
ya kuua mbu hao waenezao malaria, ambacho hakijatoboka na unapaswa kukichomeka
vizuri kwenye godoro lako.
Ni vema ukapuliza dawa ya kuua wadudu ndani ya
nyumba yako mara kwa mara kabla ya kulala na ikiwezekana weka wavu wa kuzuia
wadudu katika madirisha na milango yako ili kudhibiti mbu kuingia ndani ya
nyumba yako.
Vaa nguo zinazofunika vema mwili wako hasa nyakati
za jioni na usiku ambapo mbu huzunguka zunguka na inapowezekana epuka kuwa
katika maeneo yenye mbu wengi kwa mfano mabwawa, maji yaliyotuama au mahala
ambapo mbu huzaliana.
Ikiwa umeanza kuona dalili za malaria wahi mapema
hospitalini kupata matibabu haraka.
Makala haya kwa mara ya kwanza yalitoka Septemba 21, mwaka huu kwenye gazeti la MTANZANIA
Chapisha Maoni