KITENDO
cha mwanamke kutumia taulo ya kike kwa muda mrefu kujihifadhi wakati wa kipindi
cha hedhi pasipo kubadilisha, kunaweza kumsababishia kupata magonjwa mbalimbali
yakiwamo ya moyo.
Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo wa Taasisi ya Jakaya
Kikwete, Bashir Nyangasa amesema hayo alipozungumza na waandishi wa habari kuhusu
maadhimisho ya siku ya moyo duniani, yanayofanyika Septemba 29, kila
mwaka (leo).
“Kipindi
cha hedhi ni muhimu mwanamke awe msafi ahakikishe anabadilisha ile pedi
anayotumia kujihifadhi na si kukaa nayo kwa muda mrefu, ni hatari.
“Unapokaa
na pedi kwa muda mrefu, ile damu ikajaa pale hutengeneza bakteria (wadudu),
hapo unahatari ya kupata maambukizi kwenye kizazi, wale wadudu wanaweza
kusafiri kwenda kuathiri moyo au figo zako,” amesema.
Dk. Nyangasa (anayezungumza pichani) ameongeza
“Hiyo tunaita ‘entry point’ yaani hata ukijikata wadudu wanaweza kusafiri
kwenda kwenye moyo wako na kuuathiri, hivyo ni muhimu kuzingatia usafi katika
kipindi hicho.
Naye, Daktari Bingwa wa Magonjwa ya
Moyo wa Taasisi hiyo, Tulizo Shemu ametoa wito kwa wakazi wa jiji la Dar es Salaam
na maeneo jirani kujitokeza kwa wingi, kufika katika Taasisi hiyo hii leo.
“Tutafanya upimaji bure na tutatoa
elimu ya lishe, jinsi ya kujikinga na magonjwa ya moyo, kuanzia saa mbili hadi
saa 10 jioni bila gharama yoyote,” amesisitiza.
Ameongeza “Kuanzia Septemba 25 hadi 29,
mwaka huu tayari tumewafanyia upasuaji wagonjwa 23 kwa kushirikiana na
madaktari wenzetu kutoka Taasisi ya Madaktari Afrika, JKCI tunafanya
maadhimisho haya kwa kushirikiana pia na Chama cha Madaktari wa Moyo Tanzania
(THF).
“Wananchi watapimwa urefu, uzito,
shinikizo la damu (BP), sukari na kupewa ushauri. Kwa wale watakaokutwa
na matatizo ya moyo watafanyiwa uchunguzi zaidi na kupatiwa matibabu. Kauli
mbiu ya siku hii ni: “Moyo wenye Afya”,” amebainisha.
Chapisha Maoni