Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement

https://www.pantai.com.my/UploadedImage/Content_Blurb/manjung/other-specialties.jpgPicha kwa hisani ya mtandao

-Mapendekezo yao kuwezesha uandaaji mpango kazi wa Kitaifa, Afya kwa vijana
 
NA VERONICA ROMWALD –DAR ES SALAAM

MWILI wa binadamu wakati mwingine unaweza kuufananisha na gari, mara nyingi  gari linapoendeshwa kwa muda barabarani huhitaji kufanyiwa matengenezo ya kina.

Ndiyo maana hupelekwa kwa mafundi (gereji) kwa ajili ya matengenezo, kadhalika binadamu kuna wakati huugua na hivyo kuhitaji matibabu dhidi ya ugonjwa unaomsumbua.

Huenda ama hospitali, zahanati au kituo chochote cha afya ambako hukutana na wataalamu wanaoweza kumpatia matibabu sahihi dhidi ya ugonjwa unaomsumbua.

Lakini si mara zote tunakwenda huko kwa matibabu pekee, wakati mwingine huwa tunahitaji kwenda kwa ajili ya kupata ushauri wa kitaalamu unaoweza kutusaidia kuishi vema ili kujikinga na maambukizi ya magonjwa mbalimbali.

Licha ya umuhimu huo, vijana wengi hawana mwamko wa kwenda hospitalini, zahanati au vituo vya afya ama kupima afya zao au kupata ushauri.

Kwanini

Hivi karibuni MATUKIONAMAISHA lilipata nafasi kuhudhuria Mkutano wa Kitaifa wa Vijana wa Afya na Maendeleo uliofanyika katika ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa Julius Nyerere.

Mkutano huo ambao ni wa kwanza kufanyika nchini uliandaliwa na Shirika lisilo la Kiserikali la Save the Children kwa kushirikiana na serikali.
Vijana wakimsikiliza kwa makini mwezeshaji wakati wa mkutano huo, picha kwa hisani ya mtandao wa Save the Children

Pamoja na mambo mengine, lengo kuu lilikuwa kujadili kwa kina changamoto zinazowakabili vijana hasa katika sekta ya afya.

Ulihusisha washiriki zaidi ya 100 kutoka Tanzania Bara na Visiwani ambao walipata fursa ya kuchangia mawazo yatakayosaidia baadae serikali kutengeneza mpango kazi wa afya kwa vijana nchini.

Sabinius Paulo, mkazi wa Iringa ni miongoni mwa vijana walioshiriki mkutano huo, anasema kuna vikwazo vingi ambavyo vijana hukumbana navyo vinavyowakatisha tamaa kutafuta huduma sahihi za matibabu na ushauri.

“Changamoto zaidi inakuja pale kijana anapohitaji kupata taarifa sahihi kuhusu afya ya uzazi na ujinsia hakuna huduma rafiki hali inayowakatisha tamaa vijana wengi,” anasema.
"Madawa ya kulevya yana madhara kiafya na hupunguza uwezo wa kufanya kazi." - Dr. Cassian

Anasema vijana wanaoathirika zaidi na hali hiyo ni wale walioko katika maeneo ya vijijini kuliko wale walioko katika maeneo ya mijini.

“Mijini kuna fursa nyingi ambazo kijana anaweza kuzitumia kupata taarifa sahihi juu ya afya ya uzazi na ujinsia, kule kijijini unaweza kukutana na kijana ambaye haelewi chochote kwa mfano kuhusu huduma za uzazi wa mpango,” anasema.

Anasema lugha inayotumika pia wakati mwingine huwa ni kikwazo kufikisha ujumbe unaokusudiwa kuwaelimisha vijana walioko maeneo ya vijijini.

“Unaweza kukuta kipeperushi kimeandikwa kwa lugha ama ya Kiswahili au ya kiingereza, kwa kule vijijini inakuwa vizuri zaidi kutumia lugha zao ili kufikisha ujumbe kwa haraka zaidi,” anabainisha.

Paulo anasema kutokana na idadi kubwa ya vijana kushindwa kupata huduma rafiki za matibabu na taarifa sahihi juu ya afya ya uzazi kumechangia ongezeko kubwa la ndoa na mimba za utotoni.

“Ni tatizo kubwa, vijana wanatamani kupata taarifa sahihi lakini hawazipati kwa sababu hakuna huduma rafiki, nimefurahi kupata bahati kuhudhuria mkutano huu na naamini kile nilichokiwasilisha serikali itakifanyia kazi ili kukabiliana na hali hiyo,” anasema.

Changamoto kwa walemavu

Dorice Charles (pichani) ni miongoni mwa vijana ambao hawapo tayari kwenda hospitalini, zahanati wala kituo cha afya kilichothibitishwa kufuata matibabu ya kibingwa.

Akisimulia, Dorive anasema “Sikuzaliwa na ulemavu wa aina yoyote ile, mwaka 2004 nikiwa darasa la tatu niliugua homa kali sana nikatibiwa kwa dozi ya quinine ambayo ilinisababishia ulemavu wa kusikia.

“Hali hiyo ilinilazimu kuacha masomo kwa muda mrefu, nilirudi shuleni mwaka 2006 wanafunzi wenzangu wakawa wananitani nimekuwa kiziwi, uwezo wangu darasani nao ulishuka kwa kiwango kikubwa,” anasimulia.

Anasema hata hivyo aliendelea kujifunza licha ya changamoto nyingi alizokabiliana nazo hadi akafanikiwa kumaliza darasa la saba na kuchaguliwa kujiunga Sekondari.

“Mazingira yalikuwa magumu kwangu, miundombinu haikuwa rafiki, walimu hawakuwa na uwezo wa kufundisha lugha ya alama, nilipohitimu kidato cha nne nilifaulu kwa alama D somo la Kiswahili peke yake,” anasema.

Dorice anaongeza “Kuna siku nilijihisi mgonjwa, nikaenda hospitalini lakini daktari niliyemkuta alinibagua kwa kuwa mimi ni mlemavu, masikio yangu hayana uwezo wa kusikia (kiziwi).

Anasema siku hiyo aliwahi mapema hospitalini hapo lakini daktari aliyemkuta alimtaka akae kwenye benchi kwanza ili awatibu wagonjwa wengine ambao walikuwa na uwezo wa kusikia.

“Nilikaa pale kwenye benchi kwa muda mrefu sana, mwisho muda wa kazi ulikwisha, yule daktari akatoka na kuondoka zake, mimi nikiwa nimebaki pale pale, nikahuzunika mno, nikarudi zangu nyumbani,” anasema.

Anasema tangu wakati huo hadi sasa hayupo tayari kwenda huko kutibiwa badala yake kila anapojihisi kuwa ni mgonjwa huenda mwenyewe kwenye duka la dawa na kununua ile anayoona inamfaa na kujitibu nyumbani.
 
Mlezi

Mwanzilishi wa Kituo Maalumu cha Kusaidia Watoto wenye Ulemavu mkoani Mara, Mwalimu Wilfred Serikali (anayezungumza pichani) anasema watoto wenye ulemavu wengi wanakosa huduma zile wanazostahili.

“Mara nyingi jamii inawaacha peke yao, hawapewi taarifa sahihi juu ya ukuaji wa miili yao na elimu ya afya ya uzazi kwa ujumla ili wajitambue, wengi wamejikuta wakiishia katika mikono ya watu wasio na ni njema.

“Unakuta tayari mtoto ni mjamzito na ukimuhoji utagundua hana taarifa yoyote kuhusu afya ya uzazi na ujinsia, wazazi au walezi hawawaelezi ukweli watoto wao jambo ambalo linahatarisha afya na maendeleo yao,” anabainisha.

Kundi muhimu

RIPOTI iliyotolewa na Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Idadi ya Watu (UNFPA) ya mwaka 2014 inaonesha idadi ya vijana inakadiriwa kuwa watu  bilioni 1.8 kati ya watu bilioni 7.5 duniani.

Takwimu za Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2012 iliyofanywa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) inaonesha idadi ya vijana inakadiriwa kuwa zaidi ya watu milioni 16.2 kati ya watu milioni 44 nchini.

Hii inaonesha wazi kwamba kundi la vijana ndilo lenye idadi kubwa ya watu si Tanzania pekee bali duniani kote.

Vijana ni nguvu kazi ya Taifa lolote linalohitaji kupata maendeleo na ili itumike vema katika shughuli za maendeleo ni lazima wawe na afya njema.
Vijana wakiendelea kujadili

Ni haki ya kila raia pia (si vijana tu) kuwa na afya njema kwani hapo mtu huweza kuutumia muda wake ipasavyo katika shughuli za kiuchumi kwa faida yake, familia yake na Taifa kwa ujumla.

Ndiyo maana katika ajenda ya maendeleo endelevu ya millennia (SDGs) lengo namba tatu kati ya malengo 17 yaliyopitishwa na Umoja wa Mataifa (UN), linasisitiza juu ya kuhakikisha afya bora na kukuza maisha bora kwa watu wote na wa rika zote.

Mwakilishi wa YUNA

Mwakilishi wa Asasi za Vijana wa Umoja wa Mataifa (YUNA-Tanzania), Rahim Nasser (pichani) anasema vijana wana nafasi kubwa ya kushiriki katika kutekeleza malengo endelevu ya millennia (SDGs).

“Tunajitambua, tunafahamu tunachohitaji, dunia ipo katika mikono salama ya vijana, tukipewa nafasi, tunashukuru Save the Children wametuweka pamoja, tumechagua na kujadili kwa kina  lengo namba tatu.

“Kimsingi, vijana tunahitaji kupata taarifa sahihi kuhusu afya, kwa maendeleo yetu, Taifa na dunia kwa ujumla,” anasema.

Maandalizi ya mpango

Mkurugenzi wa uhamasishaji na habari wa Tume ya Kudhibiti Ukimwi, (TACAIDS), Jumanne Isango anasema kwa muda mrefu kumekuwa na pengo  kubwa katika kuwahusisha vijana kwenye shughuli ambazo zinawalenga wao moja kwa moja.

“Hasa katika suala la afya na maendeleo, mara nyingi ushiriki wao umekuwa hautoshelezi, ndiyo maana tuliona vema tuwalete pamoja wawakilishi kutoka mikoa yote ili tujadili na kupata mapendekezo kutoka kwao,” anasema.

Anasema mapendekezo yaliyotolewa na vijana hao yataiwezesha serikali kuandaa mpango kazi wa kitaifa wa vijana utakaojumuisha masuala yote yahusuyo afya.

“Kwa mfano kuhusu afya ya uzazi, elimu juu ya ugonjwa wa Ukimwi, uzazi wa mpango kwa vijana na masuala mengine mengi. Tunakwenda kuyapitia mapendekezo haya na tunakusudia baada ya mwezi mmoja hadi miwili tuwe tumekamilisha kazi hiyo,” anabainisha.

Isango anaongeza “Vijana wamewasilisha mapendekezo mengi mazuri kwa mustakabali wa Taifa letu, tunazungumza kuhusu malengo endelevu ya dunia (SDG’s) ambayo yanasisitiza upatikanaji wa maji safi, elimu, afya na haki nyinginezo za msingi.

“Hivyo kwa kuandaa mpango huo utatusaidia kujipima kila mwaka kwa kufanya tathmini wapi tulipotoka, tulipo na tunakwenda kufikia malengo hayo,” anafafanua.
Kauli ya serikali

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Watu wenye Ulemavu, Jenista Mhagama (pichani) anasema serikali inatambua umuhimu wa kundi la vijana.

“Ipo wazi kwamba kundi hili ndilo lenye idadi kubwa ya watu nchini kuliko makundi mengine, tunazungumzia kuelekea uchumi wa kati na Tanzania ya Viwanda tunahitaji nguvu kazi hii tuitumie ipasavyo.

“Lakini ni lazima wawe na afya imara, tunajivunia kwamba vijana wengi wana ujuzi wa kutosha ingawa wengi walijifunza katika mfumo usio rasmi lakini tumeanza jitihada za kuwarasimisha shughuli zao ili tuwatambue,” anasema.

Anasema tayari serikali imeingia makubaliano na Chuo cha  Mafunzo na Ufundi Stadi (VETA) kuwapa ujuzi rasmi na kisha kuwarasimisha vijana wenye ujuzi ambao waliupata katika mfumo usio rasmi.

Anaongeza “Serikali ipo tayari kuwasikiliza vijana, tupo tayari kupokea mawazo yao wakati wowote ili kwa pamoja tuweze kufikia lengo namba tatu la malengo endelevu ya millennia.

Anasisitiza kwamba ndiyo maana ilipitisha sheria namba 12 ya mwaka 2015 juu ya uanzishwaji wa Mabaraza ya vijana ili washiriki katika kutoa maoni yao moja kwa moja kwa serikali kuanzia ngazi ya kijiji hadi Taifa.

“Tayari tumekamilisha uandaaji wa kanuni kwa ajili ya uanzishwaji wa baraza, lengo ni kuwaunganisha vijana na kuwaleta pamoja na serikali yao kwa malengo yao na Taifa kwa ujumla,” anabainisha.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement