Na Veronica Romwald, Dar es Salaam
SERIKALI imewatoa hofu wanawake nchini juu ya uvumi
wa kuwapo kwa sidiria zinazodaiwa kupandikizwa majimaji yanayosababisha
saratani ya matiti.
Kauli hiyo ilitolewa jana na Kaimu Mratibu Program
ya Saratani ya Via vya Uzazi wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia,
Wazee na Watoto, Dk. Safina Yuna alipozungumza na MTANZANIA Jumamosi katika
mahojiano maalum.
Mahojiano hayo yalilenga kujua hatua mbalimbali
ambazo serikali inazichukua kukabili ugonjwa huo ambao unaonekana kusababisha
vifo vya wanawake wengi baada ya saratani ya kizazi na ngozi.
Akizungumza, Dk Yuna alisema hadi sasa hakuna
utafiti wowote ambao umewahi kufanyika popote kuthibitisha ukweli juu ya madai
hayo.
“Ni dhana potofu, jamii isiwe na hofu… kitaalamu
haijagundulika nini hasa kisababishi cha saratani hii lakini kuna (risk
factors) tabia hatarishi ambazo zinatajwa kuwa zinaweza kuwa kichocheo cha
kumsababishia mtu kupata saratani ya matiti.
“Kwa mfano wapo ambao wanaweza kupata kwa kurithi
yaani ikiwa kuna mtu kwenye familia au ukoo aliwahi kuwa na ugonjwa huo wapo
ambao wanaweza kuja kurithi hapo baadae,” alisema.
Aliongeza “Unywaji pombe, uvutaji sigara na kitendo
cha mwanamke kuchelewa kuzaa na kutonyonyesha mtoto huweza kumuweka kwenye
hatari ya kupata ugonjwa huu.
Alisema kwa mujibu wa takwimu kutoka Taasisi ya
Saratani Ocean Road (ORCI), kila mwaka tunapokea wagonjwa wapya 50,000 kati ya
hao asilimia 12 huwa wanagundulika kuwa na saratani ya matiti.
“Kati ya asilimia 12 ambao hugundulika asilimia 9.7
hufariki dunia, asilimia 99 ya wanaopata saratani hii ni wanawake, wanaume huwa
asilimia moja tu,” alibainisha.
Alisema hali inaonesha wagonjwa wengi hufika katika
taasisi hiyo wakati ambapo ugonjwa huwa umefika katika hatua mbaya.
“Huwa unapitia hatua nne, ndiyo maana mwezi Oktoba
ulipitishwa kuwa mwezi wa uhamasishaji… kuhamasisha jamii kuwahi mapema
hospitalini kufanyiwa uchunguzi,” alisema.
Alisema mara nyingi dalili huwa ziwa kuongezeka
ukumbwa, kubadilika rangi kuwa kama ya rangi ya chungwa, kupata uvimbe (fundo)
mgumu, chuchu kutoa majibu yasiyo ya kawaida.
“Mara nyingi huwa na rangi nyekundu au usaha mzito,
unaweza kupata maumivu kwenye ziwa au kwenye chuchu ukiona dalili hizo maana
yake tayari una saratani, kwa hiyo unapaswa uwahi tufanye uchunguzi tujue
imefika hatua gani.
“Lakini hatupendi ifike huko ni vema kujitokeza
mapema kufanya uchunguzi kabla hata ya kuona dalili hizo kwani huwa tayari
umepata saratani,” alifafanua.
Chapisha Maoni