Madaktari wakimfanyia upasuaji mgonjwa
*Inahitajika uchunguzi mgonjwa anapofariki ndani ya saa 24 tangu afikishwe hospitalini – Wakili Kikondo
*Ni muhimu kuwa na
daktari binafsi/mshauri – Wakili Kikondo
NA VERONICA ROMWALD- DAR ES SALAAM
HUDUMA za matibabu nchini zinazidi kukua na kuimarika kila kukicha
tunashuhudia namna ambavyo serikali inajidhatiti kuboresha huduma katika
hospitali zake, kadhalika hospitali binafsi nazo zinazidi kufanya uwekezaji.
Lengo ni kuhakikisha watu wanapata huduma bora za matibabu dhidi
ya magonjwa mbalimbali ili wawe na afya njema na waweze kuendelea kujenga
uchumi wao binafsi, familia zao na Taifa kwa ujumla.
Kwa kiwango kikubwa wataalamu wa afya wanajitahidi kuhakikisha
wanatoa huduma za matibabu zinazokidhi viwango vya Kitaifa na Kimataifa.
Lakini wapo wachache ambao wamekuwa wakilalamikiwa kufanya mambo
ambayo hayakubaliki hasa kulingana na maadili ya kazi zao, wakilalamikiwa kutoa
kauli za kuudhi kwa wagonjwa na wakati mwingine matibabu yasiyo sahihi.
MTANZANIA limezungumza na Wakili wa Mahakama Kuu Tanzania, Maulid
Kikondo ambaye anafafanua kwa kina katika makala haya baadhi ya makosa
yanayofanywa na wataalamu wa afya ambayo kwa namna moja au nyingine husababisha
madhara kwa mgonjwa.
“Wataalamu wa afya kwa asilimia kubwa wanajitahidi kutoa huduma
bora za matibabu, lakini kama unavyojua ingawa wapo ambao wanazingatia maadili
na weledi katika kazi wapo ambao hukiuka,” anasema.
Anatoa mfano “Wakati mwingine madhara hutokea kutoka na mazoea
mabaya yaliyojengeka kwenye jamii, kwa mfano mtu anaridhika kuwa na daktari
mmoja ambaye anakuwa anamuhudumia kila wakati anapokuwa anaugua, ni makosa
makubwa katika suala la matibabu.
“Ni vizuri kuwa na daktari binafsi ambaye anakuhudumia lakini
unapaswa pia kuwa na daktari mwingine ambaye atakuwa mshauri wako kama ambavyo
watu wengi mashuhuri hufanya,” anasema.
Kwanini?
“Kwa mfano mgonjwa anakwenda hospitalini anafanyiwa kipimo na
kuambiwa haumwi, lakini kumbe ana saratani ipo hatua za awali na daktari
hajamfanyia uchunguzi wa kina, anarudi nyumbani akiamini ni mzima.
“Kadri anavyokaa nyumbani anazidi kuumwa, anaporudi hospitalini
anakuta ugonjwa umesambaa kiasi kikubwa, daktari anakuwa amemsababishia
madhara… lakini kwa sababu alimuamini anaweza kumtibu pekee anakuwa
amechelewa,” anasema.
Anaongeza “Mgonjwa wa aina hii angekuwa na daktari mshauri, kwa
namna yoyote ile angeweza kuzungumza naye na angemshauri jinsi ya kufanya na
pengine angegundulika mapema na kusaidika, kabla hajapa madhara makubwa.
“Au unakuta daktari anaenda kufanya upasuaji akiwa hajaongozana na
daktari wa usingizi hasa huko kwenye maeneo ya pembezoni matokeo yake mgonjwa
anapata madhara kutokana na uzembe huo,” anasema.
Wakili huyo ambaye amebobea katika upande wa Sheria ya Matibabu
anasema wakati mwingine unakuta mgonjwa alihitaji kufanyiwa upasuaji mdogo
lakini anafanyiwa upasuaji mkubwa kutibu ugonjwa wake hali inayoweza
kumsababishia madhara.
“Kwa mfano msichana anakuja anatakiwa kufanyiwa upasuaji mdogo tu
kutibu tatizo linalomsumbua lakini wakati wa upasuaji daktari akaenda hadi
kugusa kizazi chake na kupelekea kuondolewa, mgonjwa huyo ana haki ya kumshtaki
ili apate haki yake,” anasema.
Anaongeza “Au wakati mwingine unakuta daktari anasahau vitu
mbalimbali tumboni mwa mgonjwa kwa mfano gozi, mkasi na vinginevyo ule ni
uzembe mkubwa mno ambao ungeweza kuepukika, mgonjwa huishi kwa maumivu makali.
“Au unakuta mjamzito anaambiwa na daktari mimba yake imeharibika na
mtoto amefia tumboni lakini anapofanyiwa upasuaji kumbe mtoto mzima, ana haki
ya kushtaki mahakamani.
Anasema hata hivyo si watu wote ambao wanajua kuwa hilo
linawezekana kutokana na elimu duni kuhusu Sheria ya Matibabu ambayo inampa
mgonjwa haki ya kumshtaki mahakamani daktari aliyemsababishia madhara.
Ni kesi ngumu
Wakili huyo anasema kesi hizo kwa kawaida huwa si rahisi
kuziendesha hasa iwapo mwanasheria au wakili anayeisimamia hana uelewa wa
kutosha kuhusu Sheria ya Matibabu.
“Mawakili na wanasheria wengi hawajajikita upande huu wa matibabu,
sasa ili aweze kusimamia vema kesi za namna hii lazima wakili au mwanasheria
awe ana ule uwelewa wa masuala ya kimatibabu.
“Kwa sababu mara nyingi madaktari ndio ambao huja kutoa ushahidi
sasa lazima ujue zile ‘terminologies’ ambazo huwa wanazitumia kwenye kutekeleza
majukumu yao ya kila siku, vinginevyo hata kama mgonjwa ana haki anaweza
kujikuta anashindwa kesi,” anasema.
Mazoea hujenga tabia
Wakili Kikondo (anayehojiwa pichani) anasema mara nyingi mazoea yanayojengeka kwa baadhi
ya wataalamu wa afya kujiamini kwamba wanaweza kufanya kila kitu husababisha
madhara kwa wagonjwa.
“Kwa mfano daktari amebobea katika upasuaji kutibu magonjwa ya
wanawake anakwenda kutoa huduma hiyo pasipo kuongozana na daktari wa usingizi
ambaye kimsingi anapaswa kuwapo katika chumba cha upasuaji,” anafafanua.
Wakili huyo anasisitiza “Kila mtaalamu ana umuhimu wake katika
kusimamia upasuaji wa mgonjwa, kwa uzembe wa aina hiyo matokeo yake unakuta
yanatokea madhara kwa sababu upasuaji haukuzingatia taratibu zinazotakiwa.
Daktari rafiki muhimu
“Makosa makubwa ambayo watanzania wengi tunafanya ni kuwa na
daktari mmoja ambaye tunamuamini kwa matibabu yetu, si kosa lakini ni vizuri
kuwa na daktari rafiki ambaye atakuwa anakushauri katika mambo fulani fulani ya
kimatibabu,” anasema.
Anaongeza “Ni mfumo ambao viongozi wengi wanautumia, ingawa ana
daktari anayemuhudumia lakini yupo daktari mwingine ambaye huwa anamtumia kwa
kumpatia ushauri wa kidaktari, hata inapotokea daktari anayemtibu amekosea huyu
mshauri humsaidia na hivyo kuepusha madhara yanayoweza kujitokeza.
Uchunguzi wa marehemu
Anasema inafahamika wazi kwamba kulingana na imani mbalimbali za
kidini inaaminika kila mwanadamu kama ambavyo alizaliwa ipo siku atakufa na
kurejea kwa muumba wake.
Anasema kwa kawaida binadamu anapofariki mwili wake huhifadhiwa
kwa kufanyiwa maziko maalumu kulingana na imani ya muhusika.
“Kimsingi hakuna anayejua siku yake ya kufa, hiyo ni siri kubwa na
ya kipekee ambayo Mwenyezi Mungu pekee ndiye ajuaye siku ya kufa ya kila
mmoja,” anaeleza.
Anaongeza “Ni kwa mantiki hiyo kila mmoja hufa kwa ‘mtindo’ wake,
wapo ambao huugua maradhi mbalimbali, wengine hufariki ghafla wakiwa usingizi,
wapo wanaopata ajali nakadhalika.
“Pamoja na hayo, mwili wa marehemu nao una haki zake, unastahili
kupatiwa haki hizo kwa sababu ni binadamu ingawa hawezi kuishi tena kama wale
walio hai katika ulimwengu huu,” anasema.
Anasema ili kulinda haki za marehemu, Sheria ya Matibabu huelekeza
mambo muhimu ikiwamo, ni lazima kuuchunguza kujua ukweli wa kile
kilichosababisha kifo cha muhusika.
“Hiyo huwa haijalishi kwamba amepata ajali au ameugua ghafla,
lazima ijulikane kwa undani kile kilichopelekea kifo chake achilia mbali
matukio hayo yanayoweza kuonekana au kusekemekana kwa nje,” anabainisha
Wakili Kikondo anasema kosa kubwa ambalo watu wengi huwa wanafanya
hasa inapotokea mtu amefariki ghafla ni kutaka kuwahi kufanya maziko.
“Kuna umuhimu mkubwa mno wa kuruhusu marehemu achunguzwe, inakuwa
ngumu kushinda kesi unapomshitaki daktari ikiwa hamkufanya uchunguzi kujua
kilichosababisha kifo cha marehemu kama ambavyo sheria ya matibabu inavyoeleza.
“Wengi wanakwepa lakini ili uweze kumshinda daktari uchunguzi ni
muhimu, ni wakati pekee unawez kubaini nini kimesababisha kifo cha marehemu na
procedure inayochukua muda mfupi tu,” anabainisha.
Anasema yapo baadhi ya maeneo watu wanapokuta marehemu amefia
ndani huwa hawaoni umuhimu wa kufanya uchunguzi wa kifo chake.
Kifo saa 24
Wakili huyo anasema kisheria ni jambo linalohitaji uchunguzi wa
kina inapotokea mgonjwa kufariki dunia ndani ya saa 24 tangu alipofikishwa
hospitalini jambo ambalo wengi hawajui.
“Inapotokea hali hiyo ni lazima uchunguzi ufanyike, nini kimetokea
hadi mgonjwa afariki. Pia inapotokea mgonjwa amefia kwenye meza ya upasuaji
wakati wa upasuaji wenyewe (madaktari) wanaita kitaalamu ‘death on table (DOT)’
yaani mgonjwa anakuwa amekufa kitandani akifanyiwa upasuaji,” anabainisha.
Anaongeza “Hata hivyo kwa kuwa watu wengi hawajui kwamba kisheria
hilo linahitaji uchunguzi wa kina basi huwa hawajishughulishi kutaka kujua nini
ambacho kimepelekea kifo cha marehemu.
“Ingawa hatuwezi kuzuia kifo, lakini kinapotokea lazima tujiulize
nini kimesababisha si kuchukulia kila kifo kwamba kimepangwa na Mwenyezi Mungu,
ikiwa marehemu amefariki kwa mfano kwa kulishwa sumu tutayajua hayo baada ya
uchunguzi, kifo chochote kile ni muhimu kufanya uchunguzi,” anasisitiza.
Changamoto
Anasema wakati mwingine huwa kuna shinikizo kutoka kwa ndugu wa
marehemu kutaka ndugu yao azikwe mapema ingawa askari wa Jeshi la Polisi
hufanya kazi nzuri kuhakikisha marehemu anafanyiwa vipimo, jamii inapaswa sasa
kutambua umuhimu wa suala hilo.
Wakili Kikondo anasema kosa jingine ambalo ndugu wa marehemu
hufanya ni kuondoka na mwili wa marehemu kwenda kuuzika pasipo kusubiri taarifa
ya daktari.
“Hakikisheni mmechukua pia taarifa ya uchunguzi wa mwili wa ndugu
yenu, ingawa ipo pia changamoto kwa baadhi ya ndugu kuogopa kuingia ndani
wakati daktari akimfanyia uchunguzi ndugu yao kujua nini ambacho kimepelekea kifo
chake,” anasema.
Anasema kutokana na hali hiyo, ikiwa kifo hicho kimetokana na
uzembe wa daktari, basi daktari husika anaweza kutumia mwanya huo kwa
kushirikiana na wenzake wasio waaminifu kutengeneza taarifa ya uwongo kuhusu
kifo cha marehemu.
“Ni muhimu ndugu wa marehemu kuhudhuria kipindi cha ‘postmortem’
ili kupata uthibitisho wa kile kilichosababisha kifo cha ndugu yao,”
anasisitiza.
Anaongeza “Matibabu yanapaswa kuwa professional, kwa mfano
unapomfikisha mgonjwa wako hospitalini akapoteza maisha ndani ya saa 24
akipatiwa matibabu, lazima ujue nini kimepelekea kifo chake.
“Nimeshuhudia wengi wanapokuja kuchukua mwili wa marehemu huwa
wanahangaika kutafuta tu barua ya kibali cha maziko lakini wanasahau kwamba
taarifa ya uchunguzi ni muhimu pia,” anasema
Kwa ushauri wa bure
na maelekezo zaidi tumia email ifuatayo mkikondo@yahoo.com
Chapisha Maoni