Picha na mtandao
Na Veronica Romwald, Dar es Salaam
SCHIZOPHRENIA
ni miongoni mwa magonjwa makubwa ya akili. Jina hilo limetoholewa kutoka katika
lugha ya kilatini ambapo asili yake ni maneno mawili ambayo ni Schizo na
Phrenia.
Kwa tafsiri
ya lugha ya Kiswahili rahisi humaanisha akili iliyogawanyika au iliyotawanyika,
yaani huwa haziendi sawa sawa… huwa hakuna muunganiko kati ya mtu na akili
yake.
Yapo
magonjwa mengi ya akili ambayo kati yake yapo yanayohusisha kuchanganyikiwa
akili kama huu wa Schizophrenia.
Daktari
Bingwa wa Afya na Magonjwa ya Akili wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Said
Kuganda anafafanua vema kuhusu ugonjwa huo katika makala haya aliyozungumza
hivi karibuni na MTANZANIA (matukionamaisha).
“Huwa
haziendi sawa sawa, yaani hakuna muunganiko kati ya mtu na akili yake, kuna
magonjwa mengi ya akili ambayo kati yake yapo yanayohusisha kuchanganyikiwa
akili kama huu wa Schizophrenia.
“Lakini pia
yapo ambayo hayahusishi kuchanganyikiwa akili, watu wengi wanaugua magonjwa ya
akili lakini huwa hawachanganyikiwi isipokuwa wapo wachache ambao wakiugua
huchanganyikiwa,” anabainisha.
Dk. Kuganda
anasema wale ambao huchanganyikiwa nao kuna vipindi fulani katika maisha yao
huwa wanakaa sawa na kuna kipindi huonesha ile hali ya kuchanganyikiwa.
Kuchanganyikiwa akili maana yake
nini?
Anafafanua “Kuna
maeneo matano ambayo ni muhimu katika mwili wa binadamu ambayo huashiria akili
kuchanganyikiwa.
“Eneo la
kwanza ni kuwa na imani ambayo si halisi (potofu) iliyopitiliza katika ule
uhalisia wake wa kawaida,” anasema.
Utajuaje?
Daktari
huyo anasema ili kubaini jambo hilo ni lazima mgonjwa apimwe kwatika nyenzo
zote muhimu zinazohitajika.
“Kwa mfano
mila na desturi zake, tunaangalia kwao wanaamini nini kuhusu hicho
anachokiamini yeye, elimu yake inamueleza nini kuhusu kitu anachokiamini na je
dini yake inaeleza nini kuhusu jambo
analoliamini,” anasema.
Anaongeza
“Wakati mwingine unakuta ana imani sahihi lakini huenda imepitiliza, sasa kujua
iwapo imepitiliza kile kiwango au la lazima tulete vigezo muhimu na tujadiliane
pamoja naye ili kujiridhisha.
“Tukibaini
kuna ambavyo ameviruka tunamuuliza sababu ya kuviruka na kwenda kwenye vigezo
vingine, kwa mfano mtu anaweza kusema yeye ni Mungu kwamba hiyo ndiyo imani yake
na anashughulikia viumbe vyote.
“Inabidi
muhojiane naye katika upande huo huo wa kuzungumzia Mungu na uwezo wake tofauti
na Mungu ambaye wengine wote tunamfahamu,” anasema.
Anaongeza “Hivyo
tuna-challenge ile imani yake, ikishafika kipindi kwamba hana uwezo wa kurudi
nyuma katika kile anachokiamini na jamii husika na elimu na vyote vilivyobaki
(background information) kwamba alipo yeye siko basi tunajua mtu huyo
amechanganyikiwa.
“Na hapo
anakuwa anashughulishwa na yale anayoamini, kama amesema yeye ni Mungu basi
unakuta hata ametengeneza mamlaka au anashurutisha watu wafanye mambo fulani
fulani.
“Matokeo
yake mambo yake huwa hayafanikiwi kwa sababu anakuwa anaendeshwa na ile imani
potofu aliyokuwa nayo,” anabainisha.
Daktari
huyo anasema lakini yapo mambo mengine ambayo huweza kubainisha mtu kuwa na
tatizo hilo la Schizophrenia.
“Kwa mfano
katika hali ya uhalisia mtu anaweza kulalamika kuna watu nje ya nyumba yake
wanamsubiri huku wamebeba silaha wakitaka kumdhuru.
“Sasa
unakuta mtu analalamika kuna watu wanamfuatilia wamdhuru nje ya nyumba yake lakini
mkifuatilia kwa kina hata kwa kukaa nje ya nyumba yake hamuwaoni watu hao
lakini yeye anang’ang’ania kwamba wapo, hiyo inakuwa ni imani ambayo si ya
kweli,” anasema.
Dk. Kuganda
anasema hali hiyo huweza kumsababishia muhusika kuogopa kabisa kutoka nje ya
nyumba yake akiamini kuna maadui wanamsubiri.
“Kama ni
mfanyakazi moja kwa moja hali hiyo huathiri ule utendaji kazi wake wa kila
siku, anaweza kuamua asiende kazini kabisa na akajikuta akifukuzwa kazi lakini
wakati huo ofisi yake huenda haijui kabisa kama anakabiliwa na tatizo la
akili,” anasema.
Anaongeza “Eneo
jingine ambalo linaashiria akili kuchanganyikiwa ni kuwa na hisia ambazo ni
potofu, kwa kawaida binadamu ana hisia tano muhimu za kawaida.
Anazitaja
hisia hizo kuwa ni za kuona, kugusa, kuonja, kusikia na kunusa.
“Lakini mtu
aliyechanganyikiwa anaweza kutumia nyenzo hizo hizo kuona, kuhisi, kunusa,
kugusa au kusikia vitu ambavyo wengine hatuoni, hatuhisi, wala kusikia,”
anabainisha.
Dk. Kuganda pichani anatoa
mfano kwamba “Muhusika anaweza kusema anaona nyoka anapita eneo ambalo mmekaa
naye pamoja lakini nyie msimuone au anasikia sauti na watu wanazungumza habari
zake, wanamshurutisha au wanamtisha lakini nyie hamuoni wala hamsikii chochote.
Anaongeza
“Wakati mwingine anaweza kudai kwamba anasikia sauti yake mwenyewe,… kwamba
yale anayowaza na kutafakari anasikia kikizungumzwa huko redioni.
“Wakati
mwingine anaweza kuhisi kuna vitu ambavyo vinatambaa mwilini mwake (hii ni
hisia ya kugusa) lakini kila
anacholalamika kwamba kinamsumbua unakuta nyie wengine hamkioni ila yeye
kinakuwa kweli kinamsumbua na mambo yake unakuta hayaendi sawa sawa,” anasema.
Anasema
wakati mwingine mnaweza kula naye chakula aina moja lakini yeye akalalamika
kupata ladha tofauti na ile mnayoipata nyie.
“Anaweza
hata akadai chakula chake kimetiwa sumu lakini si kweli, au wakati mwingine
akanusa harufu ambazo hazipo,” anasema.
Anasema
ingawa hayo wakati mwingine huwa ni mambo ya kawaida hata hivyo yakipitiliza
huashiria kuwapo kwa tatizo hasa la kuchanganyikiwa kwa akili ya muhusika.
Anasema
hali hiyo husababisha tabia za muhusika kubadilika na hata mienendo yake kwa ujumla.
“Mnaweza
kumbaini pia kwa maneno yake, anaweza kuongea vitu vingi ambavyo havina
muunganiko kutoka stori ya kwanza kwenda ya pili.
“Kwa mfano
akaanza kuwasimulia amezaliwa lini, kisha hapo hapo akahamia stori nyingine
labda kuhusu mambo ya barabarani mara akaanza tena kuwasilimulia kuhusu mambo
ya Marekani.
“Tunasema
anaongea ovyo ovyo kwa hiyo kule kuongea ovyo ovyo kunaonesha wazi dalili ya
kuchanganyikiwa hata kama hajawaambia anaumwa,” anasema.
Rahisi kumtambua
Dk. Said
anasema ni rahisi kumuangalia hata kwa matendo yake.
“Kuna kuchanganyikiwa
kwa matendo yake kwa mfano wale wanaotembea barabarani utaona wanaanza kubeba
mizigo mikubwa, wanavaa nguo zaidi ya moja wakati mwingine hadi nane, hiyo
huashiria kwamba kile kiwango cha kuchanganyikiwa kimekuwa kikubwa mno,”
anabainisha.
Anaongeza
“Yaani hata kama hujaambiwa kitu ukimtazama tu unajua kwamba mtu huyo
amechanganyikiwa.
“Unaweza
pia kubaini, wakati mwingine wagonjwa wa aina hii hujitenga na jamii,
hujitengenezea ulimwengu wa peke yao, unakuta mtu anatabasamu mwenyewe,
anaongea mwenyewe na mambo mengine kama hayo.
“Huwa
hawahitaji kuingiliwa au kuwaingilia wengine ndiyo maana hujitenga, hapo
huonesha wazi viashiria vya kuchanganyikiwa,” anasema.
Anasema
mgonjwa huweza kuonesha mambo mawili au matatu na wakati mwingine yote matano
kati ya hayo aliyoeleza hapo juu.
“Ni ugonjwa
ambao hukaa muda mrefu kuanza kuonesha dalili hadi kipindi cha miezi sita
lakini wakati mwingine hali hiyo huweza kutokea ghafla,” anasema.
Idadi ya wanaougua
“Katika
magonjwa yote ya akili tunayoyafahamu huu ni ugonjwa ambao katika ‘population’ watu
chini ya asilimia moja huugua ugonjwa huu,” anasema.
Anaongeza “Kiwango
cha kuathirika kipo sawa kwa jinsi zote ( wanaume na wanawake) lakini kuna vitu
ambavyo huchangia mtu kupata ugonjwa huu.
Idara hii hupokea wagonjwa wote wa dharura ikiwamo wanaofikishwa wakisumbuliwa na magonjwa ya akili
Visababishi
Anasema
ugonjwa huo hurithiwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine.
“Ikiwa
katika kizazi chenu kuna mtu amewahi kuugua ugonjwa huo basi kuna uwezekano wa
mmoja wenu kurithi kwa sababu shida ipo katika akili,” anasema.
Anasema
mambo mengine ambacho huchangia mtu kupata ugonjwa huo ni changamoto za
kimaisha.
“Hali ya
umaskini, kutokuwa na kazi na ikiwa mtu aliwahi kupata majanga mbalimbali
wakati wa makuzi yake anauwezekano wa kupata ugonjwa huu katika maisha yake,”
anasema.
Anaongeza
“Ingawa si visababishi vya moja kwa moja lakini mara nyingi humuwekwa mtu
kwenye hatari ya kuja kupata ugonjwa huu.
Wenye akili nyingi
Yapo madai
kwamba baadhi ya watu huzaliwa wakiwa na akili nyingi kuliko wengine na hali
hiyo hupelekea kuchanganyikiwa akili katika maisha yao, Dk. Kuganda anafafanua
madai hayo.
“Si kweli, hakuna
uhusiano wowote kati ya mtu kuzaliwa akiwa na akili nyingi na kuchanganyikiwa,”
anasema Dk Kuganda.
Anaongeza
“Isipokuwa kuna ugonjwa mwingine ambao si Schizophrenia. Huo mtu akiugua akili
zake huwa zina-charge vizuri lakini akipona akili yake hurejea katika hali yake
ya kawaida.
“Lakini huu
wa Schizophrenia hauhusiani kabisa na akili ya mtu kwamba aliyesoma sana
anaweza kuugua ugonjwa huu lakini wale ambao hawajasoma huwa kwenye hatari
zaidi ya kupata ugonjwa huu,” anasema.
Anafafanua
“Usiposoma kabisa maana yake hujaelimika na labda huna kazi, hapo vitu vingi hujipanga
na vingi huwa ni changamoto hali hiyo hupelekea akili kuwa kwenye uwezekano
mkubwa wa kulipuka.
“Tunasema
kuchanganyikiwa ni mlipuko wa akili hata wale ambao wapo barabarani jamii
huwatenga bila kujua kwamba ile hali hujitokeza tu na wakipata matibabu sahihi
akili hurejea katika hali yake ya kawaida,” anasema.
Anasema
hata hivyo pindi wanapochelewa kupatiwa matibabu sahihi ingawa hupona
wakitibiwa hata hivyo matibabu huchukua muda mrefu.
“Magonjwa
mengi ya akili huja na kuondoa ndiyo maana tunasema mlipuko tu ule yakitibiwa
huondoka na mtu hupona,” anasisitiza.
Jinsi wanavyotibu
Anasema
hwua wanatumia njia tatu kuwatibu wagonjwa wa akili ambazo ni za kibaiolojia, kisaikolojia
na
“Kibaiolojia
huwa tunawapatia dawa mbalimbali za kuondoa zile dalili lakini yapo ambayo huwa
hayahitaji kutibiwa kwamba dawa bali kwa mazungumzo maalum (kisaikolojia) na
matibabu ya kijamii.
“Huwa
tunazungumza kitaalamu na mgonjwa namna ya kupunguza msongamano wa mawazo
kwenye ubongo wake, ule msongamano ukipunguabasi mtu huweza kutafakari vizuri
na kufanya maamuzi sahihi,” anasema.
Anasema kwa
upande wa matibabu ya kijamii huwa wanakaa na kuzungumza na watu wanaomzunguka
mgonjwa husika.
“Kwa sababu
unaweza kukuta shida haipo kwa mgonjwa bali kwa jamii inayomzunguika, wakati
mwingine matibabu huhitaji kufanya kazi basi hapo huwa tunamtibu mgonjwa
kitaalamu kwani si kila kazi anapaswa kufanya kutibu akili yake,” anabainisha.
Anaongeza
“Lakini kuna wakati mwingine huwa tunalazimika kuchanganya matibabu yote haya
kwa wakati mmoja ili kupata matokeo mazuri zaidi kwa mgonjwa.
Vijana hatarini
Anasema mara
nyingi tatizo la Schizophrenia hutokea mtu anapokuwa katika hatua ya ujana hasa
kuanzia kipindi cha miaka 18 hadi 25.
“Hiyo ni
kwa sababu huo ndiyo umri wenye changamoto nyingi kuliko makundi mengine, mtu
anaweza kurithi lakini mlipuko wa kwanza wa akili ukatokea akiwa na umri wa
miaka 25.
“Kwa sababu
katika kipindi hicho mtu hukutana na changamoto nyingi za kimaisha kuliko
kipindi kingine katika maisha yake,” anabainisha.
Uelewa duni
Daktari
huyo anasema bado jamii haina uelewa wa kutosha kuhusu magonjwa hayo kwamba
pindi mtu anapougua anapaswa kuwahishwa hospitalini kupatiwa matibabu na si
vinginevyo.
“Unakuta
wengi wanawafungia majumbani au wanasukumia huko mitaani au wanawapeleka kwenye
nyumba za ibada au kwa waganga wa kienyeji wakiamini wamerogwa jambo ambalo si
sahihi,” anasema.
Anasema
kutokana na hali hiyo wengi hufikishwa hospitalini miaka miwili hadi mitatu
tangu walipoanza kuugua.
“Wale ambao
huwahishwa hospitalini mara nyingi unakuta hali ya kuchanganyikiwa huhusisha
kufanya vurugu na wapo ambao tunapoanza kuwatibu wakitulia tu ndugu zao
huwachukua na kuondoka nao huku wakiwa hawajapona vema,” anasema.
Rai kwa jamii
“Ni vema ukipata
ndugfu yako ameugua ugonjwa wa akili mumuwahishe hospitalini apate matibabu
sahihi kwani karibu magonjwa yote ya akili yanatibika na watu huendelea kuishi
kwa amani na furaha kama awali.
“Kuliko kumfungia
mgonjwa ndani si jambo zuri, kunyanyapaa pia si vizuri jaribu kufikiri jinsi
unavyomsukumia mtaani ingekuwa wewe ungejisiaje, kusema ule ukweli kwamba
wagonjwa wengi wa akili huwa hawapendi na hawajisikii vizuri kuendelea kukaa
huko mitaani,” anasema.
Makala haya kwa mara ya kwanza yametoka Desemba 28, 2017 katika gazeti la MTANZANIA ambalo nalitumikia.
Makala haya kwa mara ya kwanza yametoka Desemba 28, 2017 katika gazeti la MTANZANIA ambalo nalitumikia.
Chapisha Maoni