Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement



Wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Serikali na Afya tawi la Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TUGHE-TIC) wakiapa mbele ya Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage. Hafla hiyo ilifanyika katika ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNICC). 

Na Veronica Romwald, Dar es Salaam
SEKTA ya viwanda imepewa kipaumbele na serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Rais John Magufuli.

Mpango wa serikali ni kufikia Tanzania ya viwanda, hivi sasa mikakati mbalimbali imepangwa na inatekelezwa kufanikisha lengo hilo.

Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage anasema Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) ni miongoni mwa taasisi muhimu mno katika kufanikisha suala hilo.

Desemba 15, mwaka huu Waziri Mwijage alizindua rasmi Baraza la Wafanyakazi wa Serikali na Afya Tawi la TIC (TUGHE-TIC).

Akizindua Baraza hilo, anasema litasaidia kuongeza chachu ya ushiriki wa wafanyakazi moja kwa moja katika uandaaji wa mipango mbalimbali na utekelezaji wake.

“Ili tuweze kupata matokeo mazuri, nimepewa kazi ya kujenga viwanda, TIC ni jicho na masikio yangu katika kulitimiza jambo hilo,” anasema.


Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage akimkabidhi mkataba wa uundwaji wa Baraza la Wafanyakazi wa Serikali na Afya tawi la Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TUGHE-TIC), Mkurugenzi wa TIC, Geofrey Mwambe mara baada ya kuzindua Baraza hilo 

Anaongeza “Bado TIC hamjafanya kazi kiasi cha kunifurahisha, nataka mfanye kazi kama vile waganga wa kienyeji wanavyofanya kazi zao.

“Mganga wa kienyeji huwa hakosi majibu ya maswali aliyonayo mteja wake yeyote anayempokea katika kibanda chake.

“Nataka mtu akija kwenu kutaka kuwekeza au nikimuelekeza mtu kwenu basi apate majibu ya mahitaji yake na ikiwa hamna nendeni pembeni mnipigie simu moja kwa moja ili niwape maelekezo,” anasisitiza.

Mgongano wa kisheria

Waziri huyo anawataka TIC kufanya kazi kwa weledi na kwamba pale ambapo kunatokea mgongano wa kisheria wamjulishe mapema.

“Ili kufikia Tanzania ya viwanda inahitajika mabadiliko ya kifkira, penye mgongano wa kisheria nijulisheni ili tuipitie na kuifanyia maboresho au marekebisho pale inapobidi, tunaongozwa na sheria ambazo si msahafu wala biblia,” anasema.


Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage akimkabidhi mkataba wa uundwaji wa Baraza la Wafanyakazi wa Serikali na Afya tawi la Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TUGHE-TIC), Mwenyekiti wa Baraza hilo, Brandon Maro mara baada ya uzinduzi huo

Hali ya uwekezaji

Akizungumzia hali ya uwekezaji kwa sasa nchini, Waziri Mwijage anasema ni nzuri ikilinganishwa na hapo awali.

“Nimesema awali, TIC ndiyo jicho na sikio letu katika kufikia Tanzania ya viwanda, ninyi ndiyo receptionalist (mapokezi) yetu.

“Kimsingi watu wote wanaohitaji kuwekeza nchini lazima waanzie TIC na anayepaswa kuelekeza na kufundisha kuhusu uwekezaji ni TIC wapokeeni watu na muwaelekeze inavyopaswa,” anasema.

Anasema katika kipindi cha miaka miwili tayari kuna jumla ya viwanda 3,306 vyenye uwezo wa kuajiri kuanzia wafanyakazi 10 na kuendelea.

“Viwanda vikubwa vipo 580 na nina matumaini ya viwanda vikubwa zaidi, tunaelekeza kwenye sekta tatu viwanda vinavyotoa ajira kwa watu wengi, vinavyochakata malighafi kutoka nchini na viwanda vinavyozalisha bidhaa zinazotumika kwa wingi,” anabainisha

Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage akifafanua jambo mara baada ya kuwakabidhi wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi wa Serikali na Afya, Tawi la Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TUGHE-TIC) 

Waziri Mwijage anasema leo hii Tanzania ina uwezo wa kuzalisha saruji kuliko uhitaji wan chi, kuna uwezo wa tani milioni 10.8 na mahitaji ni tani milioni 4.87.

“Kuna viwanda viwili vinakuja cha Mamba na Nyati vyote vitakuwa Chalinze na kingine kitaenda Tanga, kuna vya kuchakata matunda.

“Dabaga naye anatengeneza tomato saurce nchini na Sayona anazindua kiwanda Januari mwakani cha kuchakata matunda, hivyo tunakwenda vizuri,” anasema.

Anaongeza “Ndiyo maana nikasema Baraza hili ni muhimu, kwa sababu wafanyakazi wakishaelewa tunategemea watawakaribisha vizuri watanzania na wageni wanaohitaji kuwekeza nchini.

Vipimo vya WB

Anasema vipimo vya Benki ya Dunia (WB) vilivyotolewa hivi karibuni kuhusu wepesi wa kuwekeza duniani Tanzania ina namba mbaya ya uwekezaji.

“Lakini mimi hiyo hainibabaishi kwa sababu vitu vingine vinahitaji ukombozi wa kifkra kuna mambo ambayo lazima tuondokane nayo ili twende kwenye nafasi tunayostahili.

“Tunataka mtu akiwekeza hapa afurahie kuwekeza Tanzania, kiujumla hali ya uwekezaji ni nzuri na hiyo misukosuko mnayoisikia ni kwa sababu ya kutaka malengo makubwa.

“Ni kama vile mgumba akiolewa miaka 30 anataka apate mtoto na amtume dukani hapo hapo, tumeahidi viwanda lazima tufikie lengo,” anasema.

Mkurugenzi wa TIC, Geofrey Mwambe anasema Baraza hilo lina jumla ya wajumbe 35 na kwamba kati yake wapo wawakilishi wa kuteuliwa kutoka nje ya kituo ambao wanaingia kwa mujibu wa sheria na kanuni.

“Baraza hili ni la muhimu mno katika kuboresha ufanisi na utendaji kazi wa kituo ikiwamo utekelezaji wa maagizo na maelekezo ya Rais John Magufuli,” anasema.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement