Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement
Na Veronica Romwald, Dar es Salaam

MARA kadhaa tumepata kushuhudia mizozo na migogoro huwa inaibuka katika familia na jamii mtu anapofariki dunia.
Ugomvi huwa nani hasa mwenye haki na anayepaswa kuuchukua mwili wa marehemu ili kwenda kuupumzisha katika ‘nyumba’ yake ya milele.

Shida zaidi hujitokeza pindi tu mgonjwa anapofariki dunia na ndugu zake kuanza kujitokeza kudai mwili wake licha ya kutojitokeza wakati akiwa mgonjwa.

Ndugu hung’ang’ania kupatiwa mwili wa marehemu huku ikiwa hakuwahi kuwataja kuwa watu wake wa karibu ambao wanastahili kupatiwa taarifa zozote kuhusu yeye au hata kuchukua mwili wake kwa maziko ikitokea amefariki dunia.

Wakili wa Mahakama Kuu aliyebobea katika Sheria ya Matibabu, Maulid Kikondo ambaye anaeleza jinsi gani jamii inaweza kuepuka migogoro ya namna hiyo.

“Wakati mgonjwa anaumwa sana, utaratibu wa kawaida wa hospitali anatakiwa kujaza maelezo maalum ikiwamo kumtambulisha mtu wake wa karibu anayeweza kuwajibika wakati yeye akiwa hospitalini hapo akipatiwa matibabu,” anasema.

Anasema mtu huyo anayetajwa ndiye ambaye ikitokea mgonjwa amefariki hospitali huwajibika kumtumia na hata kumkabidhi mwili wa marehemu ili aende kuuzika.

“Shida hutokea pale ambapo mgonjwa anapokuja hospitalini humtaja mtu ambaye hayupo karibu na familia yake labda ni rafiki tu au jirani ambaye anamuuguza.

“Inapotokea amefariki dunia unakuta ndugu zake wanaanza kujitokeza kuja hospitalini kutaka kupatiwa mwili wao wakati huo huo unakuta hawajatajwa kwenye maelezo maalum ya mgonjwa,” anasema.

“Wakati aliyeandikwa anastahili kupatiwa mwili wa marehemu unakuta ndugu labda wametoka mkoani wameshakuja pale hospitalini na kuanza kulalamika wakitaka kupatiwa mwili wao, ni changamoto,” anasema.

Mzozo

Anasema inapofikia hatua hiyo mzozo mkubwa hujitokeza juu hasa nani anapaswa kuchukua mwili ingawa maelezo ya marehemu yanamtambulisha yule aliyemtaja ambaye ndugu wakati huo wanadai hawamtambui.

“Kisheria huwa ni mgogoro mgumu mno kwa sababu yule wanayemgombea tayari ni marehemu hawezi tena kuzungumza chochote tujue ukweli ni upi kati ya hao wanaomgombania,” anasema.

Hatua  

Wakili Kikondo anasema inapotokea hali hiyo, ndugu wanaodai kuwa na uhusiano na marehemu hutakiwa kwenda kuripoti katika ofisi ya serikali ya mtaa na kuja na vielelezo vinavyoweza kuthibitisha uhalali wa wao kupatiwa mwili wa marehemu.

“Lazima walete vithibitisho kutoka serikali ya mtaa vitatusaidia sisi kutambua ikiwa kweli si mtu anayetaka kuchukua mwili wa marehemu kwa ajili ya matumizi yake binafsi na ana nia nzuri kweli,” anasema Wakili Kikondo (pichani).

Anaongeza “Kwa sababu kule mtaani wanamtambua kwamba ni ndugu halali wa marehemu na kweli ana uwezo wa kuhimili zile taratibu zote zinazohitajika kufanikisha jambo hilo.

“Hata hivyo bado na sisi (wanasheria) huwa ni jukumu letu pia kutambua kwamba yale maelezo yao ni ya kweli au si kweli inabidi na wewe utafute uthibitisho juu ya hayo waliyoeleza.

“Kwa hiyo huo si mzozo rahisi, mwenyewe (marehemu) angekuwapo angesema ukweli wa mambo lakini haiwezekani,” anasema.

Mgogoro na hospitali

Anasema mizozo ya kugombea mwili wa marehemu huweza pia kusababisha mgogoro kati ya familia ya ndugu wanaodai kuwa na uhusiano na marehemu na hospitali husika.

“Unakuta mtu anayejitokeza kuchukua mwili wakati mwingine hajawahi kujitokeza hata siku moja, kwa mfano unakuta mtu amefariki Dar es Salaam na ndugu zake wanaishi Mwanza.

“Ndugu hao hawajawahi kutokea hata siku moja kuja hospitalini na unakuta ameuguzwa na rafiki yake sasa aliyeandikwa ni huyu anayemuuguza akifariki ndugu wanakuja.

“Unakuta ni wageni hata wauguzi hawawatambui wala mtu yeyote pale hospitali na wala hata mmoja wao hatajatajwa kwenye maelezo ya marehemu na wanang’ang’ania wapewe mwili na waongoze kila kitu wao,” anasema.

Anafafanua mara nyingi katika karatasi ya maelezo huwa anaandikwa mtu mmoja lakini ikiwa mgonjwa ataeleza maelezo ya tofauti wanaweza kumpa nafasi au kwenye ile faili anaweza daktari akaeeleza japo ametajwa fulani lakini mtu huyo bado ana ndugu wa kumsaidia.

“Unakuta hakuna maelezo ya ziada, inapofikia hapo… ndugu wengi hudhani viongozi wa hospitali huwa wanafanya vile kwa kuwasumbua jambo ambalo si kweli, kiuhalisia hospitali kama taasisi haiwezi kurahisisha maamuzi kama ambavyo mtu hutaka iwe.

“Lakini ikiwa mtu (marehemu) mwenyewe amemtambulisha fulani kwamba ndiye anayemtambua kama mtu wake wa karibu na hajakutaja wewe kama mzazi au ndugu wa kuzaliwa naye, wao wana haki ya kufuata maelezo yaliyotolewa,” anasema.

Nini kifanyike

Wakili huyo anasema ili kupunguza matatizo ya namna hiyo kujitokeza kwenye jamii ni muhimu mno watu kuandikisha watu wao wa karibu na si vinginevyo.

“Ni vema kumtaja mtu ambaye anastahili kushughulikia matatizo yanayokukabili wakati wa ugonjwa na ambaye atapaswa na ataweza kusaidia kuhifadhi vema mwili wako ikiwa utafariki dunia,” anasisitiza.

Anaongeza “Kwa sababu inapotokea wakati mwingine mtu anayetajwa mule wanatofauti kubwa mno kimtazamo hadi imani ya dini, wakati mwingine huleta shida kwani huwa hawezi kufuata taratibu za mazishi kulingana na dini ya marehemu.

“Hivyo ni muhimu kuandika mtu unayemuamini ili hata ikitokea umepata shida na unahitaji upasuaji kwa mfano huku ukiwa huwezi kuzungumza basi mtu huyo kwa mujibu wa taratibu huruhusiwa kusaini badala yako ili ufanyiwe upasuaji husika.

“Hivyo, hakikisha unamuandika mtu ambaye ni wa karibu na familia yako, anajulikana lakini pia ana uwezo wa kutimiza wajibu wake kwako,” anasema.
Wosia wa maziko

Anasema inashauriwa mtu anapokuwa katika hali ya ugonjwa ana haki ya kuandika wosia wa maziko yake.

“Mgonjwa anaruhusiwa kuandika ikiwa imetokea amefariki anawataja wale ambao wanaweza kushiriki katika maziko yake ipasavyo, hata wauguzi wamefundishwa jinsi ya kusimamia hayo mambo,” anasema.

Anaongeza “Watu wamezoea kwamba wosia lazima uhusishe mali zake zote lakini si kweli, unaweza kuandika wosia ukifariki dunia nani asimamie maziko yako.

“Na mali zingine ambazo hazijatajwa kwenye wosia huo zinaweza kuamriwa kwa kuzingatia sheria zingine zilizopo, na inashauriwa ni vizuri unapotaka kuandika wosia ukamshirikisha muuguzi au daktari wako.

“Unaweza kumueleza kwamba hali yako si nzuri na unahitaji kuandika watu ambao wanaweza kuhusika moja kwa moja ikitokea umefariki dunia,” anasema.
Si uchuro

Wakili huyo anasema jamii inapaswa kuondokana na imani potofu kwamba kuandika wosia ni ‘kujiombea’ kufariki dunia mapema.

“Kufa hakuna dalili, unaweza kuwa mzima ukafa na ukawa mgonjwa pia ukafa, kwa hiyo suala la kuandika wosia ni suala la msingi mno katika maisha yetu.

“Na linasisitizwa mno kwa sababu migogoro mingi inayotokea kwenye jamii, mtu baada ya kufariki watoto na wananyanyasika inajitokeza kwa sababu wengi wanafariki na hawaachi maelezo ya msingi,” anasema.

Anaongeza “Matokeo yake watu wanajitokeza wanadai kumbe hawadai au mtu anajitokeza anaamua mali za marehemu ziuzwe na ukiacha hayo kuna baadhi ya familia ama mama au baba anakuwa anamiliki mali ambazo hazijulikani.

“Inapotokea umefariki ghafla ile mali inapotea unakuta yule mnayejuana labda ni fundi alikuwa anasimamia basi anajimilikisha labda awe mwaminifu sana aweze kuirudisha kwenye jamii (familia).

Wengi hukosea

Anasema ingawa watu wengi huandika wosia lakini tatizo ni kwamba hawazingatii taratibu za kisheria.

“Kwa sababu ile sheria inayoelekeza jinsi ya kuandika wosia inatoa taratibu kwamba yule anayeandika wosia lazima ajue kusoma na kuandika na lazima awe na mashahidi wawili ambao watashuhudia wakati akiusaini.

“Lakini unakuta mtu anaandika wosia akiwa peke yake anausaini halafu akishausaini anatafuta mashahidi wawili ili wamsainie hiyo haitakiwi kisheria,” anasema.

Anaongeza “Inatakiwa wakati wewe unasaini wale mashahidi nao wawe wanashuhudia ukiweka hiyo saini na hata watakapoitwa kwenye mizozo mahakamani swali kubwa watakaloulizwa ni kwamba je walikushuhudia ukisaini huo wosia, yule wa kwanza atajibu ndiyo kadhalika na wa pili.

“Lakini kama yule anayeandika wosia hajui kusoma wala kuandika hapo huwa kuna shida, inabidi sasa mashahidi wake wawe watano na mara nyingi hushauriwa kwamba shahidi mmoja awe miongoni mwa ndugu na ikiwa ni ya kimila inashauriwa mume au mke awe sehemu ya ushahidi.

“Lakini pia ni muhimu kuepuka mno mashahidi kuwa warithi kwa sababu wakati mwingine wosia unaweza kuwa chanzo cha migogoro katika familia.
Mfano hai

Anasema katika kitabu cha ‘The Law’s Empire’ kinaelezea kuhusu kesi ya babu mmoja aliyetaka kumrithisha mali mjukuu wake.

“Babu huyo aliamua kuoa lakini kwa kuwa mjukuu wake alijua kwamba yeye ndiye mrithi basi akapata hofu kwamba mwanamke aliyeolewa na babu yake atachukua ule urithi wake.

“Basi aliona njia rahisi ni kumuua babu yake ili arithi mapema zile mali hata hivyo hilo lilijulikana na mjukuu huyo hakurithishwa zile mali za babu,” anasema.

Anaongeza “Tangu hapo, ikatungwa kanuni ya kisheria kwamba mtu hawezi kunufaika kwa makosa yake mwenyewe, hasa inapojulikana kwamba mtu ameua ili arithishwe.

Ni siri

Anasema ili wosia uheshimike unapaswa kutunzwa, mahakama kuu, kwa wakili wako au katika taasisi maalum.

“Inapofika hapo ndiyo maana mmoja wa mashahidi awe mtu wa familia ili aweze kusimamia wosia wako pindi utakapofariki dunia,” anasema.

Anasema hata hivyo huwa zinahitajika gharama kidogo katika kuutunza wosia husika na huwa zinategemea nani anakuandikia na wewe unayeandikiwa vitu vyako ni kiasi gani na vipo wapi na wapi.

“Kuna wakati pia hutegemea wengine huwa wanaandikiwa bila kulipia gharama yoyote, inategemea na mali za muhusika,” anasisitiza.

Makala haya yametoka Februari 8, 2018 katika gazeti la MTANZANIA ambalo nalitumikia.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement