Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement
Picha na mtandao

Na Veronica Romwald, Dar es Salaam

UJAUZITO wa Miriam James mkazi wa Dar es Salaam ulipatwa na misuko suko mingi, ulipofikisha umri wa miezi mitano ulionesha dalili za hatari.

Miriam anasema ujauzito wake ulitaka kuharibika katika kipindi hicho alikuwa akisumbuliwa mno na mamumivu ya tumbo mara kwa mara.

“Tuliogopa, ilipofika miezi saba mume wangu aliona vema nije huku Muhimbili ili madaktari waniangalie kwa ukaribu, nililazwa wodini (baby rest),” anasema.

Anasema bado aliendelea kupata maumivu ya tumbo madaktari wake wakashauri ni muhimu afanyiwe upasuaji ili kumtoa mtoto.

“Hivyo, nilijifungua mtoto njiti… nilikaa mno wodini nikiendelea kujiuguza na wakati huo madaktari wakiendelea kumuhudumia mtoto wangu.

“Wasiwasi wangu mkubwa ulikuwa juu ya kupona kwake… alikuwa mdogo mno, namshukuru Mungu, madaktari walijitahidi kumuhudumia na afya yake iliimarika tukaruhusiwa kurejea nyumbani,” anasema.

Anaongeza “Si kazi rahisi kulea mtoto njitii, inahitaji moyo wa uvumlivu, wakabiliwa na matatizo mengi, kuna kipindi huwa anaishiwa damu mara kwa mara hivi sasa ametimiza mwaka mmoja na miezi saba.

Jinsi ilivyo

Kibaiolojia mtoto huishi ndani ya tumbo la mama kwa kipindi cha miezi tisa tangu kutungwa mimba hadi kuzaliwa kwake.

Lakini wakati mwingine huweza kutokea mtoto akazaliwa kabla ya kipindi hicho kukamilika wengi wetu tunawaita watoto njiti.

“Mara nyingi ngozi yao huwa haijakomaa. Ingawa viungo vyote vya ndani ikiwamo moyo, figo, ini, mapafu na vinginevyo huwa vimeumbwa tayari ila navyo huwa bado havijakomaa,” anasema Daktari Bingwa wa Watoto wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Robert Moshiro.

Anafafanua “Kwa kawaida mtoto hukamilika kuumbwa viungo vyake ndani ya wiki 24  tangu mimba ilipotunga lakini zile ogani za ndani huwa bado hazijakomaa.

“Viungo hivyo hukomaa katika zile wiki 12 za mwisho za ujauzito, mtoto huendelea kupokea virutubisho vyote muhimu kutoka kwa mama yake ili kuwezesha kukamilika kwa viungo vyake,” anabainisha.

Anasema baada ya kumalizika kwa wiki hizo 12 za mwisho za ujauzito hapo mtoto huwa na uwezo wa kupumua mwenyewe kwa sababu tayari mapafu yake huwa tayari yamekamilika vema.

“Kila kiungo hufanya kazi yake sawa sawa hata figo zake huwa zinakuwa na uwezo wa kuchuja vizuri kwani zimekamilika,” anasema.

Anasema lakini ikiwa mtoto atazaliwa kabla ya muda huo kukamilika hukabiliana na matatizo mengi kwani viungo vyake vinakuwa bado havijakomaa.

Dk. Moshiro anasema hali hiyo hutokea kwa sababu anakuwa amekuja kwenye mazingira ambayo anakuwa hawezi kukabiliana nayo.

Hali mbaya zaidi

“Kwa mfano mtoto aliyezaliwa kabla ya muda (njiti) huku akiwa chini ya kilo moja ndani ya siku tatu (tangu azaliwe) mishipa yake ya damu huwa ni laini sana.

“Hivyo, huwa kwenye uwezekano mkubwa wa kuvuja damu na hata mishipa yake kupasuka au kuvilia damu.

Matatizo ya ubongo

Anasema hali hiyo ikiwa itatokea kichwani huweza kusababisha ubongo wa mtoto kushindwa kufanya kazi inavyotakiwa.

“Ubongo wa mtoto huwa una-fail… matokeo yake anaweza kupoteza maisha kabisa au ikiwa ataishi basi anakuwa na matatizo ya ubongo katika maisha yake,”
anabainisha.

Madhara mengine

Daktari huyo anasema watoto wengine hupata matatizo mbalimbali kama vile ya usikivu (uziwi), ulemavu wa kudumu wa kuona na mengineyo.

“Lakini wakati mwingine matatizo hayo huweza kutibika ikiwa yatagundulika mapema,” anabainisha.

Anaongeza “Anapozaliwa kabla ya muda zile chembechembe za damu ambazo husaidia kinga ya mwili huwa nazo bado hazijakomaa.

“Kutokana na hali hiyo huwa anakuwa kwenye uwezekano mkubwa wa kupata maambukizi ya vijidudu.

“Maambukizi hayo huweza kumsababishia kupata homa ya uti wa mgongo, ambayo huenda pia kuharibu ubongo,” anasisitiza.

Anasema mtoto aliyezaliwa kabla ya muda huwa pia yupo kwenye uwezekano mkubwa wa kupata homa ya manjano.

“Kwa sababu ini lake huwa bado halijakomaa hivyo hushindwa kuondoa ile manjano na ikiwa itaenda kwenye ubongo huuharibu kabisa,” anasema.

Anaongeza “Huwa kunajitokeza changamoto nyingi mno… unaweza kujitahidi kwa kila namna kumtunza mtoto lakini matatizo haya yakaja kujitokeza katika
kipindi cha ukubwani.

Umri wa mimba

Anasema matatizo mengi yanayowakabili watoto waliozaliwa kabla ya muda mara nyingi huendana na umri wa mimba.

“Yaani, kwa mfano mtoto akizaa katika wiki 34 ya mimba maana yake anakuwa amebakiza wiki nne afike mwisho, mtoto huyu huwa na tofauti kubwa na mtoto
atakayezaliwa katika wiki 28 ya mimba.

“Hivyo, matatizo atakayoyapata mtoto atakayezaliwa katika wiki 28 ni makubwa zaidi kuliko ya mtoto atakayezaliwa wiki 34,” anasema Dk. Moshiro.

Hula kwa shida

Anaongeza “Jinsi ya kumlisha mtoto aliyezaliwa kabla ya muda nayo ni changamoto kubwa hasa aliyezaliwa katika kipindi cha wiki 28.

“Mara nyingi hawa ule mfumo wao wa chakula huwa nao haujakaa vizuri (haujakomaa) kuweza kumeng’enya maziwa ya mama, kwa sababu alikuwa lazima
aendelee kutegemea kondo la mama kupata chakula.

“Lakini akishazaliwa tunakuwa hatuna jinsi lazima tumlishe chakula… huwa tunawaangalia jinsi wanavyoweza kupokea yale maziwa akipokea vizuri tunaendelea kumpa,” anasema.

Anasema lakini hatua hiyo huwa inamuweka mtoto kwenye uwezekano wa kupata matatizo ikiwamo kuoza utumbo.

“Hii ni kwa sababu ule mfumo wake unakuwa haujakomaa… na ili uweze kuimarika huweza kuchukua hata wiki nzima,” anabainisha.

Mama huathirika

Anasema kutokana na changamoto hizo ambazo mtoto hukabiliana nazo mara nyingi humsababishia mama naye kuathirika kwa namna moja au nyingine.

“Kwanza jamii huwa inamchukulia tofauti, wapo watakamnyooshea kidole kutokana na kujifungua mtoto kabla ya muda,” anasema.

Anasema hali hiyo huweza kumsababishia mama kupata msongo wa mawazo tena hasa anapokuwa akitafakari juu ya uwezekano wa mtoto wake kupona.

“Kwa sababu wengi wanajua mtoto aliyezaliwa kabla ya muda huwa na uwezekano wa kufariki dunia wakati wowote, huwa tunatumia nguvu kubwa kuwatuliza,” anabainisha.

Anaongeza “Kwa sababu akiwa na msongo wa mawazo, maziwa yanakuwa hayatoki kutosheleza mahitaji ya mtoto na watoto hawa huwezi kuwapa chakula kingine
zaidi ya maziwa ya mama pekee.

“Kusema ule ukweli, wakina mama hawa (wanaojifungua watoto kabla ya muda) huwa wanapata shida mno, mara nyingi huwa wanalazimika kukaa muda mrefu
wodini.

“Ule muda anaokaa hospitalini ni mwingi kwa mfano unakuta analazimika kukaa hadi wiki sita tangu ajifungue ikiwa mtoto amezaliwa na kilo moja.

“Mtoto wake akiendelea vema huyo atakaa kidogo kama miezi miwili hadi mitatu tunamruhusu kurudi nyumbani lakini kama haendelei vizuri ataendelea kukaa wodini tukiangalia hali yake na mtoto wake,” anasema.

Daktari huyo anasisitiza kwamba kupona au kutokupona kwa mtoto mara nyingi hutegemeana na umri wake tangu alipozaliwa.

Takwimu

Anasema kwa kawaida asilimia 20 hadi 25 pekee ya watoto ambao huzaliwa kabla ya muda wakiwa na kilo moja huwa wanapona.

“Hata hivyo, ukienda sehemu ambayo hakuna huduma za kibingwa kwa ajili ya kuhudumia watoto hawa kama ilivyo hapa Muhimbili tatizo huwa ni kubwa zaidi,” anasema.

Anasema watoto waliozaliwa kabla ya muda wakiwa na zaidi ya kilo moja uwezekano wa kupona nao huongezeka.

“Asilimia 40 hadi 50 huwa wanapona, na wale waliozaliwa juu ya hapo huwa wanapona vizuri kabisa hasa wale wenye kilo mbili na zaidi,” anabainisha.

Anaongeza “Hii ni tofauti na watu wengi kwenye jamii wanavyoamini… hakuna ukweli wowote kwamba mtoto akizaliwa mimba ikiwa katika mwezi wa nane anafariki na kwamba Yule anayezaliwa katika mwezi wa saba anaishi.

“Ukweli ni kwamba anayezaliwa katika mwezi wa saba wa mimba ana uwezekano mkubwa zaidi wa kufariki dunia kuliko yule aliyezaliwa katika mwezi wa nane wa mimba,” anabainisha.

Majanga

Dk. Moshiro anasema changamoto kubwa ambayo wanaiona ni kina mama wengi kushindwa kujua umri wa mimba.

“Tanzania hii ni changamoto, kina mama wengi hawajui umri wa mimba… na si kina mama wote wanafanikiwa kufanya ultra sound.

“Kipimo hicho kinaweza kutusaidia kujua umri wa mimba ikiwa kitatumika kwa uchunguzi katika wiki ya 18.

“Ndiyo maana tunshauri kina mama kuwahi kliniki wanapojihisi kuwa huenda wana ujauzito lakini wapo ambao huja hospitalini tayari na hali ya uchungu unakuta kumbe walipitiliza mwezi bila kujua,” anabainisha.

Hali halisi MNH

Katika kipindi cha mwaka 2016/17 watoto wachanga wapatao 7,372 walilazwa katika  katika Kitengo cha Watoto Wachanga Muhimbili.

Kati ya watoto hao njiti walikuwa 1,313 sawa na asilimia 31.4.

Idadi ya watoto njiti waliofariki katika kitengo hicho kwa mwaka 2016/17 ni 543 sawa na asilimia 7.4 ukilinganisha na asilimia 19.8 ilivyokuwa mwaka 2015/16.

Watoto njiti 65 walipatiwa dawa ya kukomaza mapafu katika mwaka 2016/17 huku idadi ya watoto waliolazwa kwenye wodi ya kangaroo mwaka 2016/17 ikiwa 483.

Idadi hiyo imeongezeka kutoka mwaka jana ambayo walikuwa watoto 399.

Takwimu hizo zilitolewa Novemba 17, mwaka huu na Mkurugenzi wa Tiba Muhimbili, Dk. Hedwiga Swai wakati wa maadhimisho ya Siku ya Mtoto Njiti Duniani.

Dk. Swai anasema idadi ya watoto waliolazwa kwenye wodi ya kangaroo walikuwa kati ya gramu 500 na kilo 1.5.

“Idadi kubwa ya watoto waliotunzwa katika wodi hiyo walifanikiwa kutoka wodini na uzito wa kilo 1.6 hadi 1.7 ambayo ni sawa na asilimia 99.5 ya watoto wote waliokuwa wamelazwa,” anasema.

Anasema hayo ni mafanikio makubwa waliyopata katika kipindi cha mwaka mmoja hasa kupunguza idadi ya vifo vya watoto hao.

“Tumepata mafanikio makubwa kwa kuwapo huduma ya kangaroo, tumeweza kupunguza idadi ya vifo kutoka asilimia 19.8 mwaka jana hadi kufikia asilimia 7.4, vifo vya ghafla kutokana na kupaliwa maziwa navyo vimepungua kwa asilimia 99.

“Muda wa kukaa wodini nao umepungua pia ukilinganisha na wale wanaokaa kwenye incubator, kwa kangaroo watoto hupata nafuu haraka kuliko wale waliokaa kwenye incubator.

“Kwa njia ya kangaroo mtoto hunyonya kwa ukaribu na huwa faraja kubwa kwa mama, tumeweza kupunguza msongamano wa watoto katika wodi yetu,” anabainisha.

Changamoto

Anasema ni upungufu wa vifaa tiba ukilinganisha na idadi ya watoto wanaopokea na kwamba hiyo inatokana na huduma ya kangaroo kutokutewa katika hospitali nyingine.

“Ufinyu wa wodi ya kangaroo ukilinganisha na idadi ya watoto ikizingatiwa wengi kwa sasa wana uwezo wa kuishi hata wale wenye kilo ndogo kama vile gram 700,” anasema.

Anataja changamoto nyingine kuwa ni gharama kubwa ya kununulia dawa za kukomaza mapafu na idadi ndogo ya wauguzi na madaktari ukilinganisha na idadi ya watoto.

“Tunatoa wito kwa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kuongeza vitengo vya kutunzia watoto njiti katika hospitali nyingine kwani huduma hii ni rahisi, haihitaji gharama kubwa na imeweza kupunguza vifo vya watoto njiti kwa asilimia kubwa,” anasema.

Wizara

Mkurugenzi wa huduma za Kinga wa Wizara hiyo, Dk. Neema Rusibamayila anasema takwimu zinaonesha asilimia 13 hadi 17 ya watoto nchini huzaliwa njiti.

“Hivyo, serikali kupitia Wizara hii imekuwa ikiratibu program mbalimbali lengo ni kupunguza idadi ya vifo vya watoto wachanga na wale walio chini ya umri wa miaka mitano.

“Program hizo ni pamoja na kumsaidia mtoto kupumua baada ya kuzaliwa, kupanua huduma za watoto wachanga kwa kujenga wodi katika hospitali za Manispaa na Wilaya na kutoa mafunzo kwa wahudumu wa afya namna ya kuhudumia watoto wachanga (essential newborn care),” anasema.

Anaongeza “Ingawa program hizi zimekuwa na mafanikio makubwa bado tuna changamoto kuhakikisha tunazidi kupunguza zaidi idadi ya vifo hivi.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement