Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement

Image result for taasisi ya ocean road



*Fedha hizo zimetoka katika Chama cha Tiba ya Saratani cha nchini Marekani.


Na Mwandishi Maalum, Dar es Salaam


Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI) hivi karibuni imeshinda msaada wa fedha za utafiti na ubunifu kutoka Chama cha Tiba ya Saratani cha Nchini Marekani (ASCO) kupitia shindano lijulikanalo kama (International Innovation Grant – IIG).


Hatua hiyo ni kwa ajili ya kutekeleza mpango wa kinga ya saratani ya ngozi kwa watu wenye ulemavu wa ngozi nchini Tanzania. 


Daktari Fidel Rubagumya ambaye ni mfanyakazi wa Idara ya Taaluma na Utafiti ya ORCI ndiye ambaye aliomba fedha hizo za utafiti mwaka 2017 katika shindano hilo la kimataifa lililotangazwa na ASCO.


Desemba, 2017 ORCI ilitangazwa mshindi wa fedha hizo kwa ajili ya utafiti na ubunifu ikiwa ni taasisi pekee Barani AAfrika kushinda kwenye shindano hilo, taasisi nyingine mbili zilizoshinda ni kutoka nchi za Mexico na India.Image result for taasisi ya ocean road

Akizungumza na mtandao huu mapema leo, Mkurugenzi Mtendaji wa ORCI (Pichani), Dk. Julius Mwaiselage amesema mradi huo wa utafiti wenye jina la ‘Use of Smartphone application for early detection of skin cancers in people with albinism’ unalenga kupunguza matukio ya ugonjwa na vifo vitokanavyo na saratani ya ngozi kwa watu wenye ulemavu wa ngozi nchini kwa kupitia simu zinazotumia teknolojia ya kisasa.


Amesema kila mwaka, ASCO kupitia IIG, huitisha mapendekezo ya mawazo bunifu ya utafiti yanayolenga kuboresha matibabu ya saratani kwenye nchi za kipato cha chini na cha kati ambayo yataweza pia kufanyiwa kazi katika mazingira yanayofanana kwenye nchi nyingine zinazoendelea.


“Mradi unaofadhiliwa kwa msaada huu wa fedha za utafiti utaodumu kwa kipindi cha mwaka mmoja utatekelezwa kwa ushirikiano kati ya ORCI na Chama cha Watu Wenye Ulemavu wa Ngozi Nchini Tanzania (TAS).


“Ni matarajio yetu kwamba mafanikio ya mradi huu hapa Tanzania yatasaidia utekelezaji wa mradi kama huu kwenye nchi nyingine Barani Afrika zinazopambana na tatizo la saratani ya ngozi miongoni mwa watu wenye ulemavu wa ngozi,” amesema.


Amesema utafiti wa ORCI unaonesha kwa mwaka 2016 pekee kulikuwa na wagonjwa wapya 177 wa saratani ya ngozi, na 95% ya wagonjwa hao ikiwa ni watu wenye ulemavu wa ngozi.


“Kutokana na udhaifu katika ngozi zao, pamoja na kuchangiwa na kuchomwa na mionzi mikali ya jua, wengi wa watu wenye ulemavu wa ngozi wataathiriwa na saratani ya ngozi iwapo hatua maalum za kuwakinga dhidi ya ugonjwa huo hazitochukuliwa.


“Kwa kuzingatia hilo, uchunguzi na kugundulika kwa saratani ya ngozi ikiwa katika hatua za awali itakuwa ni njia kuu ya kuhakikisha kuwa wagonjwa wa saratani ya ngozi wanagundulika mapema na wanapewa rufaa ya kwenda ORCI ili kuanza matibabu haraka iwezekanavyo.  


“Utaratibu uliozoeleka hapo awali katika kuchunguza saratani ya ngozi unakabiliwa na changamoto za huduma hizo kuwa mbali na jamii na ucheleweshaji wa rufaa kwa wagonjwa kwenda hospitali kupata matibabu.

Mtoto mwenye ulemavu wa ngozi akiandikishwa jina lake kwa ajili ya uchunguzi na matibabu ya saratani ya ngozi hivi karibuni katika Taasisi ya Ocean Road wakati wa maadhimisho ya Siku ya Saratani Duniani.

"Hivyo basi utaratibu huu mpya wa kutumia simu za mkononi tutahakikisha kuwa huduma za uchunguzi zinapatikana kwenye jamii husika kwa kutumia mbinu ya kupiga picha vidonda vilivyoleta mashaka kwenye ngozi na kuzituma kwa madaktari.


"Program hii ya simu za mkononi itasaidia kupiga picha za vidonda vilivyoleta mashaka kwa kuambatanisha na maelezo binafsi ya mgonjwa kisha kuzihifadhi picha hizo kwa njia ya mtandao," amesema Dk Nazima Dharsee, Mkurugenzi wa Idara ya Taaluma na Utafiti, ORCI.


Ameongeza “Picha hizo zitachunguzwa mtandaoni na wataalamu wa ngozi na saratani, kisha kufanyiwa uchunguzi zaidi wa kitabibu. Wagonjwa watakaogundulika kuwa na vidonda visivyo vya kawaida watapelekwa hospitali kuthibitisha kama wameathiriwa na saratani ya ngozi, ambapo watakaokutwa na tatizo hilo watapewa matibabu stahiki.”

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement