Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement


*Mwaka huu kufanya tena kampeni Kitaifa 
*Lengo kuwafikia watoto milioni nne 

Na Veronica Mrema - Dar es Salaam

HUENDA miongoni mwetu wapo watu ambao ukiwauliza leo hii polio ni ugonjwa gani?, wasiweze kukupatia majibu hasa wale waliozaliwa kuanzia miaka ya 1990 hadi sasa.

Inawezekana pia wakawepo baadhi ambao wataweza kukupa majibu polio ni ugonjwa gani, dalili zake ni zipi? kwa ufahamu walionao baada ya kuusoma kwenye vitabu na majarida mbalimbali lakini si kwa kuufahamu kiuhalisia.

Hili lipo wazi kwani kwa miaka ipatayo 23 sasa nchini mwetu hakuna mtu yeyote aliyebainika kuathiriwa na ugonjwa huo.

Mafanikio hayo ni kutokana na juhudi kubwa zilizofanywa na Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa masuala ya chanjo kwa kuhakikisha inaimarisha huduma za upatikanaji wa chanjo dhidi ya ugonjwa huo na mengineyo.

POLIO NI NINI?

Ni muhimu kufahamu hili, kwa mujibu wa wataalamu wa afya wanaeleza ni ugonjwa wa kuambukiza ambao husababishwa na virusi ambavyo hushambulia, huathiri mishipa ya fahamu (neva) na kusababisha ulemavu wa kudumu (mwili kupooza) au kifo.

Virusi hivyo hupatikana kwenye kinyesi cha binadamu, huingia mwilini mwake kupitia kinywani kwa njia ya kula chakula au kunywa kinywajikilichoathiriwa na virusi hivyo.

Wataalamu wa afya wanaeleza takriban asilimia 90 hadi 95 ya watu wanaopata maambukizi ya ugonjwa huo huwa hawaoneshi dalili zozote.

Ni asilimia tano hadi 10 ya watu ndiyo ambao huonesha dalili za homa, maumivu ya kichwa, kutapika, kuharisha, mishipa ya shingo kukaza na maumivu katika miguu na mikono.

Hali hiyo hutokana na virusi hivyo vinapofika kwenye tumbo huweza kusafiri hadi kwenye ubongo na uti wa mgongo ambapo mgonjwa huweza kuhisi maumivu ya kichwa, kukakamaa kwa shingo pamoja na maumivu ya miguu na mikono.

Kwa kawaida watu hawa hurejea katika hali ya kawaida baada ya wiki moja au mbili, asilimia 0.5 ya waathrika huweza kupata udhaifu wa misuli suala linalosababisha kushindwa kutembea.

Hali hiyo huweza kutokea katika masaa kadhaa baada ya maambukizo.

Virusi vya polio vinapofika tumboni huweza kuzaliana na kuongezeka, hivyo kuanza kushambulia neva na kusababisha mgonjwa kupooza baadhi ya viungo.

HUATHIRI WATOTO

Ugonjwa huu, huwapata zaidi watoto walio chini ya umri wa miaka miwili kuliko wale ambao wameshavuka umri huo.

Ingawa ni asilimia ndogo sana ya wanaopatwa na polio huweza kupata ulemavu wa mwili wa kudumu, lakini hatari hiyo inalazimu ugonjwa huo kupewa umuhimu mkubwa na kuzuiwa kupitia chanjo.

HALI ILIVYO NCHINI

Meneja wa Mpango wa Taifa wa Chanjo, Dk. Dafrosa Liymo anasema hapa nchini tangu mwaka 1975 Serikali ilianza kutoa aina tatu za chanjo hadi kufikia 2018 ziliongezeka kufikia tisa.

Anasema chanjo hizo tisa zinazotolewa zinawakinga watoto dhidi ya magonjwa 13 ikiwamo, surua-rubella, saratani ya mlango wa kizazi, kifua kikuu, kifadulo, pepo punda na homa ya ini na mengine.

“Ni jukumu la Serikali kuhakikisha chanjo zipo na zinapatikana kwa wakati, hadi sasa hatuna upungufu wa chanjo nchini,” anasema Dk. Dafrosa.

Anasema tangu mwaka 1996 Tanzania ni miongoni mwa nchi zinazotambulika duniani na WHO kwamba haina mgonjwa mwenye polio.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu anasema mafanikio hayo yamepatikana kutokana na matumizi ya chanjo.

Anabainisha kila mwaka Serikali huipatia wizara hiyo kiasi cha Sh bilioni 30 kwa ajili ya ununuzi wa chanjo mbalimbali,” anasema.

Waziri Ummy anasema kwa kuwapa watoto chanjo idadi ya vifo vya watoto chini ya miaka mitano imepungua kutoka vifo 112 katika kila vizazi hai 1000 hadi kufikia vifo 67 kwa kila vizazi hai 1000 hivi sasa.

“Kwa msingi huo, Serikali itaendelea kuwekeza katika masuala ya chanjo kwani tafiti zinaeleza katika kila dola moja ambazo Serikali huwekezwa kwenye chanjo ili kukinga watu wake dhidi ya magonjwa huokoa dola 16 ambazo hutumika kutibu magojwa,” anasema.

Anaongeza “Serikali itaendelea kuchukua hatua zote kuhakikisha tunawakinga wananchi dhidi ya magonjwa, tutaendelea kufanya usafi wa mazingira vile vile tutaendelea kutoa chanjo.

“Hivyo, kadri maendeleo ya kisayansi na kiteknolojia yanavyopatikana ndivyo na sisi tutakavyojiridhisha na kuhakikisha tunapata chanjo ili kukinga wananchi wetu,” anasema.

Anaongeza “Mwaka 2020 tunatarajia kufanya utafiti wa Kitaifa kuhusu hali ya afya tunaamini kwa uwekezaji mkubwa uliofanyika idadi ya vifo itakuwa imepungua zaidi.

“Mafanikio yanaonekana wazi, kwa mliokuwa miaka ya nyuma mtakumbuka zilianzishwa kambi maalum kwa ajili ya kuhudumia watoto wenye tatizo la kuhara, kwa kuwekeza kwenye chanjo leo hii magonjwa ya kuhara, kifaduro na mengine tumeweza kuyadhibiti,” anasema.

HALI ILIVYO DUNIANI

Shirika la Afya Duniani (WHO) linaeleza hadi sasa bado hakuna dawa inayoweza kutibu ugonjwa wa polio, ila unazuilika kwa kuhakikisha watu wanapatiwa chanjo.

WHO linaeleza katika miaka ya 1980 ugonjwa huo ulikuwa ukiathiri takribani watu 350,000 katika nchi 125 kila mwaka.

Kutokana na hali hiyo, mwaka 1988 juhudi za kuangamiza ugonjwa huo zilianza tangu hapo idadi ya maambukizi imepungua kwa asilimia 99.

Takwimu zinaeleza hadi kufikia 2013 watu 416 duniani ndilo walibainika kuathiriwa na ugonjwa huo ikilinganishwa na 1980.

Mafanikio hayo yametokana na kupewa umuhimu chanjo kwa watoto takribani katika maeneo yote duniani suala lililoleta matumaini ya kutokomezwa ugonjwa huo.

Lakini tangu mwaka 2014 ugonjwa wa polio bado umebaki kuwa tatizo katika nchi za Afghanistan, Nigeria na Pakistan.

KAMPENI TANZANIA

Dk. Dafrosa anasema chanjo dhidi ya polio imeendelea kutolewa nchini japo hakuna mgonjwa ili kuendelea kuwakinga watoto.

“Kila mwaka huwa kuna wiki ya chanjo, kule katika Halmashauri huwa tunatoa chanjo hii ambayo ipo katika mfumo wa matone, aidha, mwaka 2010/11 tulifanya kampeni ya kutoa chanjo hii katika mikoa ambayo ilikuwa na kiwango kidogo cha utoaji chanjo,” anasema.

Anaongeza “Mafanikio ya kuudhibiti ugonjwa wa polio ni kutokana na mwitikio mkubwa wa wananchi ambao walijitokeza na kuleta watoto wao tukawapatia chanjo.

“Hivyo, tunaendelea kuhamasisha wananchi kuendelea kuleta watoto ili wapatiwe chanjo, maana bado kuna nchi ambazo zina mzunguko wa kirusi pori cha polio, ikiwamo Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Afghanistan, Pakistani na Nigeria.

“Kwa kuwa nchi yetu ina urafiki na tunapokea wageni wengi, ndiyo maana tunazidi kujikita kuhakikisha watoto wanapatiwa chanjo ili kuimarisha kinga,” anasema Dk. Dafrosa.

Anasema Tanzania bado inaendelea kufanya uchunguzi kila mara inapobainika yupo mtu ambaye amepata ulemavu wa ghafla.

“Yale mafriji yaliyopo hapa ofisi za mpango wa Taifa wa Chanjo, ni maalum kwa ajili ya kutunza sampuli za wale ambao wanaripotiwa kupata ulemavu wa ghafla.

“Tunatoa rai pale wananchi wanapoona mtu amepata ulemavu wa ghafla wampeleke hospitalini na sampuli yake iletwe ili tuichunguze, kwa sababu kirusi kinabebwa na kinyesi, kinaweza kuenezwa hata na wageni,” anasema.

Waziri Ummy anasema Septemba 26 hadi 30, mwaka huu Serikali kupitia Wizara hiyo itafanya kampeni ya Kitaifa nchi nzima abapo itatoa chanjo dhidi ya ugonjwa wa Surua-Rubella na polio.

“Kampeni itafanyika nchi nzima, kitaifa itazinduliwa Mkoani Morogoro katika Viwanja vya Jamhuri,” anabainisha.

Anaongeza “Japo kila siku chanjo hizi zinatolewa katika vituo vya afya, takwimu zinaeleza tumeweza kufikia watoto kwa kiwango cha asilimia 98 pekee.

“Hii inamaanisha katika kila watoto 100 tumewafikia 98, watoto wawili bado hatujawafikia, changamoto ipo zaidi maeneo ya mikoa iliyopo pembezoni mwa nchi,” anasema Waziri Ummy.

Anaongeza “Hivyo, kampeni kubwa ya kitaifa namna hii inakuwa ni sehemu ya kuongeza nguvu kuhakikisha tunamfikia kila mtoto anayestahili kupatiwa chanjo.

Anasema katika kampeni hiyo wanakusudia kuwafikia watoto milioni nane wenye umri miezi tisa hadi 59 ambao watapatiwa chanjo ya surua-rubella na watoto milioni nne wenye umri wa miezi 18 hadi 42 watapatiwa chanjo ya polio.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement