Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement


Na Veronica Mrema - Dar es Salaam
 

KWA asilimia 99 saratani ya matiti huathiri kundi la wanawake duniani, wanaume ikiwa ni asilimia moja pekee, kulingana na takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO).

Lakini pamoja na ukweli huo, kundi la wanaume linashauriwa kwamba halipaswi kubaki nyuma katika suala zima la uchunguzi wa afya ya matiti yao.

Hii ni kwa sababu ikiwa mwanaume anakabiliwa na saratani hii na hatagundulika mapema huwa kwenye hatari zaidi kuathiriwa mapafu yake kuliko ilivyo kwa kundi la wanawake.

“Kwa wastani hapa hospitalini kwa mwaka, huwa tunaona wanaume wapatao 18 wanaokabiliwa na saratani hii,”.

Anasema Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Saratani katika Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI), Crispin Kahesa.

Anaongeza “Ingawa huathiri asilimia moja ya wanaume hata hivyo kwa upande wao ni hatari zaidi isipogundulika mapema kwani huweza kuathiri mapafu yao kwa haraka.

“Changamoto kubwa tunayoiona ni kwamba katika hao tunaowagundua wengi hufika hospitalini hapa wakiwa wamechelewa na ugonjwa ukiwa katika hatua ya juu,” anasema.

Dk. Kahesa ambaye pia ni Mkurugenzi wa Huduma za Kinga ya Saratani katika taasisi hiyo anasema hali hiyo hutokea kwa sababu wanaume wengi bado hawalipi kipaumbele titi kama ilivyo kwa wanawake.

“Kwa mfano, wanaume wengi hata wanapohisi kuna uvimbe hudhani ni hali ya kawaida tena hasa ikiwa uvimbe huo hauwasababishii maumivu yoyote,” anasema.

Anaongeza “Hudhani ni hali ya kawaida lakini la hasha! Jambo la msingi wanalopaswa kufanya ni kuwahi hospitalini kwa uchunguzi zaidi.

“Ili kama uvimbe ule ni saratani wapate matibabu mapema,” anasisitiza.

ISMAIL AFUNGUKA

Hivi karibuni katika Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI), Juma Ismail (50), Mkazi wa Gongo la Mboto, alikuwa miongoni mwa waliopanga foleni kwenda chumba cha daktari, kuchunguzwa saratani ya matiti.

“Mke wangu ndiye aliyekuja kunieleza kwamba kuna uchunguzi unafanyika hapa Mloganzila, alinieleza madaktari wanasema wanaume pia tunaweza kuathiriwa na saratani hii.

“Sikuwa najua kabla kwamba hili linawezekana, nikaona vema nije nichunguzwe maana wanasema ikigundulika mapema ni rahisi kutibika na kupona,” anasema. 

Anasema elimu aliyopatiwa imemfungua mengi kuhusu saratani hiyo na kwamba atakwenda kuelimisha vijana wake nyumbani. 

“Nimejaliwa kupata watoto wa kiume watatu, nitakwenda kuwaelimisha na ikiwezekana nao waje wachunguzwe, ni muhimu kufanya uchunguzi kuliko kusubiri mpaka athari zake zijitokeze,” anasema Ismail.

 DALILI ZIPOJE KWA WANAUME?

Dk. Kahesa anafafanua “Ni rahisi kugundua saratani ya matiti kwa wanaume kuliko kwa wanawake na kwamba dalili za saratani ya matiti kwa wanaume ni tofauti kidogo na wanawake.

“Jinsi mwanamke alivyoumbwa, kifua chake mafuta mengi kuliko cha mwanaume ndiyo maana huwa si rahisi kugundua.

"Lakini kwa sababu mwanaume ana mafuta kiasi kifuani, ni rahisi hata uvimbe unapotokea anaweza kuwahi kugundua kwa sababu huwa unaonekana haraka sana.

“Lakini, nimeeleza awali kwamba changamoto iliyopo, wengi wanapohisi uvimbe hudhani ni hali ya kawaida kwa sababu mara nyingi katika hatua za awali huwa hauna maumivu.

"Ni kwa sababu hiyo wengi huchelewa kuja hospitalini kwani huwa wanachelewa pia kufikia ile hali ya chuchu kuanza kutoa majimaji au damu,” anasema.

Dk. Kahesa anaongeza "Saratani ya matiti ni hatari kwa kina baba kifua chao hakina nyama nyingi ni rahisi kuhamia kwenye mapafu na kuyaathiri, tatizo ni kwamba wengi huwa wanaona aibu kuonesha titi kufanyiwa uchunguzi.

WALIO HATARINI

Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Saratani wa Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI), Sikudhani Muya anasema kwenye taasisi hiyo, Saratani ya matiti inashika namba mbili kwa idadi ya wagonjwa wanaowaona kliniki. 

“Kundi la wanaume walio hatarini zaidi kupata saratani hii ni wale ambao kwenye familia zao kuna historia kwamba wamewahi kupata mgonjwa wa saratani hasa hii ya matiti,” anabainisha.

Dk. Muya anaongeza “Saratani hiyo huwakumba zaidi wenye umri kuanzia miaka 50 na kuendelea, hivi sasa tunaona wagonjwa hadi wale wenye umri wa kuanzia miaka 20 na kuendelea.

UCHUNGUZI UNAVYOFANYIKA

“Huwa tunafanya kwanza uchunguzi wa awali kwa kulikagua titi, tunapobaini wenye viashiria vya awali huwa tunawaweka kwenye hatua inayofuata ya uchunguzi.

“Tunafanya tena uchunguzi wa kina kwa kutumia mashine ya X- ray au ultra sound ya matiti kulingana na umri wa muhusika na vipimo.

"Hivyo hutuwezesha kujua iwapo viashiria hivyo ni ugonjwa au la! Maana si kila vivimbe ni saratani," anabainisha Dk. Muya.

KWA WANAWAKE

“Wanawake ndiyo wanaathirika zaidi kwa sababu ya maumbile wana chembechembe zaidi za matiti na wana vile vimeng'enyo ambavyo vinaweza kusababisha zaidi wapate saratani ya matiti kuliko wanaume,”.

Anasema Daktari Bingwa wa Radiolojia MNH- Mloganzila, Lulu Sakafu.

Anaongeza “Kwa mfano, uchunguzi tuliofanya hapa Mloganzila, Oktoba 26 na 27, mwaka huu ikiwa ni sehemu ya kaudhimisha mwezi wa uhamasishaji.

"Uelimishaji na uchunguzi wa saratani ya matiti, walifika wanawake zaidi ya 160, kati ya hao zaidi ya 40 tuliwakuta na viashiria vya awali saratani hii.

“Hatukupata mwanaume hata mmoja aliyejitokeza kuja kufanyiwa uchunguzi, wanawake tuliowabaini tumewaingiza katika mfumo wa matibabu.

"Tutaendelea kuwafanyia vipimo zaidi ili tuweze kujua iwapo vile viashiria tulivyowakuta navyo ni  saratani ya matiti au la,” anabainisha.

Anasema sambamba na uchunguzi huo, waliwapa elimu jinsi kuhusu saratani hiyo, dalili zake na jinsi ya kujichunguza binafsi nyumbani maana wengi bado hawajui.

Dk. Kahesa anabainisha kwamba ORCI kwa mwaka huu pekee wameweza kuona wanawake 1443 ambapo kati yao 342 wamekutwa na uvimbe 170 walikuwa na dalili za awali za saratani hiyo.

“Katika hawa 170 tulipowafanyia vipimo zaidi 68 tuliwagundua  vivimbe vile walivyokuwa navyo tayari vilikuwa ni ugonjwa wa saratani,” anasema.

Anasema miongoni mwa wanawake hao wapo ambao tayari wamepatiwa matibabu ikiwamo za upasuaji na wengine za mionzi, wapo waliomaliza na wengine wanaendelea kuhudhuria kliniki.

WENGI NI WA-MIJINI

Dk. Kahesa anasema idadi kubwa ya wagonjwa ambao huwapokea ORCI huwa wanatoka katika maeneo ya mijini hasa katika majiji makubwa.

“Tunaona wengi wanatokea hapa Dar es Salaam, ukifuatiwa na mikoa ya kanda ya mashariki, nyanda za juu kusini (Mbeya) na Mwanza,” anabainisha.

VISABABISHI

Dk. Kahesa anasema kiujumla tafiti zinaonesha kasi ya magonjwa yasiyo ya kuambukiza ikiwamo hayo ya saratani inazidi kuongezeka duniani.

“Kuna ongezeko kubwa la unene uliokithiri, uzito mkubwa, matumizi ya poimbe, uvutaji wa sigara, na ulaji usiofaa hasa vyakula vyenye chumvi nyingi, mafuta mengi na vile vya viwandani,” anabainisha.

“Ni muhimu sasa jamii yetu kubadili mtindo wa maisha kwa kuzingatia ulaji unaofaa, kuepuka unywaji wa pombe, uvutaji sigara, kuzingatia kufanya mazoezi na kuchunguza afya mara kwa mara,” anashauri.

Mwakilishi wa Chama cha Madaktari Wanawake (MEWATA), Mkoa wa Pwani, Dk. Deograsia Mkapa anasema.

uelewa wa jamii kuhusu saratani ya matiti na nyinginezo umeongezeka hivi sasa tofauti na miaka ya nyuma.

"Tunazunguka maeneo mbalimbali nchini tumeshuhudia, mwamko ni mkubwa watu kujitokeza kuchunguzwa, tunaona fahari maana ndicho hasa MEWATA tumekuwa tunatamani kukiona. 

“Serikali imejitahidi mno kusogeza karibu zaidi na jamii huduma za uchunguzi wa magonjwa ya saratani hasa hii ya matiti na ile ya kizazi,” anasema.

Dk. Mkapa anaongeza “Miaka ya nyuma ilikuwa lazima watu waende Ocean Road lakini sasa hivi zinatolewa mpaka kwenye Hospitali za Rufaa za Mikoa, Wilaya na vituo vya afya maeneo mbalimbali nchini.

“Hivyo, tunaisisitiza jamii kwenda kufanyiwa uchunguzi kwa sababu ikigundulika mapema, hutibika na kupona,” anatoa rai.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement