Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement

NA VERONICA ROMWALD – DAR ES SALAAM

KITAALUMA si daktari, ni mhudumu wa Mochwari, hiki ni chumba maalum kinachotumika kuhifadhia miili ya marehemu ikisubiri uchunguzi na maandalizi (kusafishwa) kwa ajili ya maziko.

Ingawa ni chumba muhimu mno lakini kwenye jamii yetu wapo baadhi ya watu ambao hukiogopa na hata kuwashangaa wale wanaoamua kufanya kazi ndani ya chumba hicho.

Hata hivyo, wakati wengine wakiogopa kufanya kazi hiyo wapo wanaifanya na ndiyo inayowasaidia kuendesha maisha yao ya kila siku hapa duniani.

Miongoni mwao ni Seleman Mbiza (57), Mkazi wa Tandale jijini Dar es Salaam ambaye JAMVI LA HABARI limefanikiwa kufanya naye mahojiano haya.

Mbiza anasema tangu 1984 amekuwa akifanya kazi hiyo baada ya kushawishiwa na ndugu yake ambaye wakati huo alikuwa mhudumu wa mochwari katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH).

“Sikuwahi kufikiri wala kutarajia kwamba ipo siku nitakuwa muhudumu wa chumba cha kuhifadhia maiti (mochwari), awali nilikuwa mfanyabiashara, nikiuza kahawa kule maeneo ya uwanja wa ndege (kipawa).

“Nilianza rasmi kazi hii (mochwari) 1984 baada ya kushawishiwa na huyo ndugu yangu (si wa kuzaliwa tumbo moja, tulisoma wote Shule ya Msingi), alikuwa anafanya kazi hii hapa Muhimbili,” anasimulia

Anasema kabla ya kuanza kufanya kazi hiyo naye pia alikuwa anawashangaa wale waliokuwa wakiifanya na  alikuwa akiogopa kuingia ndani ya chumba hicho.

“Ndugu yangu huyo alikuwa kila akija kunitembelea ananisimulia na kunisisitiza kwamba si kazi ngumu na naweza hata mimi kuifanya,” anasimulia.

Mbiza anasema kuna wakati alikuwa anakwenda Muhimbili kumtembelea ndugu yake huyo na ndipo alipata nafasi kushuhudia jinsi ambavyo mwili wa marehemu huhifadhiwa.

“Taratibu nikajikuta naanza kupenda kazi aliyokuwa akiifanya, nikawa natafuta nafasi zaidi na kwenda kuangalia namna anavyofanya.

"Woga ukanitoka kabisa, nikaona ni jambo la kawaida na nikajikuta na mimi natamani kuifanya,” anasema.

Anaongeza “Nilikuwa nakuja na kuangalia anavyofanya kwa kipindi cha takribani mwaka mmoja, nikachukua hatua, nikaamua kuandika barua ya kuomba kazi kwa uongozi wa hospitali, ikapokelewa.

NDANI YA CHUMBA

Anasema aliitwa kazini mara moja na kuanza kipindi cha majaribio ambacho kilikuwa miezi sita kumpima uwezo wake wa utendaji kabla hajapewa mkataba.

“Sikuwa na hofu, wasiwasi wala woga kwa sababu tayari mazingira yale nilikuwa nimeshayazoea ingawa katika siku za mwanzo niliona ilikuwa ngumu kidogo,

".., yule ndugu yangu alinitia moyo kwamba ipo siku nitazoea kabisa,” anasimulia.

Anasema alikuwa akifanya kazi hiyo kwa kusimamiwa na madaktari waliobobea akiwamo Profesa Kitinye, Dk. Mushi na Profesa Kahaya.

“Kumbuka hadi nilipoomba hii kazi mimi sikuwa nimesomea, sijawahi kwenda darasani kusomea jinsi ya kuhudumia maiti wala chumba cha kuhifadhia maiti.

“Hivyo hao wataalamu watatu ndiyo walikuwa walimu wangu, walinifundisha pia miiko ya kazi hii kwamba natakiwa kuzingatia usafi na kuwa na lugha nzuri kwa wafiwa.

“Walinifundisha jinsi ya kubeba mwili, jinsi ya kuuosha, kuuweka dawa, kuhifadhi mochwari na yale yanayopaswa kufanyika wakati wa uchunguzi.

"Nilikuwa najifunza pia mambo mengi kupitia kwa yule ndugu yangu,” anasimulia.

Anaongeza “ Baada ya miezi sita ya majaribio kupita nilionekana kuwa ninaweza kufanya kazi hiyo, nikapewa mkataba.

NYAKATI NGUMU

Mbiza anasimulia wakati mgumu kwake katika kazi hiyo ni kipindi mwili wa marehemu unapokuwa ukifanyiwa uchunguzi kubaini kifo hasa ikiwa kinaonekana ni cha utata.

“Kwa hakika, kipindi cha ‘postmortem’  ndicho ambacho naona huwa ni kigumu, tena afadhali hivi sasa nina ule uzoefu awali ilikuwa changamoto kubwa mno kwangu.

“Maana daktari ataeleza wanahitaji kufanya uchunguzi, hivyo wanataka baadhi ya viungo vya marehemu kwa mfano moyo, figo, ini, matumbo ili wayachunguze, inabidi achanwe ili kupata viungo hivyo.

“Wanakueleza pa kuchana na kuvitoa lakini kabla ya kuchana lazima uvae mavazi maalum ya kujikinga kwa sababu kuna magonjwa mbalimbali ya kuambukiza.

“Kwa mfano, ikiwa marehemu inasadikika amekufa kutokana na ugonjwa wa tauni, baada ya kumaliza kazi hiyo lazima muhudumu amuone daktari kuna dawa maalum atampatia za kutumia ili kujikinga.

“Lakini wakati mwingine inaweza kutokea bahati mbaya muhudumu amemchana marehemu, kisu kikapitiliza na kumkata yeye pia, wanasema baada ya hapo lazima akachome sindano maalum,” anasimuliza.

Anaongeza “Ndiyo maana nasema kipindi cha uchunguzi huwa ni kigumu kwa sababu inabidi muhudumu uwe makini mno kuepuka madhara yanayoweza kutokea kwa namna moja au nyingine.

‘MIKWARUZANO NA WAFIWA’

“Mabosi wangu wana imani kubwa na mimi na siku zote nahakikisha nafanya kazi kwa weledi na kwa kuzingatia maadili na miiko, lakini wakati mwingine hutokea mikwaruzano ya hapa na pale na wafiwa.

“Naelewa sipaswi kukwaruzana nao lakini wakati mwingine huwa inatokea tu najikuta tumekwaruzana, basi kuna ambao nawaomba radhi wanaridhia.

"Lakini wengine huenda ofisi za utawala kulalamika, nimewajibu vibaya, naomba radhi, kwa sababu na mimi ni binadamu kuna wakati nakosea,” anasema.

Anaongeza “Kimsingi anayefanya kazi hii hapaswi kuwa mwenye ghadhabu ingawa wakati mwingine wafiwa wanaweza kumsababisha kughadhibika lazima ajifunze kuwa mtulivu na mvumilivu.

“Ukiwa mwenye ghadhabu ikatokea kwa mfano umempiga kofi mfiwa kumbe ni mgonjwa anaishia kudondoka na kufa unajikuta umepata kesi bila kutegemea, uvumilivu ni jambo la msingi,” anasema.

SHUGHULI ‘PEVU’ KUPATA MKE

Mbiza anasimulia kwamba haikuwa kazi rahisi kwake kupata mke wa kuoa na kwamba ilimlazimu kutumia mbinu mbadala kufanikisha nia yake hiyo.

“Kutokana na mtizamo uliopo kwenye jamii, muhudumu wa mochwari anaogopwa na kuonwa mtu asiye wa kawaida kumbe la!, kwa msingi huo niliona wazi nikipata msichana na kumueleza ninafanya kazi hiyo ni wazi atanikimbia.

“Hivyo niliamua kujiita daktari na kweli nilifanikiwa, nilipata mke ambaye nimebahatika kuzaa naye watoto wanane, awali hakubaini kabisa kwamba ninafanya kazi mochwari hadi siku nilipoamua kumueleza.

“Sasa anajua lakini hawezi kunikimbia kwa sababu kama ni maji tayari yameshamwagika,” anasema Mbiza na wote tunajikuta tukiangua kicheko.

MUDA WA MAITI MOCHWARI

Anasema kulingana na utaratibu uliowekwa hospitalini hapo, maiti inapaswa kukaa mochwari kwa muda wa hadi siku 21 pekee.

“Zikiisha siku hizo ikiwa ndugu hawatajitokeza uongozi uandika barua maalum ambapo huwapa kibali hamashauri ya jiji kuuchukua mwili huo na kwenda kuuzika,” anabainisha.

Anaongeza “Nimeshuhudia maiti nyingi tu zikizikwa na halmashauri kwa sababu ndugu zao hawakujitokeza, siwezi kukumbuka idadi kamili kwa sasa nadhani ni zaidi ya 80.

IDADI KWA SIKU

Anasema idadi hutofautiana siku na siku kwamba kuna wakati hupokea maiti sita had inane na au asipokee kabisa hata moja.

“Lakini muda wa kuisafisha maiti na au kuifanyia uchunguzi hutegemeana na sababu ya kifo chake, kwa mfano kama mtu amefia majini unakuta mwingine ameanza kuoza pale huwa ni kesi ngumu kidogo.

KUHUSU MAJI YA MAITI

JAMVI LA HABARI liliuliza ukweli juu ya madai kwamba maji ya maiti huweza kumsaidia binadamu kupata mafanikio kama wengi wanavyosema.

“Nimeyasikia hayo madai, ni mambo yanayosikitisha na kushangaza mno, hakuna ukweli juu ya hilo, ni imani potofu kabisa, binafsi siamini katika hilo,” anasema.

Anaongeza “Sisi hapa Muhimbili haturuhisiwi kabisa kuuza maji ya maiti, ni kosa tena kubwa mno kimaadili, marehemu anastahili heshima  pia.

MAFANIKIO LUKUKI

Anasema anajisikia fahari kufanya kazi hiyo kwani ameweza kuwasomesha watoto wake hao na kujenga nyumba huko Tandale ambako ndiko anakoishi.

“Nimeweza kujuana na watu wengi, leo hii naweza kufanya kazi popote pale, watu wananiamini, kumbuka nimekuambia sijasomea fani hii.

"Sina hata cheti lakini kuna vijana wanasoma fani hii huko chuoni, wanakuja mafunzo kazini hapa Muhimbili, ninawapokea na kuwafundisha kazi.

“Hili kwa hakika najivunia kwamba wananisikiliza na wanavuna maarifa kutoka kwangu pia, wakienda chuoni wanafaulu vizuri na kutunukiwa,” anasema.

Anaongeza “Nawasihi vijana wasiogope kufanya kazi hii, si kazi mbaya, binafsi najisikia fahari kumsaidia kumsitiri binadamu mwenzangu ambaye ametangulia mbele za haki.

".., na naamini siku nikiondoka duniani na mimi nitasitiriwa vizuri na watakaokuwa wamebaki.

“Sijachoka kufanya kazi hii, bado natamani kuifanya ingawa mkataba wangu unaonesha utaisha mwaka 2021, ikiwa wataniongezea nipo tayari kuendelea kuifanya.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement