Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete
(JKCI) Prof. Mohamed Janabi akimkabidhi zawadi ya ngao yenye ramani ya Tanzania
daktari bingwa wa magojwa ya moyo kwa watoto kutoka nchini China Zhao Lijian ikiwa ni
ishara ya kumshukuru baada ya kumaliza muda wake wa kufanya kazi kwa zaidi ya miaka miwili katika Taasisi hiyo.
Katikati ni kiongozi wa madaktari hao
ambaye pia ni Daktari bingwa wa usingizi Qin Chengwei anayefanya kazi katika
Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH).
Madaktari Bingwa watatu wa magonjwa ya moyo ambao ni raia wa
China wameagwa na uongozi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) baada ya
kumaliza muda wao wa kufanya kazi nchini.
Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China kila baada ya miaka
miwili huwa inatoa wataalamu wake kwenda nchi mbalimbali Barani Afrika kutoa
huduma za matibabu.
Hivyo, madaktari hao akiwamo daktari bingwa wa wagonjwa walioko katika chumba cha uangalizi
maalum (ICU), daktari bingwa wa magojwa ya moyo kwa watoto na daktari bingwa wa upasuaji wa moyo walikuwapo
nchini baada ya kusainiana makubaliano hayo katika ya Serikali yao na Tanzania kupitia
Wizaya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto.
Akizungumza wakati wa hafla ya kuwaaga madaktari hao mapema
hii leo, Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI, Profesa Mohamed Janabi, amesema
walikuwapo nchini kwa kipindi cha miaka miwili tangu tarehe 22 Juni, 2018 hadi kufikia
mwaka huu.
“Madaktari hawa wamemaliza muda wao wa kufanya kazi nchini
na wanatarajia kurudi nchini kwao katikati ya mwezi Oktoba, mwaka huu.
“Tumejifunza mengi kutoka kwao, tumeshirikiana nao kwa
ukaribu, niliwaona ni sehemu ya timu yetu ya wataalamu mabingwa wa JKCI,”
amesema.
Ameongeza “Wanarudi nchini kwao, tutaendelea kuwakumbuka
kwa kazi nzuri waliyofanya hakika walishirikiana nasi kwa ukaribu mno, wameshakamilisha
taratibu za kusafiri kurudi China.
“Wanapoondoka tunatarajia timu nyingine ya wataalamu kutoka
China ambao wameshakamilisha taratibu za kuja nchini, tutaungana nao kuendelea
kuimarisha huduma zetu,” amebainisha.
Akizungumza kiongozi wa timu hiyo ya madaktari kutoka China
waliokuja nchini kushirikiana na JKCI ambaye pia ni Daktari Bingwa wa Usingizi anayefanya kazi Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Dk. Qin Chengwei, amesema kipindi hicho
ya mashirikiano kimekuwa chenye manufaa kwa pande zote mbili.
“Binafsi naona miaka miwili imeisha haraka mno, mmeshirikiana
vizuri mno na wataalamu wetu, tunashukuru, kwa zaidi ya miaka 50 sasa Serikali
yetu imekuwa ikituma madaktari nchi mbalimbali za Afrika.
“Tunaahidi kuendelea kushirikiana na kuipa kipaumbele Tanzania,
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete, kuendelea kuleta wataalamu wetu kufanya nao
kazi,” amesema.
Ameongeza “Tunaamini kwa jinsi mlivyofanya kazi na timu hii
inayomaliza muda wake, mtafanya hivyo pia kwa timu ya wataalamu tunayoitarajia
kuja nchini Tanzania wakati wowote kuanzia sasa.
Mmoja wa madaktari hao, Dk. Hu Bin ameshukuru uongozi wa
Taasisi hiyo na wafanyakazi wote kwa kufanya nao kazi vizuri katika kipindi
chote walichoishi nchini.
“Niliishi hapa kama nyumbani, mmekuwa nasi katika nyakati zote, kila hatua, hakika niliona JKCI ni hospitali yangu, ya maisha yangu,” amesema.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi akimkabidhi zawadi ya ngao yenye ramani ya Tanzania na cheti daktari bingwa wa upasuaji wa moyo kutoka nchini China Hu Bin ikiwa ni ishara ya kumshukuru baada ya kumaliza muda wake wa kufanya kazi kwa zaidi ya miaka miwili katika taasisi hiyo. Kulia ni kiongozi wa madaktari hao ambaye pia ni Daktari bingwa wa usingizi Qin Chengwei anayefanya kazi katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH).
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi akimkabidhi zawadi ya picha yenye mchoro wa tingatinga daktari bingwa wa wagonjwa walioko katika chumba cha uangalizi maalum (ICU) kutoka nchini China Cui Jian ikiwa ni ishara ya kumshukuru baada ya kumaliza muda wake wa kufanya kazi katika Taasisi hiyo. Mwezi wa sita mwaka 2018 Serikali ya China ilitoa madaktari bingwa 11 kuja kufanya kazi hapa nchini wakiwemo madaktari bingwa watatu wa magonjwa ya moyo.
Kiongozi wa madaktari kutoka nchini China ambao wanafanya kazi hapa nchini ambaye pia ni Daktari bingwa wa usingizi Qin Chengwei katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) akiishukuru menejimenti ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa jinsi walivyoshirikiana na Madaktari bingwa wa magonjwa ya moyo watatu ambao wamefanya kazi katika Taasisi hiyo kwa zaidi ya miaka miwili.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi pamoja na wafanyakazi wa taasisi hiyo wakiwa katika picha ya pamoja na madaktari bingwa wa moyo kutoka nchini China mara baada kumaliza kuwaaga kutokana na muda wao wa kufanya kazi kwa zaidi ya miaka miwili katika Taasisi hiyo kumaliza. Mwezi wa sita mwaka 2018 Serikali ya China ilitoa madaktari bingwa kuja kufanya kazi hapa nchini wakiwemo madaktari bingwa watatu wa magonjwa ya moyo.
Madaktari Bingwa wa magojwa ya moyo kutoka nchini China wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kuagwa na Menejimenti ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) ambako walikuwa wanafanya kazi kwa zaidi ya miaka miwili. Mwezi wa sita mwaka 2018 Serikali ya China ilitoa madaktari bingwa 11 kuja kufanya kazi hapa nchini wakiwemo madaktari watatu wa magonjwa ya moyo.
Picha na JKCI.
Chapisha Maoni