Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement


Na Veronica Mrema – Dar es Salaam

Alipofikisha umri wa miaka 40, Nyakolema Silla Bhoke aligundulika ana ugonjwa wa saratani ya matiti, ilikuwa ni miaka minne tangu alipofunga ndoa na mwenza wake (hakupenda jina lake liandike).

Nyakolema anasimulia kwamba aliolewa akiwa na umri wa miaka 36, katika kipindi chote cha mapenzi yao ‘motomoto’ hawakubahatika kupata mtoto na mumewe.

“Ndoa yetu ilijawa furaha na mahaba tele, tulipendana mno na mume wangu, kipindi chote hatukukata tamaa ya ‘kutafuta’ mtoto,” anasema.

Anaongeza “Lakini nilipogundulika nina saratani ya matiti na daktari kushauri ziwa langu likatwe ili kutibu, hapo ndipo penzi letu ‘liliota mbawa’.

ALIVYOHISI TOFAUTI

Nyakolema anasema mkasa aliokutana nao katika maisha yake ni mtihani mzito anaokabiliana nao lakini hajakata tamaa akiamini ipo siku Mwenyezi Mungu atamfuta machozi.

“Kabla sijagundulika hospitalini, mimi mwenyewe siku moja nilihisi tofauti katika mwili wangu, nilipojikagua maziwa yangu, nilistaajabu nilipoona chuchu ya ziwa langu la kushoto imeingia ndani tofauti na chuchu ya ziwa langu la kulia.

“Nilianza kulifuatilia kila siku, mimi ni mkazi wa Dar es Salaam, lakini kipindi kile nilikuwa safarini Kanda ya Ziwa, Mkoani Mara, ziwa langu lilizidi kuvimba na  kunistaajabisha,” anasimulia.

Anaongeza “Nilianza kuperuzi mitandaoni, nilisoma maandiko mengi, katika andiko moja niliona wakieleza kwamba chuchu kuingia ndani ni miongoni mwa dalili za awali za saratani ya matiti.

Anasema aliporudi Dar es Salaam aliamua kwenda Taasisi ya Saratani Ocean Road, kwa sababu alikuwa anafahamu ndiyo taasisi ya Umma inayohusika na magonjwa ya saratani.

“Nilifanyiwa uchunguzi wa awali (kulipapasa ziwa) wakabaini kweli kulikuwa na uvimbe, wakanichukua sampuli ya majimaji ili wahakikishe kwa vipimo vya maabara iwapo uvimbe ule ulikuwa wa kawaida au saratani.

“Vipimo vilipotoka, majibu yalionesha nina saratani ya matiti, daktari alishauri nirudi baada ya siku kadhaa ili wachunguze tena kujiridhisha, ikionekana tena ni saratani basi matibabu yake ni kukatwa ziwa,” anasema.

Nyakolema anasimulia “Dah!... baada ya kuelezwa hayo, kwangu ikawa changamoto, nikatwe ziwa?... nikajiuliza itakuwaje?... maana ukiangalia ni kitambulisho cha mwanamke, halafu kiondolewe!... ilikuwa mtihani mzito kwangu.

ALIHANGAIKA

“Basi kabla sijarudi tena Ocean Road, niliamua kwenda hospitali nyingine ili nako wanichunguze, nilikwenda Aghakan majibu yalipotoka bado yalionesha nina saratani ya matiti,” anasema.

Anaongeza “Daktari alinieleza vile vile kwamba matibabu ni kukatwa ziwa.

“Ilibidi nilimuuliza. Hamuwezi kuondoa hako ka-uvimbe maana wakati ule kalikuwa bado kadogo? Daktari alinieleza kulingana na sehemu ka-uvimbe kalipokaa ilikuwa lazima waondoe ziwa lote.

“Maana waki-kiondoa tu chenyewe (ka-uvimbe), titi lisingekuwa na ‘shepu’ (muonekano),” anasema.

Anasema ingawa alielezwa hayo bado aliamua kwenda tena hospitali nyingine kufanyiwa uchunguzi akiamini huko pengine angepata majibu tofauti.

“Nilikwenda hospitali moja huko Temeke, majibu yalikuwa yale yale kama niliyoelezwa kule kwengine, nilifika hadi Hospitali ya Taifa Muhimbili, majibu bado yalikuwa yale yale,” anasema.

Anaongeza “Niliamua kurudi Ocean Road, kwa sababu niliona kadri ninavyohangaika kuzunguka huku na kule, ndivyo nilivyokuwa najiweka kwenye hatari ya kusambaa kwa saratani kwenye mwili wangu.

UPASUAJI KULIONDOA

Nyakolema anasema daktari alimchunguza tena na kujihakikishia ni saratani, alimuandikia rufaa kwenda Muhimbili (Mloganzila) kwa ajili ya upasuaji wa kuliondoa titi lake.

“Nililazwa Mloganzila, nilichukuliwa vipimo kwa ajili ya maandalizi ya upasuaji, yalipokamilika, nilifanyiwa upasuaji, walilikata, hali yangu ya afya ilipoimarika, niliruhusiwa,” anasimulia.

Nyakolema Silla Bhoke ambaye sasa anatumia titi la bandia akizungumza katika mahojiano maalum na mwandishi wa makala haya hivi karibuni.

HOFU YA KIFO

Anaongeza “Waliponiruhusu walinieleza upasuaji wa kuliondoa ni sehemu ya mwanzo ya matibabu, hivyo lazima nirudi Ocean Road kwa matibabu zaidi ya mionzi, nilipata hofu kubwa maana nilishawahi kusikia simulizi kwamba inaua.

“Watu walidai wanaotibiwa huko wanakufa, wakati huo sikuwa najua kwamba kuna tiba nyingine ya kemia (chemotherapy), daktari alinisaidia kunielewesha, hofu ikanitoka.

HOMONI ZILICHANGIA

Nyakolema anasema kwenye ukoo na familia yao yeye ndiye wa kwanza kugundulika kuugua ugonjwa huo hospitalini, hali iliyomshangaza.

“Hivyo, niliwauliza wataalamu kitu gani kilichangia mimi kupata saratani hii, niliulizwa kama niliwahi kupata ujauzito na kunyonyesha... nilijibu hapana... basi nilielezwa kwamba  homoni zangu za mwili kwa sababu nilichelewa kuzaa na kunyonyesha, nilichelewa kuolewa,” anasimulia.

Anaongeza “Kwa mujibu wa wataalamu homoni zimechangia, kwa sababu ... wanasema mwanamke akinyonyesha inavyotakiwa kuna kemikali inaachiliwa mwilini mwake na kumkinga dhidi ya saratani ya matiti na mtoto lazima anyonyeshwe miaka miwili.

“Daktari alinieleza pia kubadilika badilika kwa mzunguko wa hedhi si suala la kupuuzia, sasa mimi nilikuwa nakaa hata miezi miwili, sijaona siku zangu niliona ni jambo la kawaida, kumbe la hasha! Nilipaswa kwenda hospitalini kufanyiwa uchunguzi na tiba.

MUME ‘AMKIMBIA’

Nyakolema anasema alisubiri hadi kidonda kilipofunga vizuri, alianza ‘safari’ ya tiba kemi pamoja na ile ya mionzi, katika hatua zote za awali mume alikuwa bega kwa bega pamoja naye alimtia moyo asikate tamaa atapona maradhi hayo.

“Kwa kweli, nilipogundulika nina saratani, yeye alikuwa mbali, safarini kikazi, hivyo kipindi chote tulikuwa tunawasiliana kwa njia ya simu, taratibu mawasiliano yetu yalianza kupungua.

“Hakuwa ananitafuta kama alivyokuwa anafanya awali, alianza kunikwepa taratibu, mwisho ‘akaenda na upepo wa kisulisuli’, akaniacha, mpaka sasa nipo mwenyewe, sijui aliko.

“Nikitafaki huwa najisemea mwenyewe labda aliona simfai tena kwa sababu sijamzalia hata mtoto mmoja na sasa sina ziwa moja tena,” anasimulia kwa huzuni.

Anaongeza “Lakini sijakata tamaa bado napambana na matibabu, sijawahi kutetereka, afya yangu inaimarika, ukweli kuna changamoto kwenye hizi dawa mtu anapoanza matibabu.

“Lakini mimi hazijawahi kunisumbua, wapo wanaopata kichechefu, wanatapika, wanashindwa kula na hata kutotamani kuhisi harufu yoyote, kwangu haijawahi kunitokea hali hizo.

“Kila ninapokwenda kliniki wataalamu wananipima kinga zangu za mwili na wingi wa damu, nilipatiwa mizunguko minne ya tiba mionzi, ingawa awali niliandikiwa mizunguko sita, walinipunguzia kwani hali yangu inaimarika, sasa nimemaliza, namshukuru Mwenyezi Mungu,” anasema.

Anaongeza “Kwa sasa naendelea kupata dawa kidonge kimoja kila siku kwa muda wa miaka miwili ambazo ni kama kinga, ili kuzuia saratani isirudi kwa sababu hizi ni seli za mwili ambazo huwa zinajiongeza bila utaratibu.

“Sasa mimi ni shujaa, nimepona saratani naendelea kufuatiliwa hali yangu ili kuzuia isirudi, watanifuatilia kwa miaka mitano, naendelea na maisha yangu kama kawaida, 'nakula bata' (raha).

Anasema bado ana matumaini makubwa kwamba atakapomaliza matibabu  ataweza ‘kushika’ ujauzito kama wanawake wengine, kuzaa na kunyonyesha.

DAKTARI ANENA

Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Saratani wa Kitengo cha Uchunguzi wa ORCI, Maguha Stephano anasema ingawa jinsi zote wana matiti lakini kwa asilimia 99 huathiri wanawake na wanaume asilimia moja.

“Kuna visababishi mbalimbali vinaweza kuchangia, naweza kuviweka katika makundi mawili, vinavyozuilika na visivyozuilika,” anasema.

Anaongeza “Visivyozuilika ni vile tunavyozaliwa navyo, ukiwa jinsi ya kike upo kwenye hatari zaidi kuliko jinsi ya kiume. Kurithi pia ni kisababishi kingine ambacho hakizuiliki, kama ndugu wa karibu (wa damu) kwa mfano shangazi, bibi, mama aliwahi kuugua nawe upo hatarini.

Dk. Maguha anasema inashauriwa mwanamke anyonyeshe angalau miaka miwili lakini ikiwa hatanyonyesha kabisa au akanyonyesha kwa kipindi kifupi anajiweka kwenye hatari ya kupata saratani hiyo.

“Mwili wa mwanamke una homoni iitwayo oestrogen, anaponyonyesha kiwango cha homoni hii hushuka na hivyo kumkinga dhidi ya saratani ya matiti, kuliko yule asiyenyonyesha,” anafafanua.

Anaongeza “Mwanamke anaponyonyesha kuna faida nyingine pia kwa mtoto kupata virutubisho muhimu kwa ukuaji wa afya ya mwili na akili na ‘kujenga’ ukaribu na mama yake.

VISABABISHI VINGINE

Dk. Maguha anasema licha ya kichocheo hicho cha oestrogen vipo pia visababishi vingine vinavyoweza kuchangia mwanamke kupata saratani hiyo.

“Suala la mtindo mbovu wa maisha, unene uliopitiliza, uzito mkubwa, kutokufanya mazoezi mara kwa mara, kujifungua katika umri mkubwa.

“Siku hizi wapo wanaopata hedhi mapema na wengine wanachelewa kukoma, maana yake ni kwamba kiwango kile cha homoni ya eoestrogen huwa kingi kwa wakati mwingi na hivyo kuwa kwenye hatari ya kupata saratani hii,” anabainisha.

Anaongeza “Ndiyo maana tunashauri kufanya uchunguzi wa mara kwa mara ili kama mtu ana saratani hii aweze kugundulika na kutibiwa mapema, kwani ikigundulika mapema katika hatua ya kwanza na ya pili ni rahisi kutibika na kupona kuliko akichelewa hadi hatua ya tatu na nne ya ugonjwa.

MAKADIRIO YA WHO

Mkurugenzi wa Huduma za Kinga wa ORCI, Dk. Crispin Kahesa anasema kwa mujibu wa takwimu za Taasisi ya Globalcan za 2018, inakadiriwa kila mwaka kuna zaidi ya wagonjwa 42,060 wa saratani nchini Tanzania, asilimia 7.2 kati ya hao ni wa saratani ya matiti.

“Takwimu zetu nchini zinaonesha mwaka 2018 wagonjwa wa saratani walioweza kuhudhuria hospitalini ni zaidi ya 12,215 kati ya hao 42,060 wanaokadiriwa, kati ya hao 12,215 walioweza kuhudhuria wanawake waliogundulika kuugua saratani ya matiti walichukua asilimia 16 ya wagonjwa wote.

Dk. Kahesa anasema takwimu za ORCI zinaonesha saratani ya matiti ni tatizo kubwa ikishika nafasi ya tatu kwa kuwa na idadi kubwa ya wagonjwa, baada ya saratani ya kizazi na saratani ya tezidume.

“Wastani wa umri wa wanawake wanaogundulika kuugua hii ORCI nao umeshuka, takwimu zetu zinaonesha mwaka 2008/09 wanawake waliokutwa wakiugua walianzia miaka 64 lakini mwaka 2019 walianzia miaka 56 na wapo hadi wenye umri wa miaka 25 wamegundulika," anabainisha.

HUDUMA YA UPANDIKIZAJI

Mkurugenzi Mtendaji wa ORCI, Dk. Julius Mwaiselage anasema “Saratani ya matiti ni saratani inayoongezeka kwa kasi nchini. 

"Miaka 10 iliyopita ilikuwa inashika nafasi ya nne kwa kuwa na idadi kubwa ya wagonjwa hapa ORCI sasa hivi inashika nafasi ya pili.

“Changamoto tunayoiona hivi sasa kwenye jamii ni wimbi la taarifa potofu zilizopo kwenye mitandao ya kijamii, baadhi ya wagonjwa hushawishiwa kwenda kupata dawa za kienyeji ambazo hata hazijafanyiwa utafiti na hivyo huacha tiba za hospitalini.

“Hatujafanya utafiti kamili ila tunakadiria asilimia 10 ya wagonjwa wa saratani zote tunaowatibu hukacha matibabu, huondoka wodini na kwenda kwa waganga wa kienyeji au kwenye maombezi.

“Wengine hupoteza maisha huko na wale wachache wanaorudi ugonjwa huwa upo hatua za juu, tiba huwa ngumu, wanapoteza maisha,” anabainisha.

Anaongeza “Tunasisitiza wazingatie matibabu, hata wakienda huko, wasiache matibabu, Serikali inazidi kuboresha huduma, sasa tunao uwezo wa kuigundua mapema na kuitibu pasipo kuondoa titi lote, ikiwa mtu atagundulika mapema.

“Kila mwaka tunatibu kwa njia hii ya upasuaji pasipo kuondoa titi lote, wanawake 100 ikiwa ni sawa na asilimia 30 ya wagonjwa wote tunaowatibu, tunayo, kwa wale waliofanyiwa upasuaji na kuondolewa katika titi lote jitihada zinafanyika.

"Hivi sasa wataalamu wetu wapo China wakijifunza jinsi ya kufanya upasuaji wa kupandikiza matiti, walikuwa wawe wameshamaliza masomo yao na kurejea nchini tayari kuanzisha huduma hii,” anasisitiza.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement