Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement


Na Veronica Mrema - Dar es Salaam

Teknolojia ya kisasa ya matibabu dhidi ya saratani pasipo mgonjwa husika kulazwa wodini, kutundikiwa dripu (tiba kemia/ chemotherapy), imeanza kutumika katika Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI).

Hatua hiyo inalenga kuboresha utoaji huduma ya matibabu kwa wagonjwa hao ili wasilazimike kulala wodini wakipata matibabu hayo, kupitia teknolojia hiyo wataalamu hufanya upasuaji mdogo na kuweka njia (tube) maalum kwa ajili ya kuweka dawa chini ya ngozi.

Mkurugenzi wa Huduma za Kinga za Saratani Ocean Road, Dk. Crispin Kahesa amesema hayo alipozungumza na MATUKIO NA MAISHA BLOG katika mahojiano maalum.

Dk. Kahesa amesema kupitia teknolojia hiyo kwa kuwa mgonjwa halazwi wodini ana uwezo wa kuendelea na matibabu huku akitekeleza majukumu yake ya kila siku.

“Serikali imeboresha huduma za upatikanaji wa dawa za saratani ndani ya taasisi kwa sasa upatikanaji wa dawa ni wa kiwango cha asilimia 94,” amesisitiza.

Ameongeza “Katika kuendelea kuboresha huduma zetu, tumepata mfumo mpya mwingine wa utoaji dawa kwa wagonjwa tunaowahudumia, zamani tulikuwa tunatoa dawa kwa njia ya dripu lakini sasa tuna maboresho.

“Tunao mfumo mwingine ambapo dawa ile ile badala ya mgonjwa kuwekewa kwa njia ya dripu, tuna njia nyepesi ya kumuwekea chini ya ngozi hii ni teknolojia ya kisasa, madhara ni madogo na inampa mgonjwa nafasi ya kuendelea na shughuli zake za kila siku,” amesema.

Amefafanua “Kwa njia ya dripu ililazimu mgonjwa aje hospitalini, akae wodini tumuwekee lakini kwa njia hii ya teknolojia ya kisasa, atafanyiwa upasuaji mdogo kuweka ‘tube’ itakayokuwa inatumika kupitishia dawa kwenda chini ya ngozi na kurudi zake nyumbani.

“Hatalazimika kukaa hospitalini, dawa itakuwa inatoka taratibu kwenye ‘ki-pakti’ chake na kupita kwenye mishipa midogo ya damu kwenda mwilini mwa mgonjwa kupambana na saratani.

“Kwa njia ya dripu tulikuwa tunalazimika kutafuta mshipa mkubwa wa damu ndipo tumuwekee mgonjwa dawa ndiyo maana ilikuwa lazima mgonjwa akae mule mule wodini,” amesema Dk. Kahesa ambaye pia ni Bingwa wa Magonjwa ya Saratani katika Taasisi hiyo.

Amesema teknolojia ya kisasa wanayotumia ni rafiki kwa mteja na inayobebeka kirahisi (portable).

“Changamoto iliyosalia ni kwa upande wa huduma ya upasuaji, wagonjwa wetu wanaohitaji upasuaji sasa hivi wanalazimika kwenda kwenye hospitali nyingine ambazo tunashirikiana nazo zikiwamo za kanda na za mikoa ambako kuna mabingwa wa upasuaji.

“Wakishafanyiwa wanarudi ili tuendelee kuwahudumia kwa tiba nyingine tulizonazo hapa, tunatafuta mwarobaini wa kuondoa adha hii bado kwa huduma za upasuaji tunataka wagonjwa wapate bila kupata adha tupunguze muda wa mgonjwa kuzungunka.

Mkurugenzi Mtendaji wa ORCI, Dk. Julius Mwaiselage amesema wanatoa tiba hiyo ya teknolojia ya kisasa kwa kushirikiana na Kampuni ya Roche Pharmaceuticals.

“Tunazidi kuboresha huduma zetu, lengo letu ni kuhakikisha kwamba Taasisi hii inakuwa bora katika utoaji huduma za uchunguzi na matibabu dhidi ya saratani si tu Tanzania bali pia katika Bara la Afrika,” amesisitiza.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement