Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement


Na Veronica Mrema - Dar es Salaam

Kabla ya kukua kwa sayansi na teknolojia chupa moja ya damu (unit moja) ilipochukuliwa kutoka kwa mchangiaji mmoja iliweza kutumika kumsaidia mgonjwa mmoja tu, aliyehitaji kuongezewa damu.

Maendeleo ya sayansi na teknolojia sasa yanawezesha wataalamu wa afya kutumia chupa moja ile ile ya damu kutoka kwa mchangiaji mmoja kuweza kuokoa maisha ya watu watatu wenye uhitaji wa kuongezewa damu.

Wataalamu hao wanao uwezo wa kuvuna mazao yanayopatikana kwenye damu na kuyahifadhi vema kitaalamu kwa ajili ya matumizi pale yanapohitajika.

Kwa mujibu wa wataalamu chupa moja ya damu ina ujazo wa mililita 450 sawa na chupa moja ya soda na kidogo, huenda msomaji wetu wa MATUKIO NA MAISHA BLOG  unajiuliza mazao ya damu ni yapi?.

“Damu ina mazao makuu matatu ambayo ni chembechembe nyekundu (packed Red Blood), chembe sahani (Platelets) na Plasma (Fresh Frozen Plasma),” anabainisha Mkurugenzi Mtendaji wa Mpango wa Taifa wa Damu Salama Tanzania (NBTS), Dk. Magdalena Liymo katika mahojiano maalum na BLOG HII.

Dk. Magdalena anaongeza “Chembe nyekundu husaidia kubeba oksijeni mwilini, chembe sahani husaidia damu kuganda, watumiaji wakubwa wa chembe sahani ni wagonjwa wa saratani.

“Plasma ni kimiminika ambacho kinatengenezwa kutoka kwenye damu na kina ‘protein’ ambazo husaidia kugandisha damu isiendelee kutoka hasa kwa mama wajawazito, wanaotokwa damu wakati wa uzazi.

Dk. Magdalena anasema Tanzania hivi sasa inajikita zaidi katika matibabu ya kibingwa na yale ya ubingwa wa juu, hivyo NBTS nayo inazidi kuongeza kasi ya ukusanyaji wa damu (salama) na uzalishaji wa mazao ya damu.

“Imezoeleka kwamba NBTS huwa tunakusanya damu, ni jukumu letu la msingi lakini kwenye kuboresha huduma za afya hatuwezi kuitumia damu yote kama ilivyokusanywa (chupa moja nzima kwa mtu mmoja).

“Hivi sasa kuna huduma za kibingwa na za ubingwa wa juu ambazo zinaendelea kufanyika kwenye hospitali zetu kubwa ikiwamo Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Taasisi ya Tiba ya Mifupa Muhimbili (MOI), Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na katika hospitali za rufaa za kanda.

“Kwa mfano upandikizaji figo, mishipa ya damu na hivi karibuni nchi yetu inatarajia kuanza upandikizaji wa uloto Muhimbili, haya ni matibabu ya ubingwa wa juu, maana yake ni kwamba, nchi yetu tunaongeza matumizi ya mazao ya damu.

“Ili kuboresha huduma za afya hatuwezi kutumia ‘all blood’, NBTS tunataka kuboresha zaidi eneo hili la uzalishaji mazao ya damu ili… kwa mfano ikiwa kuna mtu anahitaji  chembe sahani awekewe, akiwepo anayehitaji plazima awekewe, kila Mgonjwa anatakiwa apate 'right product',” anabainisha.

Chupa moja (unit moja) ya damu kutoka kwa mtu mmoja ina uwezo wa kutoa aina tatu za mazao ya damu na hivyo kuweza kuokoa uhai wa wagonjwa watatu wenye uhitaji.

MASHINE ZA KISASA

Anaongeza “Ndani ya kipindi cha uongozi wa Serikali ya awamu ya tano chini ya Rais John Magufuli, tumepata mafanikio  makubwa ikiwamo kupata mashine za kisasa zenye uwezo wa kuchunguza sampuli nyingi za damu ndani ya saa chache, tofauti na hapo awali.

“Tumepata mashine mpya 24 ambazo zimesambazwa katika kila kituo kwenye kanda sita tulizonazo, kila kanda zimesimikwa mashine nne, mashine hizi nne gharama yake ni Sh. bil 13.2,” anabainisha.

Dk. Magdalena anasema mashine hizo nne zilizosimikwa kwenye kila kanda, mashine mbili ni maalum kwa ajili ya kuchunguza maambukizi katika damu na mbili nyingine ni kwa ajili ya kutambua kundi la damu.

Anaongeza “Mashine za kupima makundi ya damu zina uwezo wa kupima sampuli 156 ndani ya masaa mawili.

Anasema kwa upande wa mashine zinazopima maambuki, kila chupa inayokusanywa hupimwa maambukizi ya magonjwa manne ukiwamo ugonjwa wa Ukimwi, Virusi vya Homa ya ini B na C pamoja na kaswende.

“Hivyo, katika kila chupa ya damu inayokusanywa huwa tunapima maambukizi hayo manne, mashine zina uwezo wa kupima sampuli 100 kila moja ndani ya masaa mawili, maana yake ni kwamba mashine hizi zinatupa majibu 400 ndani ya masaa mawili,” anabainisha.

Anaongeza “Tunazo pia mashine nyingine mbili ambazo zimefungwa Mkoa wa Dar es Salaam na Mwanza zenye uwezo wa kutoa majibu, 600 ndani ya saa moja.

“Kwa kusimika mashine hizi, mafanikio ni kwamba zinahitaji rasilimali watu wachache zaidi, inatusaidia kukabili ule upungufu wa watumishu, kwa sababu  hatuwezi kuwa na watumishi wa kutosha asilimia 100.

“Kwa mashine hizi mtaalamu anaweza kukaa mtaalamu mmoja, akaweka sampuli mashine ikaendelea kufanya kazi na tukapata majibu ya sampuli 600 kwa wakati mmoja,” anasema.

Anaongeza “Tukilinganisha na awali kabla ya kupata mashine hizi tulitumia zile za 'semi-automated' ambazo sampuli 88 zilichukua saa tatu hadi nne kupata jibu moja (maambukizi ya ugonjwa mmoja.

“Ililazimu wakae watalaamu wanne 'full time' kufuatilia kila sampuli moja, kila ugonjwa mmoja,” anabainisha.

“Sasa hivi tunao uwezo wa kupima kwa ‘speed’ (kasi) mara sita zaidi ya ile ya zamani, kazi zinaweza kufanyika ‘hand off’ yaani zile mashine zinaweza kufanya kazi zenyewe baada ya mtaalamu kuweka sampuli na ‘ku-set’ mashine.

“Majibu ya sampuli nayo yanakuwa ya uhakika zaidi, tunaishukuru mno Serikali kwa kuboresha eneo la maabara na upimaji, uhakika na ubora wa huduma zetu umeimarika kwa wateja wetu wote (mchangiaji na anayechangiwa),” anasema Dk. Magdalena.

NYOTA NJEMA

Anasema Mpango huo hivi sasa umefanikiwa kuongeza kiwango cha ukusanyaji damu nchini kimeongezeka kwa asilimia 20 kutoka asilimia 40 ilivyokuwa mwaka 2015 hadi asilimia 60 mwaka 2019

“Haya ni matokeo ya kufanya kazi kwa ushirikiano, hamasa ya jamii imekuwa kubwa, kila mtu sasa anaelewa umuhimu wa damu, tumepiga hatua kubwa ingawa bado hatujafikia asilimia 100,” anasema.

Anasema kulingana na takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO) ili nchi itosheleze mahitaji ya damu inahitaji kukusanya asilimia moja ya wananchi wake.

“Tanzania, tunakadiriwa kuwa tupo watu milioni 50, maana yake tunatakiwa kukusanya chupa 50,000 za damu kila mwaka, mwaka 2016/17 tulifanikiwa kukusanya chupa 196,735, mwaka 2017/18 chupa 257,557 na mwaka 2018/19 idadi iliongezeka hadi kufikia chupa 309,379,” anabainisha.

MTANDAO NCHINI

Anasema NBTS ina vituo saba vya Kanda ukanda wa Kaskazini (Kilimanjaro), Kanda ya Ziwa (Mwanza), Kanda ya Magharibi (Tabora), Kusini (Mtwara), Nyanda za Juu Kusini (Mbeya).

“Kanda ya Mashariki (Dar es Salaam, Morogoro Pwani) na Kanda ya Kati (Dodoma),” anasema Dk. Magdalena.

Anaongeza “Pia tunashirikiana kwa ukaribu na Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Kanda ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).

“JWTZ wenyewe hawana mipaka ya mikoa wanayohudumia, wanahudumia nchi nzima.

“Ili kuimarisha ufuatiliaji na usimamizi wa ukaribu kwenye kila mkoa na wilaya kuna mratibu wa damu salama lengo ni kuhakikisha kote huko kuna mtu ambaye anahakikisha damu ipo,” anasisitiza.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement