Mganga Mkuu wa Serikali (CMO), Prof. Abel Makubi akizungumza wakati wa uzinduzi wa mradi huo utakaohusisha taasisi zilizopo Tanzania Bara na Visiwani.
Na Veronica Mrema – Dar es Salaam
Mifumo ya udhibiti wa majaribio ya dawa, vifaa tiba na maadili
ya tafiti mbalimbali za afya zinazofanywa kwa binadamu, iliyopo nchini itazidi
kuimarishwa zaidi, hatua hiyo inakusudiwa kufikiwa kupitia mradi wa ASCEND.
Mradi huo pia unalenga kupunguza muda wa kutathmini maombi
ya kufanya tafiti za majaribio ya dawa nchini na hivyo kuwezesha upatikanaji wa
vibali vya utafiti ndani ya muda mfupi.
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba Tanzania
(TMDA), Adam Fimbo amesema hayo leo alipozungumza mbele ya Mganga Mkuu wa
Serikali, Prof. Abel Makubi wakati wa uzinduzi wa mradi huo ambapo Tanzania
imefanikiwa kupata fedha za utekelezaji baada ya kuandika andiko la ombi la
mradi.
“Taasisi zinazoshiriki katika mradi huu ni pamoja na TMDA
ambayo ina jukumu la kudhibiti kwa mujibu wa sheria, nyingine ni NIMR, Mamlaka
ya Chakula na (ZFDA), KCRI, MUHAS, ZAHRI na St. Andrew’s University ya
Uingereza,” ametaja Fimbo.
Amesema Tanzania imepata fedha za mradi, kupitia andiko la
pamoja na taasisi hizo na kwamba fedha hizo huwa zinatolewa kwa nchi ambazo
zimeendelea katika Bara la Europa na katika nchi zinazoendelea ambapo
hushirikiana kwa pamoja.
“Lengo la kusaidia kufanya tafiti mbalimbali ili kujenga
mifumo na ili iwe thabiti katika kufanya majaribio na tafiti mbalimbali, hivyo,
baada ya kuandika andiko la mradi tumefanikiwa kupata fedha kwa utekelezaji wa
kipindi cha miaka miwili na nusu kuanzia Novemba hii,” amebainisha.
Ameongeza “Kikubwa tutakachofanya ni kuweza kuboresha
mifumo yetu ya udhibiti wa majaribio ya dawa, mifumo ya utafiti namna ya kusoma
na kupitisha maombi mbalimbali ya udhibiti wa majaribio ya dawa kabla ya
kufanyika nchini.
“Vile vile, kuweka mifumo vizuri ya kufuatilia wale ambao
wanaweza kupata madhara wakati wanatumia dawa za majaribio, kimsingi dawa za
majaribio unakuwa hufahamu kama ni salama au si salama.
“Kwa hiyo unatakiwa kuweka mfumo ambao utahakikisha wale
ambao wanapewa dawa hizo wanabaki kuwa salama bila kupata madhara yoyote, mfumo
huo tunao, kupitia mradi huu utatusaidia kuuboresha zaidi ili hatimaye tuweze
kulinda wale wote wanaoshiriki tafiti mbalimbali,” amesema.
Amesema kupitia mradi huo, MUHAS utawezesha mafunzo kwa wataalamu
mbalimbali waliopo ndani ya mamlaka za udhibiti pamoja na wanaofanya utafiti
ili tuwe na uelewa mpana zaidi kwenye masuala hayo.
Fimbo amesema mradi huo unahusisha Tanzania Bara na
Visiwani, kwa sababu taasisi zinafanya kazi zinazofanana, ni nchi moja, aidha
ni sehemu ya takwa la mradi waliona wakae na kutengeneza mradi huo wa pamoja
ili waweze kusaidiana.
“Taasisi zetu zinahitaji kupata msaada zaidi kwa maana ya kuwa
na wataalamu wabobezi kwenye kufanya tafiti hizi pamoja na ufuatiliaji wa
majaribio ya dawa.
“Kwa mujibu wa Sheria ya Dawa na Vifaa Tiba nchini, kwa
mfano Tanzania, TMDA ina jukumu la kudhibiti majaribio ya dawa na tumekuwa
tunatoa vibali vya kuruhusu majaribio kuweza kufanyika,” amesema.
Fimbo ameongeza “NIMR pia ni sehemu ya kazi yao wanatoa
vibali kuruhusu binadamu kushiriki, kwenye majaribio ya dawa, kwa sababu kuna
masuala ya maadili ambayo lazima yafuatwe linapokuja suala la kufanya tafiti kwa
watu.
“Mgeni rasmi (CMO) yeye ndiye lazima aidhinishe vibali
hivyo kama sehemu ya utaratibu ambao umewekwa ili kuruhusu majaribio kufanyika nchini
kwa mujibu wa taratibu zilizowekwa hasa kulinda wale wanaoshiriki kwenye
majaribio haya.
“Hivyo, kuna miongonozo ambayo tutaipitia kuiweka sawa
ifanane Zanzibar na bara, na wale wote wanaoshiriki ili hatimaye tuweze
kutekeleza yale ambayo tumeyaomba wenyewe na kupata fedha hizi,” amesema.
Akizindua mradi huo, Mganga Mkuu wa Serikali, Prof. Makubi
amezipongeza taasisi hizo kuungana pamoja kuandika mradi huo na kufanikiwa
kupata fedha hizo.
“Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii,
Jinsia, Wazee na Watoto, imewapa TMDA majukumu mbalimbali likiwamo la kudhibiti
viwango vya tafiti mbalimbali hasa hizi zinazolenga kugundua ama dawa au vipimo
ambavyo vinaweza kutumika kwa binadamu.
“Ili utafiti ukamilike lazima upitie hatua mbalimbali kabla
binadamu wengi kutumia hizo dawa au vipimo, katika hiyo ‘process’ tunaanza na
watu wachache ambao huwa wanajitolea.
“Baadae dawa au kipimo kikionekana hakina madhara ndiyo
inaenda hatua za mwishoni kuruhusu kutumika hiyo dawa au vipimo.
“Tunashukuru TMDA na vyuo vyetu vya mafunzo na taasisi zetu
za tafiti Bara na Visiwani pamoja chini ya project hii, ambayo itaupa uwezo
TMDA ifanye jukumu lake la usimamizi na udhibiti vizuri, lakini pia na
kuziwezesha taasisi zetu kwa maana ya mafunzo za tafiti mbalimbali hasa hizi
clinical trials,” amesema.
Prof. Makubi ameongeza “TMDA iangalie pia namna
itakavyoweza kupunguza baadhi ya kero za wananchi ikiwamo kuchelewa kupata
kwenda kufanya mwezi hadi miwili, pengine itaweza kujenga mifumo kuondoa hizo
kero.
“Tunatoa wito kwa tmda na wenzake kuangalia suala la
gharama za usajili ili kupata ruhusa ya majaribuo ya dawa, hasa wanafunzi
wanaokuwa masomo elimu ya juu, hupata fedha lakini si nyingi hivyo unakuta
anahangaika sana na supervisor wake inachukua muda mrefu kumaliza masters yake
na phd.
“Angalieni hilo muone jinsi gani mnaweza kufacilitate bila kupunguza viwango na kubadilisha zile taratibu mkaweza kumsimami,a na kumpa aporoval na mentorship kwamba atakapokuja kuwa researcher kamili awe ameimarika,” ametoa rai.
Baadhi ya washiriki kutoka taasisi mbalimbali wakimsikiliza kwa makini Mganga Mkuu wa Serikali, Prof. Makubi (hayupo pichani) wakati wa uzinduzi huo.Mkurugenzi Mkuu wa TMDA, Adam Fimbo, akizungumza wakati wa uzinduzi huo mapema hii leo.
Chapisha Maoni