Waziri Jafo akiingia ukumbini kuzungumza na walimu wakuu wa shule za Sekondari Tanzania.
Na Veronica Mrema – Dodoma
Wakurugenzi wa Halmashauri nchini wameagizwa kuhakikisha
wanasimamia ipasavyo upimaji wa maeneo ya viwanja vya shule zote nchini na
yapatiwe hati miliki.
Agizo hilo limetolewa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais,
Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Suleiman Jafo ambaye amemtaka
Katibu Mkuu wa Wizara hiyo anayesimamia Idara ya Elimu, kusimamia.
Waziri Jafo ametoa agizo hilo leo alipozungumza wakati wa
ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa 15 wa Wakuu wa Shule za Sekondari Tanzania
(TAHOSSA) unaofanyika jijini hapa.
Amesisitiza kwamba atafuatilia kwa ukaribu utekelezaji wa
agizo hilo na Wakurugenzi watapimwa utendaji kazi wao kwa utekelezaji
watakaofanya.
“Yaani, shule halmashauri kwako, wataalamu wapo kwako,
wapimaji wapo kwako, lakini unakuta shule haina hati miliki, hili ni jambo la
aibu, mwaka 2021 ni wa upimaji wa maeneo yote ya taasisi za shule zetu zote
ndani ya Jamhuri ya Muungano.
“Ni agizo kwa wakurugenzi wote wa halmashauri,.. na eneo la
upimaji utendaji kazi wenu, ni jinsi gani mkurugenzi alisimamia maeneo ya
serikali yaweze kupimwa na kupata hati miliki,hili jambo tuseme limefika mwisho
na halina mzaha,” amesisitiza.
Awali, Waziri Jafo ametumia jukwaa hilo kueleza mafanikio
yaliyopatikana kwenye sekta ya elimu katika utendaji kazi wa Serikali ya Awamu
ya Tano inayoongozwa na Rais Dk. John Magufuli.
Amesema ndani ya kipindi hicho sekta ya elimu imepiga hatua
kubwa ikiwamo utoaji wa fedha za elimu bila malipo kutoka Sh. bilioni 20.8 hadi
kufikia Sh. bilioni 24.
“Tumeweza kukarabati jumla ya shule kongwe 86 za Serikali
hadi sasa, ufaulu wa wanafunzi kidato cha nne umeongezeka kutoka asilimia 67.91
mwaka 2015 hadi asilimia 79.41 mwaka 2019,” amebainisha.
Amewapongeza walimu kwa juhudi kubwa wanazofanya katika
usimamizi wa miradi ya Serikali na fedha za elimu bila malipo kwamba utendaji
kazi wao umekuwa chachu katika kufikia mafanikio kwenye sekta hiyo.
Amesema katika mwaka wa fedha wa 2020/21 Serikali imekusudia kuhakikisha shule zake zote zinajengewa maabara ili kuwezesha wanafunzi kufanya majaribio ya kisayansi na hilo linakwenda sambamba na kuongeza idadi ya walimu wa masomo ya sayansi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Global Education Link, Abdulmalik
Mollel (pichani) ambaye pia ni mratibu wa mkutano huo, amesema kimekuwa kikao chenye mafanikio.
“Tumeweza kuwakutanisha wakuu wote wa shule za sekondari
nchini ambao kwa pamoja wametoa maoni, wanashauri yatakayosaidia kuboresha
sekta ya elimu.
“Tuliona kuna malalamiko mbalimbali, wanafunzi wanaomaliza
kidato cha sita, wanapotaka kujiunga na elimu ya juu, au wa kidato cha nne
wanapotaka kujiunga na program za nacte huwa wanashindwa kuelewa baadhi ya
taratibu.
“Katika kikao hiki wapo Nacte, Bodi ya Mikopo na taasisi
nyingine za elimu ambapo wanawaelewesha walimu wakuu nao wakirudi kule
watakwenda kusaidia wanafunzi wao,” amesema.
Amesema Taasisi ya Elimu Tanzania nao ni miongoni mwa wadau waliohudhuria kikao hicho, vile vile wamepata huduma ya uchunguzi wa afya dhidi ya magonjwa mbalimbali.
Baadhi ya walimu wakuu wa shule za sekondari wakimsikiliza Waziri Jafo (hayupo pichani), mapema leo.Walimu wakuu wa sekondari wakipata huduma katika banda la Gel Medical Tourism.Walimu wakuu wa sekondari wakipata huduma katika banda la Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).Walimu wakuu wa sekondari wakipata huduma katika banda la bodi ya Mikono Tanzania.Walimu wakuu wa sekondari wakipata huduma katika banda la Gel Medical Tourism.
Chapisha Maoni