Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement


Na Veronica Mrema – Dar es Salaam

Janga la CORONA bado linaitesa dunia, ingawaje yapo matumaini ya kupatikana kwa chanjo, nchi mbalimbali zikiwa tayari zimeanza kutoa kwa raia wake na kueleza ni hatua ya mafanikio.

Hata hivyo, kubainika kwa aina mpya ya virusi katika mataifa kadhaa ikiwamo Marekani na Nigeria ni suala linaloibua hofu kwa binadamu, likiangaziwa kwa ukaribu zaidi hivi sasa.

Mwanzoni mwa Desemba, 2020, Kituo cha Kukinga na Kudhibiti Magonjwa cha Afrika (Africa CDC) kilinukuliwa kikieleza idadi ya jumla ya maambukizi yaliyothibitishwa ya virusi vya Corona barani humu imekaribia milioni 2.25, huku idadi ya vifo ikifikia 53,543 na wengine wapatao milioni 1.9 wameugua na kupona Afrika.

Kwa mujibu wa Africa CDC, nchi zilizoathiriwa vibaya zaidi na virusi hivyo barani humo ni Afrika Kusini, Morocco, Misri na Ethiopia, huku Kenya nayo ikishuhudia ongezeko la maambukizi miongoni mwa raia wake katika siku za hivi karibuni.

Eneo la kusini mwa Afrika linatajwa kuwa lenye kiwango cha juu zaidi cha maambukizi ya COVID-19 na vifo vinavyotokana na ugonjwa huo huku eneo la kaskazini mwa Afrika likiwa la pili.

Shirika la Afya Duniani (WHO) lenyewe limewatoa wasiwasi wanadamu hasa juu ya aina mpya ya virusi hivyo iliyoripotiwa kwenye mataifa kadhaa.

WHO linasisitiza pia chanjo hizo zilizotengenezwa kupambana na COVID - 19 zina uwezo wa kutoa kinga dhidi ya virusi hivyo, lakini uchunguzi zaidi unaendelea.

NI MWAKA MMOJA

Kufikia Desemba, 2020 dunia ilitimiza mwaka mmoja tangu Desemba, 2019, iliposhuhudia mlipuko wa ugonjwa huo huko Wuhan, China.

Awali haukujulikana ulikuwa ugonjwa gani na ulisababishwa na aina gani ya virusi hadi pale wataalamu walipofanya uchunguzi wa kina wa kimaabara.

Hatimaye ilibainika chanzo chake ni maambukizi ya virusi vya Corona vinavyosababisha ugonjwa wa homa kali ya mapafu, ukapewa jina COVID – 19.

Mithili ya moto uteketezao nyika, ulianza kuenea kwa kasi kwengineko duniani, wengi wakaambukizwa virusi hivyo na wengine kupoteza maisha hasa wazee na watu wanaokabiliwa na magonjwa yasiyoambukiza (sugu).

Takwimu za WHO zinaeleza tangu Desemba, 2019 hadi Januari 3, 2021 jumla ya wagonjwa milioni 83.32, vifo milioni 1.8 vimeripotiwa.

Hivi sasa nchi mbalimbali zimeendelea kuchukua hatua ikiwamo kuweka sharti la upimaji ya maambukizi hayo kwa wasafiri wanaotoka nchi moja kwenda nyingine, Tanzania ikiwamo.

TANZANIA

Machi 16, 2019 Tanzania iliripoti kisa cha kwanza cha mwanamke mmoja mwenye raia wa Tanzania, alithibitika kuambukizwa virusi hivyo na kuugua, aliwasili nchini akitokea Ubelgiji kwa ndege ya Shirika la Rwanda.

Kulingana na Ofisi ya Taifa ya Takwimu Tanzania (NBS) idadi ya visa iliongezeka kutoka kimoja hadi kufikia 480, April, 2020 huku vifo 18 vikiripotiwa kutokana na ugonjwa huo.

Serikali ya Tanzania ilichukua hatua mbalimbali kuukabili ili kuhakikisha inalinda wananchi wake dhidi ya janga hilo na mara kadhaa imenukuliwa ikisisitiza hivi sasa hakuna kisa chochote cha Corona.

Miongozo ya kitaalamu ilitolewa kwa umma kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto ikielekeza jinsi ya kuepuka maambukizi ya ugonjwa huo usio na tiba hadi sasa duniani.

Hatua hizo ni pamoja na kukaa umbali wa mita moja hadi mbili kati ya mtu na mtu hasa anayekohoa na mwenye historia ya kusafiri kutoka nje ya nchi, kunawa mikono kwa maji safi tiririka na sabuni, kuvaa barakoa na kutumia vitakasa mikono.

Mikusanyiko ya watu nayo ilizuiliwa kwa muda, kwa mfano shule na vyuo vyote nchini vilifungwa, kwa lengo la kuepusha uwezekano wa kusambaa zaidi kwa maambukizi hayo.

TAFITI ZA DUNIA

“Ni changamoto ya dunia nzima, mlipuko wa Corona uliibua hofu kwamba huenda inaenezwa kwa njia ya kuongezewa damu.

“Lakini tafiti mbalimbali zilipofanyika zilionesha haiambukizwi kwa njia ya kuongezewa damu,” anasema Meneja wa Mpango wa Taifa wa Damu Salama Tanzania (NBTS), Dk. Magdalena Liymo (pichani) katika mahojiano maalum na MATUKIO NA MAISHA BLOG hivi karibuni.

Dk. Liymo anaongeza “Hivyo wagonjwa waliopatiwa huduma ya kuongezewa damu maana yake ni kwamba hakukuwa na maambukizi ya Corona kwa njia hiyo.

“Kwa kuwa haienezwi kwa njia ya damu, lakini pia mikusanyiko ilizuiliwa, NBTS tulifanya maboresho ya mazingira ya uchangiaji damu kwenye vituo vyetu kwa kuzingatia maelekezo ya Wizara ya Afya, ili kuwalinda wananchi na watoa huduma wetu.

“Tulihamasisha jamii kujitolea damu kwa hiyari, tukaweka vitanda vyetu kwa kuzingatia umbali wa mita moja, vitakasa mikono, maji safi tiririka na sabuni, tukahimiza uvaaji wa barakoa na hatua zote muhimu ili kuepusha maambukizi ya ugonjwa huo.

“Jamii ilihamasika, watu walijitokeza kuchangia damu kwa hiyari, tulipata upungufu kiasi cha asilimia kati ya tano hadi 20 ya makusanyo ya damu kulinganisha na kipindi ambacho hakukuwa na ugonjwa,” anabainisha.

RIPOTI ZA NBTS

Kwa mujibu wa NBTS zaidi ya asilimia 80 ya wachangia damu ni wanafunzi na wana - vyuo. Kutokana na marufuku ya mikusanyiko ya watu ikiwa ni hatua ya kukabiliana na Corona, ililazimika kuchukua hatua mbadala kukusanya damu salama ili kuendelea kuhudumia jamii pale ilipohitajika.

Takwimu za NBTS zinaonesha katika kipindi hicho makusanyo ya damu salama yalishuka ambapo kipindi cha kuanzia April, 2019 yalikuwa chupa za damu 22,044 ikilinganishwa na chupa za damu 25,737 kipindi cha Machi, 2019 (ugonjwa ulipothibitishwa) na chupa za damu 31,502 kipindi cha Februari, 2019 kabla ya ugonjwa kuingia nchini.

Ripoti za NBTS zinaeleza kushuka huko kwa makusanyo kulichangiwa na kufungwa kwa shule na vyuo, kukosa fursa ya kukusanya damu katika ofisi mbalimbali pamoja na zuio la mikusanyiko ikiwa ni hatua ya kukabiliana na ugonjwa huo kuzuia usienee.

Hata hivyo, hatua zilizochukuliwa kipindi cha mwezi Juni, 2020 ‘kilizaa matunda’ ambapo Tanzania, mapinduzi yalishuhudiwa kwenye kampeni ya ukusanyaji damu kitaifa, ambayo ilifanyika kuelekea kilele cha siku ya wachangia damu duniani.

Hatua hiyo ilifikiwa kutokana na ushirikiano mkubwa wa wadau wa vyombo vya habari kwenye kutoa elimu kwa jamii ambayo ilisaidia kuwaondolea hofu wananchi na kujitokeza kuchangia damu.

Kipindi hicho Tanzania ilikuwa katikati ya mapambano dhidi ya Corona, ambapo kampeni hiyo ililenga kukusanya chupa za damu 24,800 na makusanyo yalikuwa chupa 18,075 sawa na asilimia 79.3.

Takwimu za NBTS zinaeleza katika kampeni hiyo ambayo wananchi walijitokeza kwa wingi kuchangia damu kwa hiyari, timu za halmashauri walikusanya jumla ya chupa za damu 14,841 sawa na asilimia 67.5 na timu za Kanda 3234 sawa na asilimia 116.

RIPOTI ZA WHO

Kila nchi ili itosheleze mahitaji yake inahitaji kukusanya damu kiasi cha asilimia moja ya idadi ya watu wake, kulingana na tathmini ya WHO.

Hivyo, kwa idadi ya Watanzania zaidi ya milioni 50 kulingana na Ofisi ya Taifa ya Takwimu, Tanzania inahitaji kukusanya chupa za damu salama zipatazo 550,000 kutosheleza mahitaji yake.

“Lakini hatujawahi kufikia kiwango hicho, ingawa tumedhamiria kukifikia, kwa mwaka 2015/16 tulikusanya chupa za damu 196,000, mwaka 2016/17 chupa za damu 233,000, mwaka 2018/19 chupa za damu 309,376,” anabainisha Dk. Liymo.

Anasema katika chupa za damu 309,376 kundi lililochangia kwa kiwango kikubwa lilikuwa la O+ kwa kiwango cha asilimia 51 na kwamba kwa makundi adimu ikiwamo A-, B-, AB- na O- hayo ukusanyaji wake ulikuwa chini ya asilimia moja.

“Hawa wenye makundi adimu walikuwa wachache mno, ndiyo maana sasa hivi tunawaweka kwenye kanzi data zetu, ili tuwafahamu na kuendelea kuwahimiza kuchangia damu kwa ajili ya kuokoa maisha ya wahitaji wa makundi haya pale inapotokea,” anabainisha.

USALAMA NA UBORA

Dk. Liymo anasema damu zote zinazokusanywa nchini huchunguzwa usalama na ubora wake kabla ya mgonjwa kuongezewa.

“Tunazifanyia uchunguzi wa kimaabara iwapo zina maambukizi ya Homa ya ini B na C, Virusi Vya Ukimwi na kaswende zile zitakazokuwa salama ndizo zinazotumika na zile ambazo si salama zinaharibiwa,” anasema.

Anafafanua “Kwa mfano, tunachukua nusu lita ya damu kutoka kwa mchangiaji (sawa na mils 450), ikiwa kiasi hicho cha ujazo hakikufika au kimezidi, au kukawa na matatizo kwenye uhifadhi, na kasoro nyinginezo zitakazobainika, damu hiyo inaondoshwa, haitatumika.

“Tunahakikisha, damu tangu imechukuliwa kwa mchangiaji, imepita kwenye hatua zote za uchunguzi wa usalama na ubora wake hadi inamfikia mgonjwa inakuwa imekidhi vigezo vyote,” anasema.

Meneja huyo wa NBTS anaongeza “Mwaka 2019 asilimia 15 ya damu iliyokusanywa iliharibiwa ambapo asilimia 13 ilibainika kuwa na maambukizi ya magonjwa na asilimia mbili haikufikia vigezo vinginevyo vya ubora na usalama.

“Kimsingi tunataka kuwahakikishia watu damu inayotumika imekidhi vigezo vyote vya ubora na usalama,” anasisitiza.

Anasema katika utoaji wa huduma baadhi ya makundi ya watu kwenye jamii hupewa kipaumbele kuhakikisha yanapohitaji damu salama yanahudumiwa ikiwamo lile la wagonjwa wa siko seli, saratani, wajawazito na watoto chini ya miaka mitano.

UTENGENEZAJI MAZAO

Dk. Magdalena anasema NBTS huzalisha mazao ya damu ambapo kwa kila chupa moja (unit) huweza kuzalisha mazao matatu na hivyo kuokoa uhai wa wagonjwa watatu wenye uhitaji kwa wakati mmoja.

“Tunazalisha plasma, chembe sahani na chembe nyekundu, lakini ikiwa tunabaini damu haikuwa salama hata yale mazao yake hatuwezi kuyatumia kwani si salama, hivyo tunayaharibu,” anabainisha.

Anabainisha “Kwa kuzalisha mazao ya damu tunaweza kuhudumia wagonjwa watatu kwa kila chupa moja ya damu, kwa sababu tunapata mazao ya aina tatu, mgonjwa wa saratani atahitaji chembe sahani ataongezewa, anayejifungua atahitaji chembe nyekundu ataongezewa.

Swali linasalia, Je! Watanzania wamejifunza na kubadili mtizamo juu ya uchangiaji damu badala ya kusubiri kuhimizwa na kufuatwa kuchangia damu wajenge utamaduni wa kuchangia wenyewe kwa hiyari?

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement