Na Mwandishi Maalum – Dar es Salaam
Taasisi ya Tiba ya Mifupa na Mishipa ya Fahamu Muhimbili
(MOI) kwa mara ya kwanza imeanza kutoa huduma ya uchunguzi wa mishipa ya damu
kwenye ubongo bila kufungua fuvu la kichwa katika maabara ya kisasa ya upasuaji wa ubongo (Angio Suite).
Uchunguzi huo umefanywa kwa saa tatu na jopo la
madaktari bingwa, wauguzi, watalamu wa radiolojia wazalendo sita kutoka MOI, Hospitali
ya Taifa Muhimbili (MNH), Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) pamoja na
hospitali ya Aghakhan.
Mkurugenzi Mtendaji wa MOI Dkt Respicious
Boniface amesema kuanza kwa maabara hii ni ishara ya mageuzi makubwa katika
sekta ya afya hapa nchini kwani maabara ya kisasa kama hii haipo kwenye nchi nyingine kwenye ukanda wa afrika
mashariki kati.
“Leo ni siku ya furaha sana kwani tumeanza
kutumia maabara yetu ya upasuaji wa ubongo (Angio suite) ,hii imewezekana
kutokana na dhamira ya dhati ya Mh Rais Dkt John Pombe Magufuli ya kuboresha
huduma za afya hapa nchini kwani maabara hii imejengwa Serikali ya awamu ya
Tano kwa zaidi ya Tsh Bilioni 7.9, kwakweli tunamshukuru sana Mh Rais” Alisema
Dkt Boniface
Kwa upande wake Daktari bingwa wa upasuaji wa
Ubongo MOI Dkt Lemery Mchome amesema kuanza kwa maabara hii kumeleta mageuzi
makubwa katika huduma za uchunguzi na upasuaji wa ubongo hapa nchini kwani
hakuna mgonjwa atakayelazimika kwenda nje ya nchi kufuata huduma hii ambayo
ilikuwa haipatikani hapa nchini.
“Tunashukuru upasuaji umefanyika salama na kwa mafanikio makubwa, tumeweza kufika kwenye ubongo wa mgonjwa bila kufungua fuvu, tumefanya upasuaji huu katika mazingizra mazuri kwani mitambo hii ni ya kisasa sana, kama mnavyoona mgonjwa yuko macho na anaongea vizuri kabisa ,hana kovu wala maumivu, hii ni hatua kubwa sana kwetu kama wataalamu.
Mgonjwa aliyefanyiwa upasuaji huo Bwana Hafidhi
saidi kutoka mkoani Singida amemshukuru Mungu kwa huduma aliyopata kwani
amakuwa akipata maumivu kwa kipindi kirefu bila kujua anasumbuliwa na ugonjwa
gani.
“Namshukuru sana Mh Rais Dkt John Pombe
Magufuli kwa kununua vifaa hivi ambavyo vimesaidia leo nimehudumiwa hapa MOI,
Nawashukuru madaktari na wataalamu wote walionihudumia, nimefurahi sana na
nawaambia watanzania wenzangu wenye shida kama yangu waje wahudumiwe hapa MOI,”
Alisema Hafidhi
Huyu ni mgonja wa kwanza kupata huduma katika maabara hii ya kisasa ya upasuaji wa Ubongo iliyojengwa na Serikali ya awamu ya Tano Kwa zaidi ya Tsh Bilioni 7.9
Jopo la wataalamu kutoka MOI,MNH, JKCI na Agakhan lililofanikisha uchunguzi huo wa kihistoria.
Chapisha Maoni