Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement


Na Veronica Mrema – Mwanza

Je! U miongoni mwa watu wanaobakiza dawa pindi wanapojihisi kupata nafuu? Je! U miongoni mwa watu wanaotumia dawa holela kwa kujinunulia wenyewe madukani (safe medication)? Na Je! U miongoni mwa watu wanaotupa holela dawa zilizobaki nyumbani?

Ikiwa u miongoni mwao, basi unapaswa kubadilika mara moja, kwa sababu hayo ni baadhi ya mambo yanayotajwa kuweka ‘rehani’ afya yako na jamii kwa ujumla.

Kulingana na wataalamu wa afya aina yoyote ya dawa inayotumika kutibu inapaswa mgonjwa kwanza ni lazima aandikiwe na daktari au apatiwe na mfamasia tena baada ya kufanyiwa vipimo vya uchunguzi.

Aidha, dawa husika inapaswa kutumiwa na kumalizwa ndani ya muda aliondikiwa ili kutibu ugonjwa unaomkabili.

Kimsingi, wanasisitiza dawa haipaswi kubakizwa hata ikiwa mgonjwa husika anapata (anahisi) nafuu dhidi ya maradhi yanayomsumbua.

Mkazi wa Busweru Mkoani Mwanza, Eliud Bwire ni miongoni mwa waliohojiwa na MATUKIO NA MAISHA BLOG anasema yeye huwa hamalizi dozi, anapojihisi nafuu kwa sababu huamini kwamba tayari amepona ugonjwa unaosumbua, jambo ambalo ni kinyume na maelekezo ya wataalamu.

“Sasa nitumie ya nini, si nimepona, naacha, wakati mwingine natumia ninapojihisi kuumwa tena, ikiwa sitazitumia kwa muda mrefu kama ni vidonge nitavitupa kwenye shimo la taka kwa sababu naamini zitakuwa hazifai tena kwa matumizi. Nyumbani kwangu sina mtoto mdogo ndiyo maana sioni shaka kuzitupa shimoni, zitakaa humo hadi siku nitakapochoma taka.

“Kama ni dawa za majimaji hizo nazimwaga kwenye sinki, chupa nazitupa shimoni na wakati mwingine simwagi nazitupa humo humo, nitakuja kuchoma kwa pamoja,” anasema.

UHALISIA WA MAMBO

“Kila dawa hutengenezwa na kiambata hai chake na kila kiambata hai kina muda wa kuishi ndani ya dawa husika,” anasisitiza Bugusu Nyamweru ni Kaimu Mkuu wa Maabara ya Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba Tanzania (TMDA – Kanda ya Ziwa).

Nyamweru anasisitiza mgonjwa anapomeza dawa husika kila kiambata hai kina muda wake kutoka mwilini kwenda kutibu ugonjwa husika.

“Mgonjwa anapoandikiwa dozi na daktari anapaswa kuimaliza kwani kiambata hai kina muda wa kuishi ‘expire’ ndani ya dawa husika.

“Kiambata hai kina muda wa ‘kuishi’ ndani ya dawa, ndiyo maana kuna ‘expire date’ (muda wa kuisha kwa matumizi), unapoisha wastani wa asilimia 10 ya kiambata hai hupungua na kubaki asilimia 90.

“Ile asilimia 90 inakuwa na uwezo wa kutibu lakini tunakuwa hatujui mule ndani ile asilimia 10 ambayo imepungua imebadilika kuwa nini, labda imekuwa sumu tayari, hivyo kile kinachoharibika kinaweza kuleta madhara,” anabainisha.

Nyamweru anaongeza “Ndiyo maana hata ‘syrup’ ikishafunguliwa, haitakiwi kubaki kwa sababu inaweza kuleta madhara, tunahimiza watu wazingatie matumizi ya dawa kama walivyoelekezwa na wataalamu.

MAJUMBANI!

Mkaguzi wa Dawa wa TMDA – Kanda ya Ziwa, Mtani Njegere anasema kutupa dawa kwenye mazingira, sinki la maji inaleta athari kubwa kwa binadamu na viumbe hai wengine na hata kusababisha tatizo la usugu wa vimelea vya magonjwa dhidi ya dawa.

“Hatujawahi kufanya tafiti kujua kwa kiwango gani kwenye familia zetu watu wanabakiza dawa na kuzitupa, kwa sababu imani yetu, kimsingi dawa zinapaswa kutumika kama ilivyoelekezwa na daktari na kumaliza.

“Lakini kuna dawa zinabaki majumbani kwetu, mtu anaweza kutumia kabla haijaisha anaiacha, ukienda baadhi ya familia unazikuta.

“Ni vema wananchi wanapokuwa na dawa hizo wawasiliane na maeneo yanayotoa huduma za tiba au famasi, wazirudishe huko ili wao (famasi, vituo vya kutolea huduma za tiba / afya) wawasiliane na sisi (TMDA) kwa ajili ya uteketezaji.

“Kimsingi, dawa hata kama eneo halikai watu haifai kuteketezwa kwenye eneo hilo kwa sababu inaweza kuteketeza hapo lakini ikachukuliwa ama kwa mvua hadi kwenye maeneo ya makazi ya watu na kuleta madhara.

“Kwa mfano hapa Kanda ya Ziwa, inaweza kunyesha mvua, mmeteketeza eneo la wazi, dawa ikachukuliwa hadi ziwani, matokeo yake mtu anajikuta anakula samaki ambaye tayari ana madhara ya dawa.

“Kwa mfano ikiwa ni antibiotics, ziliteketezwa zikasafiri hadi ziwani, samaki wakaathirika, hali ile siku za usoni inaweza kuleta madhara kwa binadamu ikiwamo usugu wa vimelea vya magonjwa dhidi ya dawa,” anasema.

Anaongeza “Ndiyo maana tunahimiza jamii, dawa lazima itumike iishe, lakini ikiwa ilibakizwa isiteketezwe holela, pia wadau wetu  wote wazingatie mwongozo wa utektezaji wa dawa ambao upo wazi ni ‘public document’ ipo pia kwenye webste yetu.

NI JUKUMU KISHERIA

Mtani ambaye pia ni Mratibu Msimamizi wa Dawati la Udhibiti wa Vifaa Tiba na Vitendanishi, TMDA – Kanda ya Ziwa anasema Mamlaka hiyo ina jukumu kisheria la kusimamia uteketezaji salama wa bidhaa za dawa na vifaa tiba nchini kwa mujibu wa Sheria kifungu namba 49 na 85.

Anasema TMDA hutekeleza jukumu hilo kwa kufuata mwongozo wa uteketezaji wa dawa wa mwaka 2009 ambapo hatua mbalimbali hufuatwa.

“Uteketezaji wa dawa na vifaa tiba upo wa aina mbili. Uteketezaji wa hiari wa bidhaa kutoka kwa wafanyabiashara na uteketezaji wa dawa usio wa hiarikwa dawa na vifaa tiba vilivyokamatwa kwa sababu mbalimbali,” anabainisha.

Anaongeza “Uteketezaji wowote kati ya aina hizo mbili hufuata sheria ya dawa sura 219, kanuni za uhifadhi na uteketezaji wa dawa za mwaka 2015 zilizotengenezwa chini ya kifungu 122 cha Sheria ya Dawa na Vifaa Tiba na mwongozo wa uteketezaji wa dawa wa mwaka 2009.

UTEKETEZAJI WA HIARI

Mtani anasema hatua mbalimbali hufuatwa ikiwamo kufanya maombi ya kuteketeza dawa kutoka muhusika anayehitaji kuteketeza dawa au vifaa tiba (kwa watoa huduma za afya, maduka ya dawa).

“Hatua hii ya maombi huambatana na orodha ya dawa na vifaa tiba vinavyopaswa kuteketezwa ambayo kawaida huandaliwa kutoka katika rejesta ya dawa au vifaa tiba vilivyokwisha muda wake wa matumizi.

“Orodha huwa na taarifa muhimu za dawa, kwa mfano jina la biashara la dawa, jina halisi la dawa (generic name), nguvu ya dawa, aina ya dozi (vidonge, sindano kapsuli na nyinginezo), toleo la dawa au vifaa tiba, tarehe ya kwisha muda wa matumizi, kiasi cha dawa, thamani na sababu ya kuteketezwa,” anasema.

Mtani anaongeza “Maombi hayo siku hizi yanaweza pia kufanyika kwa njia ya mtandao wa taasisi hiyo kupitia mfumo wa imis2.tmda.go.tz/portal.

Anasema baada ya maombi na orodha kuwasilishwa katika ofisi za mamlaka hiyo, wakaguzi huandaa ukaguzi kuthibitisha taarifa zilizowasilishwa na thamani halisi iliyowasilishwa.

FOMU MAALUM

“Katika ukaguzi huu, wakaguzi pia hupendekeza njia bora ya uteketezaji wa dawa kulingana na aina ya dawa husika, ukaguzi wa kujiridhisha hufanyika na taarifa zote hujazwa katika fomu maalum ‘verfication form) ambayo husainiwa pia na mmiliki wa dawa au vifaa tiba vinavyotakiwa kuteketezwa,” anabainisha.

Anasema iwapo bidhaa zitathibitishwa pamoja na thamani, Mamlaka hiyo hupanga tarehe na mahala ambapo zitateketezwa na kumjulisha mteja kwa barua.

“Tunaiandikia pia Mamlaka ya usimamizi wa eneo ambako uteketezaji utafanyika ili kuwajulisha juu ya jambo hilo, TMDA huwajibika kuzitaarifu taasisi zingine zinazohusika ili kushiriki katika uteketezaji huo likiwamo Jeshi la Polisi, Mfamasia, Afisa Mazingira, Usalama wa Taifa na mwakilishi wa mmiliki wa dawa au vifaa tiba vinavyoteketezwa,” anabainisha.

USALAMA WA VIUMBE

Mtani (pichani) anasisitiza “Uteketezaji wa dawa hufanyika kwa kuzingatia sheria zilizopo ambazo hulenga kulinda usalama wa mazingira na viumbe vilivyomo.

“Pamoja na mwongozo wa uteketezaji salama wa dawa nchini, pia tunazingatia Sheria ya Baraza la Mazingira nchini (NEMC).

“Kutokana na tabia za dawa mbalimbali, tuna wajibu wa kuainisha njia sahihi ambayo hufaa kwa uteketezaji fulani ili kuhakikisha usalama wa mazingira na viumbe unalindwa,” anasema.

Anasema baada ya uteketezaji kukamilika fomu maalum hujazwa (disposal waste) ambayo huainisha eneo ambapo uteketezaji umefanyika, njia iliyotumika kuteketeza bidhaa husika, uzito na thamani halisi bidhaa iliyoteketezwa.

“Fomu hiyo kwa kawaida husainiwa na maafisa waliosimamia uteketezaji pamoja na mmiliki au mwakilishi wa mmiliki wa bidhaa husika,” anabainisha.

Anasema uteketezaji unapokamilika cheti maalum utolewa ‘disposal certificate’, cheti hicho cha uteketezaji wa dawa au vifaa tiba huwa na taarifa muhimu ikiwamo njia iliyotumika kuteketeza, kiasi au uzito wa dawa pamoja na thamani ya dawa au vifaa tiba.

“Kila wakati ni jambo muhimu na la msingi kuzingatia njia sahihi za uteketezaji salama wa dawa au vifaa tiba, kwa sababu husaidia kuhakikisha uteketezaji umekamilika na bidhaa zimeharibiwa kwa asilimia 100.

“Hivyo hazina madhara tena kwa mazingira na viumbe, kuhakikisha tukio zima la uteketezaji halizalishi kemikali au mazao ambayo yanaweza kuathiri mazingira na viumbe katika eneo husika,”  anasisitiza Mtani.

BAADHI YA NJIA ZINAZOTUMIKA

“Dawa ngumu, nusu –imara na poda hizi tunatumia njia ya kufukia, joto la juu 850C hadi 1000C na kupunguza kusambaa (immobilization).

“Kwa vimiminika tunateketeza kwa kupitisha chini ya ardhi katika mabomba maalum (sewer), kwa joto la juu, kubadili dawa ili kutokuwa na madhara kwenye mazingira (treated waste),” anasema.

Anaongeza “Dawa za saratani tunateketeza kwa kubadili dawa ili kutokuwa na madhara katika mazingira au kufukia, kuteketeza kwa joto la juu au kurudisha kwa mtengenezaji.

“Dawa zinazodhibitiwa (enye dawa za kulevya) tunateketeza kwa kubadili dawa ili kutokuwa na madhara katika mazingira au kufukia, kuteketeza kwa joto la juu.

“‘Aerosol and Inhalers’ hizi tunazifukia bila kubadili dawa ili kutokuwa na madhara katika mazingira.

“Vipukusi hivi tunateketeza kwa kupitisha chini ya ardhi katika mabomba maalum (sewer) au kupitisha katika maji yaendayo kasi.

“PVC plastiki, glass (ampuli, chupa na vials) hizi tunafukia au kubadili na kuzitumia tena (re-cycling) na kwa upande wa ‘paper na cardboard’ hizi tunabadili kwa matumizi mengine tena, tunachoma au kufukia,” anabainisha.

Mtani Anaongeza “Dawa nyingi ambazo tumekuwa tukiteketekeza kwenye mazingira yetu zina sifa ya kuteketezwa kwenye vinu vyenye joto la juu, kwa hapa mazingira yetu (Kanda ya Ziwa) tunateketeza Hospitali ya Rufaa ya Kanda - Bugando.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement