Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement


Na Veronica Mrema - Dodoma

Mgonjwa mmoja mwenye tatizo sugu la figo (kidney failure) huhitaji huduma ya uchujaji damu ‘dialysis’ si chini ya mara tatu kwa wiki, katika kila awamu hulazimika ‘kukaa’ kwenye mashine kwa wastani wa saa nne.

Hii ni ratiba mpya ambayo mtu aliyegundulika kuugua tatizo hilo hulazimika kuianza na kuishi nayo maisha yake yote ama hadi pale atakapofanikiwa kupata mtu wa kumchangia figo nyingine ya kupandikizwa.

Kulingana na wataalamu wa afya, kuna aina mbili za magonjwa ya figo, yale ya dharura na sugu.

Wanatoa mfano kwamba, mjamzito anapopoteza damu nyingi wakati wa kujifungua au majeruhi wa ajali akipoteza damu nyingi, hupata tatizo la dharura la figo, figo hushindwa kabisa kufanya vema kazi yake ya kutoa sumu taka mwilini.

“Mtu anapougua ugonjwa wa dharura wa figo, ikiwa hatagundulika mapema na kupatiwa matibabu sahihi kwa wakati anaweza kuishia kuugua ugonjwa sugu wa figo, yaani figo zake hushindwa kabisa kufanya kazi yake ya kuchuja sumu taka mwilini,” anasema Mtaalamu wa Afya ya Jamii wa Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH), Dodoma, Awadhi Mohamed.

Anaongeza “Yapo baadhi ya magonjwa ikiwamo kisukari, shinikizo la damu mtu anapougua, asipotibiwa kwa wakati, asipozingatia maelekezo ya wataalamu anaweza pia kuishia kuugua ugonjwa sugu wa figo.

“Figo ni kiungo chenye umuhimu mkubwa kwa binadamu ikiwamo kuweka sawa ‘pressure’ ya mwili. Tatizo la ‘pressure’ na ugonjwa wa figo, ukiangalia kwa kina utaona ni kama vile kuku na yai.

“Yaani ‘pressure’ inaweza kusababisha figo kuathiriwa, vile vile figo zikipata shida zinaweza kuathiri ‘pressure’ ya mwili,” anasema.

Mohamed anaongeza “Mtu huyu anaweza kupata athari kubwa kwa sababu kazi kubwa ya figo ni kutoa sumu taka mwilini, hivyo kama hazitoki atabaki na kiasi kikubwa cha maji mwilini.

“Anaweza kupata shida ya kupumua, mwili kujaa maji, kuvimba, kwa sababu sumu hazitoki mwilini mtu huyo tunategemea atabaki na kiasi kikubwa cha maji mwilini, shida ya kupumua.

“Figo zinasaidia pia katika uzalishaji wa chembechembe hai za damu mwilini, ambazo humsaidia binadamu damu yake kuongezeka inapokuwa imepungua na kuzalisha damu mpya.

“Ndiyo maana binadamu anaweza kuchangia damu na baada ya muda damu inarudi katika kiasi kile ambacho kinahitajika mwilini mwake,” anabainisha.

Anaongeza “Lakini figo zinaposhindwa kufanya kazi, hali hiyo huweza kusababisha mtu kupata upungufu wa damu mwilini mwake.

SUMU TAKA

Mohamed (pichani) anasema mtu akipata athari ya figo, sumu taka hazitoki, kuna uwezekano akashindwa kupata haja ndogo.

“Kwa sababu, haja ndogo hutengenezwa kutokana na ule uchakataji wa sumu taka mwilini ili kuzitoa nje kwa njia ya mkojo.

“Kwa kuwa sumu taka hazitoki mwilini kwa njia ya haja ndogo, zinaanza kuwa nyingi mwilini, hatimaye muhusika anakuwa kwenye hatari ya kupoteza maisha, ikiwa kitakachofanyika (matibabu) kwa wakati,” anasema.

Anaongeza “Hivyo, atahitaji kutengenezewa njia mbadala kumsaidia, ndiyo hiyo ya usafishaji wa damu (dialysis) ili kuondoa sumu taka mwilini na pia kupunguza kiwango kikubwa cha maji mwilini mwake.

“Kwa sababu, zile sumu tyaka hazitoki mwilini, ndizo zinazomletea athari kubwa, kwa hiyo kinapunguzwa ili kumrudisha mtu kwenye hali yake,” anasema.

MASHARTI MUHIMU

Mohamed anasema lakini kwa sababu mtu huyu anaendelea kuishi, kula na kunywa maana yake atahitaji kuendelea kufanyiwa ‘dialysis’ kwa maisha yake yote hadi pale atakapoweza kupata mtu wa kumchangia figo nyingine, apandikizwe.

“Mgonjwa atapewa masharti maalum ya kuzingatia nini ale, nini asile, nini anywe, kwa kiwango gani ili kumsaidia asipate matatizo mengine yanayoweza kumfanya augue,” anasema.

Anaongeza “Ni kipindi kigumu, maisha yake hubadilika ghafla, ukiacha huo muda wa kukaa kwenye mashine akipatiwa huduma hiyo, bado kuna muda wa kwenda hospitali na kurudi nyumbani, kuna suala la gharama na mengine mengi.

“Si kila mtu huweza kwa haraka sana kubadilika na kuikubali haraka hali hii mpya, kwa mfano unakuta mwingine ni mwajiriwa, pengine anaishi eneo mbali na kilipo kituo cha usafishaji damu.

“Unakuta alikuja hospitali akitarajia kutibiwa na kurudi nyumbani lakini sasa analazimika kukaa kwa muda kwa ajili ya kufanyiwa ‘dialysis’, tayari hii ni shida kwake,” anasema.

Anaongeza “Atakaa hospitali kwa siku kadhaa na anaporuhusiwa bado atatakiwa kurudi tena hospitalini kliniki, athari  tunaanza kuiona, huenda ana familia inayomtegemea, sasa hawezi tena kuisaidia, analazimika kuomba msaada.

“Je, jamii inayomzunguka nayo inamuelewa namna gani, ipo tayari kumsaidia?.. mambo mengi yanajitokeza, hapo ndipo kitengo chetu umuhimu wake ulipo, kuhakikisha familia yake inaelewa ugumu wa aina ya matibabu anayoyapitia.

“Je! Yanachukua muda gani na yanawahitaji kiasi gani ili yawe endelevu kwa mgonjwa husika,” anafafanua Mtaalamu huyo wa Afya ya Jamii BMH.

Anasema hivyo, kitengo hicho humsaidia mgonjwa kumuunganisha na huduma nyingine pale inapohitajika.

“Kwa mfano, inawezekana alikuja hospitalini akiwa ameaga siku mbili kazini, amefika amepewa ratiba mpya ya kukaa mwezi mzima kwa matibabu, lazima ofisini kwake wajulishwe, kitengo chetu kinahusika kufikisha taarifa hiyo.

“Wengine wanalazimika kuhitaji msaada wa kuhamia vituo vya kazi jirani na vituo vya usafishaji hadi pale watakapomaliza matibabu (upandikizaji figo),” anasema.

Mohamed (pichani) anaongeza “Hiyo ni hatua ya mbele, hatuwezi kwenda kwenye upandikizaji kama hali yake ya ugonjwa inahitaji usafishaji kwanza.

NAFASI YAO

 “Idara yetu inawajibika pia kuhakikisha huduma zote zinazotolewa hapa zinakuwa rafiki kwa watu wote, zinafurahiwa na kila mtu na lengo la matibabu linafikiwa,” anasema.

Anaongeza “Kulingana na tafsiri ya neno afya, kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), ni ile hali ya mtu kuwa vizuri kimwili, kiakili na kijamii na si tu kuwa na ugonjwa ama udhaifu mwilini mwake.

“Tafsiri hii ilitolewa na WHO tangu mwaka 1948 hadi sasa haijabadilishwa, ndiyo sababu katika hospitali wapo watalaamu mbalimbali ikiwamo wanaohusika na masuala ya afya ya jamii.

“Wataalamu hao wanafanya kazi upande wa pili wa kimatibabu ukiacha yale yanayohusisha utaalamu wa kitabibu moja kwa moja, dawa, upandikizaji, na mengineyo,” anasisitiza.

Mohamed anasema katika maeneo yote ya hospitali kuna kipande ambacho ni lazima mtu awe imara kama maana ya afya inavyoeleza kiafya, kijamii na kiuwezo.

“Kwa maana ya mtu kujiweza katika kufanya maamuzi, katika kukubali, kufahamu vitu na shida gani imempata, na anatakiwa apitie taratibu zipi za matibabu, itachukua muda gani, ni ugumu gani atakutana nao.

“Katika yote hayo kuna kujengewa hali ya mtu kuweza kuishi hali aliyonayo, hapo ndipo hizi timu zinakutana (daktari na ‘social worker’), kila mmoja atatoa huduma kwa upande wa utaalamu wake, kumsaidia mgonjwa husika,” anasema.

Anaongeza “BMH tumefanikiwa kuwapandikiza figo wagonjwa zaidi ya 15, kwa zaidi ya asilimia 95 wanazingatia maelekezo tunayowapa, asilimia iliyobaki bado kuna changamoto katika kuzingatia, tunazidi kuongeza juhudi kuwahamasisha wazingatie kwa kutumia mbinu mbalimbali tulizonazo.

“Zaidi ya asilimia 98 ya wagonjwa wanaopata huduma ya ‘dialysis’ BMH  awali walipofika hapa hawakuwa wanajua hali zao na kwamba wanatakiwa kuanza kupata huduma hiyo, mapema,” anabainisha.

Picha zote kwa hisani ya BMH 

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement