Na Mwandishi Maalum
Vimelea vya bakteria {Escherichia coli}, ambaye kwa kawaida anaishi katika takamwili za mfumo wa chakula wa binadamu na wanyama wengine {kinyesi} vimebainika kuwapo kwenye juisi za miwa katika baadhi ya maeneo huko Nyamagana, Mwanza.
Utafiti huo wa awali umefanywa na watafiti wa Chuo Kikuu cha Utafiti Kikatoliki cha Sayansi za Afya (CUHAS – Bugando) na kuchapishwa katika Jarida la Kongamano la Kisayansi la 12 la Chuo hicho.
Watafiti wameeleza utafiti huo ulilenga kuonesha hali halisi ya usafi kwa juisi za miwa zinazouzwa wilaya ya Nyamagana Jijini Mwanza.
Wameeleza kwamba walitumia njia za kimaabara kuonesha uwepo wa bacteria huyo.
"Kwa hiyo kama bacteria huyu akipatikana katika chakula, maji au vimiminika vingine kama juisi, hali hii inaonyesha viashiria vya uwepo wa takamwili," wamesema.
Utafiti huo ulihusisha wajasiriamali {wauzaji} 24 wa bidhaa hiyo ambao waliombwa ridhaa ya kushiriki.
Kulingana na andiko hilo, wajasiriamali hao waliulizwa maswali mbalimbali kuhusiana na uandaaji wa juisi zao.
Watafiti hao walichukua sampuli 120 za juisi kwa muda wa siku tano na kufanyiwa uchunguzi wa maabara chuoni hapo.
"Asilimia kubwa ya sampuli zilionekana kuwa na bacteria, 96.7% (116/120) na kati ya hizi sampuli 71 zilikuwa na bacteria Escherichia coli," wamesema.
Wakati utafiti ukiendelea watafiti waliendelea kutoa elimu kuhusu usafi wa mazingira ya kazi kwa wauzaji, usafi wa mikono na njia zingine kuhakikisha juisi zao zinakuwa bora.
Kwa hatua hiyo utafiti ulionesha uwepo wa bacteria katika juisi uliendelea kupungua kadri elimu ilivyokuwa ikiendelea kutolewa kutoka asilimia 87.5 (sampuli 21 za juisi kati ya sampuli 24 zilizopimwa) siku ya kwanza mpaka asilimia 45.8 (sampuli 11 za juisi kati ya sampuli 24 zilizopimwa) siku ya tano," wanaeleza watafiti hao.
Wamesema huo ni utafiti wa awali na unasisitiza kuongeza elimu zaidi kwa watengenezaji na wauzaji wa juisi
za miwa ili kuhakikisha bidhaa hizi zinakidhi ubora.
Imeelezwa Chuo hicho kwa kushirikiana na taasisi zingine wamepanga kuwaleta pamoja wajasiriamali hao na kuwapa mafunzo zaidi kuhusu uandaaji wa juisi kwa kuzingatia vigezo mbalimbali vya ubora.
"Baaada ya hapo tutafanya tena
ukusanyaji wa sampuli na kuona ni kwa kiwango gani tatizo hili limepungua au
kutoweka kabisa.
"Tutaangalia kwa kina mnyororo wa uandaaji wa juisi hizi za miwa ili kujua
eneo/hatua halisi ambapo bacteria Escherichia coli anaingia katika juisi (Je, ni katika mashamba au ni katika usafirishaji au mazingiria ambako juisi
inaandaliwa au maji yanayotumika au mikono ya waandaaji?) ili kusaidia
kukinga tatizo hili .
Asante kwa Elimu hakika Nimewapenda Sana kwa haya hakika mko making Sana
JibuFutaAsante kwa pongezi msomaji wetu, tumedhamiria kukujuza/kukuelimisha. Karibu sana
FutaChapisha Maoni