Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement


Na Veronica Mrema

Upo uwezekano mkubwa wa beseni la kumuogeshea mtoto kugeuka ‘kiota’ {chanzo} cha kupata maambukizi ya U.T.I {Urinary Track Infection} mara kwa mara na hali hiyo ya kujirudia rudia kwa U.T.I kunaweza kusababisha magonjwa ya figo, hata hivyo jamii haina uelewa juu ya hili.

Hata kitendo cha kumuacha mtoto na nepi/‘pampasi’ kwa muda mrefu kinamuweka kwenye hatari ya kupata U.T.I mara kwa mara, endapo hujisaidia na kukaa kwa muda mwingi pasipo kubadilishwa na kusafishwa vema.

U.T.I ni ugonjwa unaosababishwa na maambukizi ya bakteria ambaye vimelea vyake hushambulia mfumo wa mkojo hususan kibofu, mrija wa urethra na figo zenyewe.

Magonjwa ya figo nayo yamegawanyika katika makundi makuu mawili, yale ambayo hutokea kwa dharura {acute kidney failure} na yale ya kudumu {chronic kidney failure}, vipo vyanzo/sababu nyinginezo pia zinazoweza kusababisha magonjwa haya.

Yameelezwa hayo na Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili, Profesa Francis Furia alipozungumza katika mahojiano maalum na MATUKIO NA MAISHA BLOG hivi karibuni, yaliyoangazia magonjwa ya figo kwa watoto.

“Jambo la msingi linalopaswa kuepukwa hapa ni kuto-kumuogesha mtoto akiwa amekalishwa ndani ya maji badala yake aogeshwe akiwa amesimama wima,” amesisitiza Prof. Furia.

Amefafanua zaidi kwamba “Wadudu wanaosababisha maambukizi ya bakteria kwenye njia ya mkojo wengi wanapatikana kwenye kinyesi, kwa hiyo kinyesi kikiingia kwenye njia ya mkojo, wale wadudu watasababisha U.T.I.

“Kwa hiyo, mtoto akikaa na nguo/nepi/‘pampasi’ ambayo imeshika kinyesi kwa muda mrefu kuna uwezekano kile kinyesi kikaingia njia ya mkojo kikasababisha maambukizi ya U.T.I, usafi wa mtoto ni muhimu,” amesema.

Pamoja na hayo, Prof. Furia amesisitiza kwamba “Watoto kupata U.T.I mara kwa mara cha kwanza, kuna uwezekano wana matatizo ya kimaumbile {congenital abnormalities} katika mfumo wa mkojo.

“Njia ya mkojo imeumbwa kwa ajili ya kuhakikisha kwamba mkojo ukitoka kwenye figo unaenda moja kwa moja kwenye kibofu kisha unatoka nje. Kama kuna kitu chochote kinazuia mkojo usitoke nje, mkojo ukikaa kwenye kibofu kwa muda mrefu unasababisha maambukizi ya bakteria wanaoishi pale wasababishe U.T.I.

Amefafanua “Kwa hiyo kila mtoto anapopata U.T.I yale maambukizi ya bakteria huwa yanaathiri figo, zinakuwa na makovu, yale makovu yanaharibu utendaji kazi wa figo kwa muda mrefu, hivyo kupata maambukizi ya bakteria kwenye njia ya mkojo mara kwa mara husababisha figo ziharibike.

Prof. Furia ambaye pia ni Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Figo kwa Watoto, Hospitali ya Taifa Muhimbili {MNH}, amesema kwenye kliniki zao huona watoto waliozaliwa na matatizo ya figo na wengine waliyapata katika kipindi cha ukuaji, kutokana na kuugua magonjwa mengine kama vile malaria.

“Kwa wastani kliniki kwa siku wanakuja wagonjwa wapatao 15 hadi 20, kuanzia wachanga hadi miaka 16, si wapya hawa wanakuja kliniki mara kwa mara, wapo wa miaka 10 iliyopita tunaendelea kuwaona, wengine walianza kliniki wakiwa shule ya msingi na sasa wamefika vyuo vikuu,” amebainisha.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement