moja

Responsive Advertisement


Na Veronica Mrema – Dar es Salaam

Ipo hatari kubwa {high alart} kwa Tanzania kupata maambukizi ya mlipuko wa ugonjwa wa Ebola, ambao upo nchi jirani ya Uganda, ikiripotiwa kirusi kilichozuka huko hakuna chanjo ya kukidhibiti duniani.

Ukaribu na muingiliano mkubwa wa idadi ya watu wa mataifa haya mawili ya Afrika Mashariki kupitia njia rasmi za usafiri zinaongeza tishio hilo, huku pia ikitajwa changamoto ya uwepo wa njia zisizo rasmi.

Tanzania kupitia Wizara ya Afya imewaagiza wakuu wa mikoa kujiandaa ipasavyo kumtambua mapema mhisiwa yeyote mwenye dalili za Ebola, kumtenga na kumpa matibabu.

Wameagizwa kuandaa timu za wafuatiliaji za wataalamu, ‘ambulance’ za kuwasafirisha, dereva hadi eneo la maziko iwapo kifo kitatokea.

Wizara imesisitiza mtu aliyefariki kwa ugonjwa huo atazikwa na jopo maalum na kwa heshima zote kulingana na miongozo ya kimataifa.

Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu ametoa maelekezo hayo mbele ya waandishi wa habari wakati alipokuwa akitoa tahadhari kwa wananchi juu ya ugonjwa huo uliozuka Uganda tangu Septemba 20, 2022.

“Hadi sasa hakuna kisa chochote kwa Tanzania,” amesema.

Waziri Ummy ameongeza “Ripoti ya Wizara ya Afya Uganda zinaeleza kufikia Septemba 26, 2022 tayari wagonjwa 43 na vifo 23 vimerekodiwa.

“Ni takriban kilometa 130 kutoka ilipo Wilaya ya Mubende hadi Kampala, Makao Makuu ya Uganda na takriban kilometa 220 kutoka Kampala hadi Mutukula Mkoani Kagera, Tanzania.

“Umbali kutoka Mubende kwenda Mutukula Mkoani Kagera Tanzania kupitia Masaka ni umbali wa kilomita 230,” amesema.

Ameongeza “Taarifa zinaonesha kuwa watu hawa wana dalili za homa kali, degedege, kutapika matapishi yenye damu, kuharisha na kutokwa damu machoni.

“Uchunguzi wa kimaabara umethibitisha kuwepo kwa ugonjwa wa Ebola anuai aina ya Sudan (Ebola-Sudan strain).

“Hadi sasa jumla ya watu 425 waliotangamana na wagonjwa (Contacts) wameanishwa na kati yao watu 127 wamepatikana na wanafuatiliwa ikiwa wataonyesha dalili za kuwa na ugonjwa huu.

“Uwepo wa ugonjwa wa Ebola katika nchi jirani unaiweka nchi yetu katika hatari kubwa kutokana na mwingiliano mkubwa wa shughuli za kiuchumi na kijamii kupitia mipaka rasmi na isiyo rasmi.

Ameongeza “Uchambuzi wetu umeonyesha kuwa Mikoa iliyo hatarini zaidi ni Kagera, Mwanza, Kigoma, Geita na Mara.

“Aidha Mikoa ya Dar es salaam, Arusha, Kilimanjaro, Songwe, Mbeya na Dodoma ipo katika hatari kwa sababu ya uwepo wa viwanja vya ndege na vituo vikubwa vya mabasi ya kutoka nchi jirani.

“Hata hivyo, hadi sasa hakuna mgonjwa wa Ebola nchini Tanzania. Hivyo yatupasa kila mmoja wetu kuchukua hatua na kuhakikisha ugonjwa huu hauingii nchini.

“Kwa mamlaka niliyopewa nawaagiza wakuu wa mikoa kujiandaa na ni lazima waainishe gari lipi la wagonjwa ‘ambulance’ itatumika, timu ya wataalamu wa ufuatiliaji, mtu yupi wa maabara atahusika katika kuchukua sampuli.

“Mgonjwa akipatikana atapelekwa wapi, vifaa vitawekwa wapi, tusidharau tetesi yoyote kuhusu wahisiwa wa Ebola, waandae maeneo ya maziko tukipata kifo cha mgonjwa wa ebola tunapaswa kumuhifadhi wapi.

“Waliokuwa karibu na mgonjwa pia wanapaswa kufuatiliwa na wakuu wa mikoa wajue watawekwa wapi,” ameagiza.

Ameongeza “Tusidharau hata dalili ya homa maana wagonjwa wengi wa Uganda waliliripoti dalili hii, dalili nyingine ambazo waliripoti ni degedege, kutapika matapishi yenye damu, kuharisha na kutokwa damu machoni.

Uchunguzi wa kimaabara umethibitisha kuwepo kwa ugonjwa wa Ebola anuai aina ya Sudan (Ebola-Sudan strain) na hauna chanjo.

Waziri huyo mwenye dhamana ya afya amesema Ugonjwa wa Ebola uligundulika kwa mara ya kwanza mwaka 1976 katika nchi za Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) na Sudan.

Tangu kugundulika kwake, kumekuwa na milipuko kadhaa katika nchi za Uganda na DRC ambapo DRC imekuwa na milipuko mingi zaidi. Nchi za Uganda na DRC tunapakana nazo

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement