Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement

Na Veronica Mrema – Dar es Salaam

Msemo uliozuka ghafla na kujizolea umaarufu miongoni mwa jamii hususan kwa kundi la vijana ‘mwagilia moyo’, wakiutumia kuhimizana ‘kula’ starehe haswa unywaji wa pombe kupita kiasi, utawagharimu wengi siku zijazo.

Wataalamu wa afya wamezidi kutoa tahadhari, pombe ni kati ya vichochezi / visababishi ambavyo kwa kiasi kikubwa huchangia mtu kuishia kwenye janga la magonjwa yasiyoambukiza {sugu}.

Magonjwa hayo ni pamoja na yale ya moyo, saratani, shinikizo la damu, kisukari, kiharusi na mengineyo.

Pombe inatajwa kuwa na athari nyingi ikiwamo kusababisha upungufu wa nguvu za kiume, kuzaa watoto wenye ulemavu, saratani za kinywa, koo, ini, utumbo, matiti na tezidume.

Ni kichocheo cha ngono zisizo salama ambazo huchangia kasi ya maambukizi ya magonjwa ya zinaa, Ukimwi na mimba zisizo tarajiwa, ajali za barabarani, nyumbani, ugomvi na athari nyinginezo nyingi.

Akizungumza katika semina maalum ya siku moja kwa waandishi wa habari iliyofanyika kupitia mtandao wa zoom mapema hii leo Mkurugenzi Msaidizi wa Mpango wa Taifa wa Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa Yasiyoambukiza, Dkt. James Kiologwe amesema,

“Magonjwa haya yanazidi kushika kasi, hivi sasa nchini yanachangia takriban 41% ya vifo vyote vinavyotokea kila mwaka na ni gharama kubwa kuyatibu.

Ameongeza “Vijana mna tabia nyingi ngumu… haya mambo ya kumwagilia moyo ni changamoto, wanahabari tusaidieni kuelimisha jamii.

Amesema pamoja na unywaji pombe kupita kiasi, tabiabwete nayo ni changamoto nyingine ambayo inawaweka watu wengi kwenye hatari ya kuishia kupata magonjwa hayo.

“Bado wengi hawafanyi mazoezi, wengine ni wavutaji wa sigara, hawazingatii ulaji unaofaa... wanakula vyakula vyenye chumvi nyingi, sukari nyingi, mafuta mengi na vinywaji vyenye sukari nyingi, hivyo wanazidi kujiweka kwenye uwezekano wa kuishia kwenye magonjwa hayo.

Amesisitiza ni muhimu jamii kuelekeza nguvu zaidi katika kupambana, kudhibiti na kuzuia magonjwa hayo ambayo hivi sasa ni janga kubwa nchini na duniani.

“Tafiti zinaonesha duniani watu milioni 15 wanakabiliwa na kiharusi, 8% wanaishi Afrika na kiharusi pekee huchangia 85% ya vifo vinavyotokea kila mwezi kutokana na kiharusi Barani Afrika.

“Tanzania tafiti zinaonesha 26% ya watu wana Shinikizo la Damu katika Hospitali ya Taifa Muhimbili 33% ya wagonjwa wanaopokea wana kiharusi na hufa ndani ya mwezi mmoja tangu wamepokewa.

“Tafiti zinaonesha pia robo tatu ya wagonjwa hawakuwa wanajua hali zao kabla, walifikishwa Muhimbili wakiwa tayari wamepata madhara yatokanayo na ugonjwa kwa mfano figo kushindwa kufanya kazi.

Ameongeza “Tuna kazi kubwa ya kuelimisha watu, wapime/wachunguze afya zao mara kwa mara, ikiwa mtu ana umri wa miaka 40 na kuendelea inashauriwa angalau mara moja kwa mwaka.

“Magonjwa yasiyoambukiza yanasababisha vifo vya mapema, tafiti zetu zinaonesha kuna zaidi 75% ya watu wana shinikizo la damu nab ado hawajui hali zao.

“Kwa upande wa saratani zaidi ya robo tatu ya wagonjwa wameenda hospitali ikiwa tayari imesambaa sana hatua za juu {tatu na nne ambazo kwa kawaida ni ngumu kutibika na kupona}.

“Zaidi ya 64% ya wenye kisukari hufika hospitalini wakiwa tayari wameanza kupata madhara ya ugonjwa kwa mfano kwenye macho, figo nakadhalika.

Dkt. Kiologwe amesema kutokana na hali hiyo ndiyo maana inashauriwa watu kuchunguza afya zao mara kwa mara waweze kugundulika mapema na kupatiwa matibabu ya mapema ili kuepushwa na madhara yanayoweza kusababishwa na magonjwa hayo.

“Vituo vya afya vihakikishe vinapima kiwango cha sukari kwenye damu, shinikizo la damu na kiwango cha mafuta kwenye damu kila mtu anayefika kituoni kupata huduma.

Amesema wanashauri pia watoto wenye umri chini ya miaka mitano tunashauri wapime macho angalau kila mwaka.

“Ni muhimu pia kina mama kuweka utaratibu wa kuchunguza afya za matiti na kizazi angalau mara moja kwa mwaka,” ametoa rai.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement