Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement
Rwanda

Mataifa yaliyopo Barani Afrika yamehimizwa kuongeza uwekezaji katika mifumo yake ya sekta ya afya ili kuimarisha zaidi ulinzi wa afya ya jamii kwa ujumla dhidi ya majanga na magonjwa mbalimbali hususan ya milipuko.

Rai hiyo imetolewa na Waziri wa Afya wa Rwanda Dkt. Yvan Butera alipokuwa akizungumza wakati wa kuhitimishwa kwa mkutano wa pili wa kimataifa CPHIA, uliofanyika Mjini Kigali.

Mkutano huo uliosimamiwa chini ya shirika la Africa CDC ambao ulijikita kuangazia uwekezaji wa mifumo ili kuimarisha ulinzi wa afya ya jamii Barani Afrika.

“Ni muhimu kuenelea kuwapo ushirikiano kati ya mataifa ya Afrika na washirika wa kimataifa {wadau wa maendeleo} ili kuendeleza ‘uzalishaji’ wa bidhaa za afya kwa ubora zaidi, kuimarisha mifumo ya kukabiliana na dharura, kuimarisha afya kwa wote ulimwenguni,” amesema Dkt. Butera.

“Serikali ya Rwanda kupitia Wizara ya Afya inafuraha kushirikiana na Africa CDC katika utekelezaji wa mpango wa ‘The New Public Health Order’ katika nyanja mbalimbali ikiwamo kuimarisha taasisi za afya ya umma.


Ameongeza “Kujenga nguvu kazi ya afya ya umma, kupanua viwanda vya ndani, kuongeza uwekezaji wa ndani katika afya na kukuza ubia wa kimkakati.

Amesema hayo yote yanaakisi malengo makuu ya mkutano huo katika kuhakikisha mataifa yanaweka ahueni na mifumo imara ya kudhibiti na kuzuia magonjwa ya milipuko na majanga kwa siku zijazo.

Katika hatua hiyo mpya inayolenga kuimarisha mifumo ya ufuatiliaji afya ngazi ya jamii, nguzo muhimu za kufikia malengo zimetajwa ni pamoja na uongozi imara, usawa, uvumbuzi na kujitegemea.

Wadau wameunga mkono kwamba ni vema kuwepo kwa mbinu mpya itakayoyawezesha mataifa ya Afrika kuwa na utayari wa kukabiliana na changamoto za ki-afya kwa siku zijazo.

"Mazungumzo na matukio haya yanaonyesha kile ambacho sote tunafanya ili kufikia lengo, ni wazi kwamba tumetoka mbali tangu tulipozindua mpango wa kwanza mwaka 2020.

“Lakini tuna kazi zaidi ya kufanya kabla ya kila mmoja wa kaka na dada zetu kupata huduma bora za afya,” amesema Kaimu Mkurgenzi wa Africa CDC, Dkt. Ahmed Ogwell Ouma.

Sambamba na hilo, Africa CDC iliweza kutambua michango ya baadhi ya wataalamu wa afya waliojiweka mstari wa mbele katika kuimarisha huduma kwenye mataifa yao.

Miongoni mwa walitambuliwa kwa tuzo maalum ni Dkt. Ameyo Stella Adadevoh kutoka Nigeria ambaye alisaidia mapambano dhidi ya Ebola.

Mwengine aliyetunukiwa ni Prof. Rose Leke kutoka Chuo Kikuu cha masuala ya Sayansi – Cameroon. Africa CDC pia imemtambua Gorreti Marie Zalwango kutoka Uganda na Dkt. Mutia Kehwalla Aza.

Katika mkutano huo makubaliano mbalimbali pia yamesainiwa ili kuhakikisha sekta ya afya inazidi kupewa kipaumbele Barani humo.

Mkutano huo wa siku 3 {13-15 Desemba, 2022} ulifanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kigali ukiwa na washiriki zaidi ya 2,500 kutoka nchi 90 katika Bara la Afrika na kwingineko.

Umewajumuisha wakuu wa nchi na mawaziri wa afya, wanasayansi na watafiti wakuu, wawakilishi kutoka. sekta binafsi, mashirika ya kiraia, mashirika ya kimataifa ya afya na maendeleo.

Uliongozwa na wasemaji wakuu mbalimbali, akiwamo Rt. Mhe. Édouard Ngirente, Waziri Mkuu, Jamhuri ya Rwanda; Mhe. Dk. Yvan Butera, Waziri wa Afya wa Jimbo, Jamhuri ya Rwanda; Dk. Tedros Adhanom Ghebreyesus, Mkurugenzi Mkuu, Shirika la Afya Duniani {WHO}.

Wengine ni Chikwe Ihekweazu, Mkurugenzi Mkuu Msaidizi, Shirika la Afya Duniani {WHO} kwa Ufuatiliaji na Ujasusi wa Dharura wa Afya; Bi Winnie Byanyima, Mkurugenzi Mtendaji UNAIDS,  Prof Awa Marie Coll Seck.

Wengine ni Waziri wa Nchi kwa Rais wa Jamhuri ya Senegal na Dkt. Ahmed Ogwell Ouma, Kaimu Mkurugenzi, Kituo cha Afrika cha Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa {Africa CDC.}

Mkutano wa tatu wa CPHIA unatarajiwa kufanyika Lusaka, Zambia ambapo mwenyeji mkuu wake ni Wizara ya Afya nchini humo.

Picha kwa hisani ya akaunti rasmi za Africa CDC

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement