Na Veronica Mrema
Kuna dalili za wazi kwamba ifikapo mwaka ujao wa 2023 panapo
majaliwa ya Mwenyezi Mungu, unatazamiwa kuwa mwaka utakaoleta furaha {kicheko}
kwa waandishi wa habari nchini Tanzania.
Serikali imeahidi kuanza mwaka huo kwa kushughulikia
ipasavyo changamoto ya maslahi duni kwa waandishi wa habari kadhalika baadhi ya
Sheria ambazo bado zimeendelea kuwa mwiba kwa tasnia hiyo.
Akifungua kongamano la maendeleo ya ya sekta ya habari la mwaka, ndani ya ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Dar es Salaam, Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Nape Nnauye amesisitiza Serikali itasimamia hayo.
Waziri Nape amesema Serikali ina nia ya dhati ya kuboresha sekta hiyo nchini na kwamba itahakikisha inazidi kuweka mazingira bora ya ufanyaji kazi.“Mwaka ujao Serikali imekusudia kuongeza nguvu zaidi
katika kuboresha maslahi ya wanahabari ikiwa ni pamoja na kusimamia mikataba ya
ajira zao na kulipwa madeni yao kutoka taasisi mbalimbali zikiwemo halmashauri
za wilaya,” amesisitiza.
Amesema kongamano hilo ni la kwanza kufanyika nchini na
kuweka wazi litaendelea kufanyika kila mwaka ili kuwaleta pamoja wadau wa
habari na Serikali kujadili mambo muhimu ya kuipeleka mbele tasnia hiyo.
Pamoja na hayo, amehimiza waandishi wa habari kuendelea
kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia miiko na maadili yao na kuhakikisha
wanalinda rasilimali na amani ya nchi.
“Pale ambapo rasilimali zinapotumika vibaya endeleeni kufichua wabadhirifu,” amesema.
Amesisitiza pia ni muhimu waandishi wa habari kuendelea kushirikiana na Serikali katika shughuli mbalimbali ili Taifa lizidi kupata maendeleo na hatimaye kukuza uchumi wa nchi.Kongamano
hilo lilijumuisha wadau mbalimbali wa habari ikiwa ni pamoja na wahariri na
wamiliki wa vyombo vya habari, jukwaa la wahariri wa habari, maafisa habari
kutoka Serikalini, Taasisi Binafsi na Mashirika ya Kimataifa.
Chapisha Maoni