Tanzania
Ndoto na dhamira aliyokuwa nayo kijana Maxmillian Godwin, kusaidia jamii kwa dhati katika kupambana dhidi ya magonjwa yasiyopewa kipaumbele {NTD’s}, imezimika ghafla kwa ajali.
Miongoni mwa magonjwa yaliyo katika kundi hilo ni pamoja na
kichocho, usubi, trakoma {vikope}, matende na mabusha.
Siku kadhaa zilizopita, katika ukurasa wake wa twitter
kijana huyo, ‘alipost’ picha ya gari ndogo aliyokuwa akisafiria.
“… Kipekee namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniepusha na
ajali hii iliyotokea jana, mimi na kaka zangu wawili sote tumetoka salama
kabisa,” aliandika.
Gari hiyo muonekano wake kwa mbele ulikuwa umeharibika mno, hata hivyo usiku wa jana katika mitandao ya kijamii zilianza kusambaa taarifa juu ya kifo chake.
Saidi Livemba ameandika katika ‘tweet’ hiyo ya Maxmillian “Huyu mwamba amefariki, ingawa alisema ametoka salama kwenye hii ajali ila kumbe alikuwa ameumia ndani kwa ndani.
“Dear members, tunasikitika kuwatangazia kifo cha mpendwa wetu Max, tumeambiwa amefariki kwa ajali Songea.Maxmillian ndiye kijana ambaye alitambuliwa mchango wake katika kuelimisha jamii masuala ya afya kwa mwaka 2022.
Akipokea tuzo hiyo mwezi Agosti, ndani ya ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa Julius Nyerere {JNICC}, alimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kumjalia ushindi.
Tuzo hizo hutolewa na taasisi isiyo ya kiserikali ya African Youth Transformation {AYT} kwa ushirikiano na Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na wenye Ulemavu.
AYT ushirikiana pia na wadau wengine mbalimbali wa maendeleo likiwamo Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Masuala ya Watoto {UNICEF}.
Kijana huyo akiwa jukwaani aliwashukuru wote ambao wamekuwa na mchango mkubwa kwake katika maisha yake.
Kipekee alimtaja aliyekuwa Mkurugenzi wa WHO katika Idara ya kushughulikia NTD's, Dkt. Mwelecele Ntuli Malecela kwamba ni miongoni mwa waliokuwa na mchango mkubwa kwake.
Dkt. Mwelecele alifariki dunia, mwaka huu akiwa Geneva Uswizi na mwili wake ulirejeshwa nchini Tanzania na maziko yake kufanyika kijijini kwao Mvumi, Dodoma.
Kupitia mitandao yake rasmi ya kijamii, Mkurugenzi Mkuu wa WHO Dkt. Tedros Ghebreyesus, ametuma salamu za rambirambi kufuatia kifo cha kijana huyo.
Kupitia ukurasa wa taasisi ya Youth Combating NTD’s, wameeleza pia kusikitishwa na taarifa juu ya kifo hicho.
Wamemtaja kwamba alikuwa kinara katika kupambana dhidi ya magonjwa hayo, miongoni mwa waliokuwa mstari wa mbele hususan katika kampeni mbalimbali.
Mkuu wa Wilaya ya Mtwara, Dunstan Kyobya ambako marehemu alikuwa akifanya kazi kwa kujitolea, amesema...“Godwin alikuwa anasoma Ufamasia katika Chuo Kikuu cha
Zambia… alipata ajali Desemba 5, mwaka huu akitokea Njombe kuelekea Songea,”
amesema.
Chapisha Maoni