Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement


Na Veronica Mrema

Chumba cha siri cha Chief wa Kabila la Wahehe, Mkwavinyika Munyigumba Mwamuyinga maarufu Mtwa Mkwawa inahitaji ujasiri na kujiamini kiwango cha hali ya juu kuingia.

Historia ya kipekee yenye mvuto wa aina yake inapatikana ndani ya Tanzania pekee, katika mapango yaliyoumbwa na kujiunda kwa mtindo wa kuvutia na wa aina yake.

Katika eneo hilo kuna mabaki ya vitu kadhaa alivyowahi kutumia Mtwa Mkwawa ikiwamo vyungu, friji ya asili, jiwe alilosugulia miguu yake, mafiga alipokuwa akipikiwa chakula chake.

Kuna kijito cha maji ya baraka ambayo aliwahi kuyanywa na kupona ugonjwa uliomsumbua muda mrefu akitibiwa bila mafanikio kwa dawa mbalimbali na tabibu wake.

Mapango hayo yapo pembezoni kidogo mwa Maporomoko ya Kimani eneo la Mpanga Kipengere, Mkoani Njombe, ndiko kilipo chumba hicho. Lipo pia bwawa lake la kuogelea kwenye maporomoko.

Kituo cha radio Highland Fm kwa kampeni yake ya ‘Kikwetukwetu’, imefanikiwa kwa ushirikiano na wadau wake ambao wengi ni wasikilizaji wake, kufanya utalii wa ndani ndani ya eneo hilo lililobeba historia ya Mtwa Mkwawa enzi za uhai wake.

Akizungumza Kaimu Mkurugenzi wa Jiji la Mbeya Triphonia Kisiga amesema eneo hilo lina mvuto wa kipekee usiopatikana kwengineko duniani.

 “Highland Fm wametushangaza, tumefurahia kwa kiwango ambacho waswahili wanasema kiwango cha lami, tumeona vitu vingi,” amesema.

Ameongeza “Tumefurahia zaidi tulipoenda kwenye maji, chumbani cha siri cha Chief Mkwawa alipokuwa anafanya mambo yake.

“Tulivyoingia mule kwa kweli tumefurahia sana, kilichonifurahisha zaidi namna ya kuingia kwenye chumba cha siri, wale tulioingia mmeona.

“Kama haupo ‘strong’ huwezi kuingia kwenye kile chumba cha siri, Kile chumba cha siri kwa kweli tumefurahia sana, ningetamani na wenzetu wangefika kile chumba.

Amesema wamefurahia kuona mimea mbalimbali ukiwamo wenye uwezo wa kurudisha mahusiano ya wanandoa yaliyotetereka.

“Kuna watu wameogelea hadi katika Bwawa la Mapenzi, kila mtu amefurahia sana, tumeona mandhari nzuri ukiwa kule Mbeya huwezi kuona mandhari nzuri kama hii.

Amehimiza Highland Fm kuendelea kuandaa ziara nyingine za utalii wa ndani na utamaduni ili kuzidi kuitangaza historia nzuri ya Tanzania ambayo haipatikani kwengineko duniani.

Akimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Afisa Utamaduni wa Mkoa huo, Victoria Shao ameongeza “Kama mkoa tumeshangazwa, hongereni {Highland Fm} mmeweza kutufurahisha wote tuliofika hapa.

“Niwaombe tuendelee na utalii huu, kwa sababu unakusanya watu wengi tuendelee kuenzi masuala ya utamaduni, wakati tunapewa historia mtaweza kuona masuala ya utalii na utamaduni ni mambo yanayoenda sambamba.

“Kuna utamaduni unaoshikika na ule usioshikika, wa kushikika ni kama ngoma, vyakula, mimea lakini kuna masuala ya imani haya ni utamaduni usioshikika, tumeambiwa kuna maji ya baraka ukinenea chochote unafanikiwa.

“Tumeona vyungu, kitanda, mafiga yale kwamba historia bado inatunzwa, niwaombe isiwe mwisho tuhakikishe tunaendelea na 'tour' hizi na kuandaa matamasha.

Amesisitiza “Tuone namna gani tunaendelea kutoa elimu kwa jamii, tumeona kuna mmomonyoko wa maadili, tutumie hizi ‘tour na matamasha kuhimiza watu kurudi kwenye tamaduni, mila na destuiri zetu.

“Hata kama tunaiga tusiige yenye madhara, tumeoneshwa kwenye vyakula vipo hadi vya mama mjamzito, tuwe mabalozi tuendelee kutoa elimu na kuhimiza mila na desturi zetu.

Pamoja na hayo, amesema Mkuu wa Mkoa huo, anapenda masuala ya utalii na anahimiza wadau kuendelea kuhimiza masuala ya utalii.

Amesema mkoa huo pia utaendelea kuhimiza utunzaji wa mazingira ili kuzidi kutunza na kulinda vyanzo vya maji kwa upandaji miti katika vyanzo vyake na maeneo mengine mbalimbali.

Mkurugenzi wa Highland Fm Eveline Mwakyambiki amewashukuru wadau wote walioungana na kituo hicho na kuahidi kuyatekeleza maelekezo yaliyotolewa na viongozi hao.

1 Maoni

  1. Hakika kuingia kwenye Chumba cha Siri cha Mtwa Mkwawa yahitaji ujasiri.

    JibuFuta

Chapisha Maoni

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement