Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement

Bidhaa za dawa, vifaa tiba na vitendanishi vilivyokamatwa katika oparesheni maalum ya TMDA

Na Veronica Mrema

Oparesheni maalum iliyofanyika Novemba 20 hadi 24, 2023 imeibua mikoa minne vinara wa uchepushaji dawa, vifaa tiba na vitendanishi vya Serikali ni Dar es Salaam, Lindi, Ruvuma na Simiyu.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba [TMDA] Adam Fimbo amebainisha hayo leo katika mkutano wake na waandishi wa habari alipotoa ripoti kuhusu oparesheni hiyo.

Ilihusisha kukamata dawa, vifaa tiba na vitendanishi vya Serikali, dawa bandia, duni, zisizo na usajili na pamoja na dawa za kulevya.

“Hii ndiyo mikoa vinara ambako dawa za Serikali zilichepushwa na tunaendelea kufanya upelelezi kwa wale ambao tuliwakuta nazo,” amesema.

Ameongeza “Kwa sababu  tukikuta kwenye maduka ya dawa binafsi ameletewa, kikubwa unarudi nyuma kuangalia mtandao mzima atusaidie kutuambia aliyeleta ni nani?.

“… na huyo aliyeleta amezipata wapi? Mpaka tujue mnyororo mzima, turudi kwenye chanzo nani amefanya hivyo.

“Kwa sababu dawa zikitoka MSD [Bohari ya Dawa] zinaenda hospitali kwenye utaratibu wa Serikali, tukirudi nyuma tutajua wanaohusika kina nani?.

“Wote hao tunawafuatilia, tuwapate wote,” amesisitiza. Oparesheni hiyo ya TMDA ilihusisha pia Ofisi ya Rais TAMISEMI, Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya [DCEA], Baraza la Famasi na Jeshi la Polisi.

Fimbo amesema walikamata dawa zilizokuwa na maandishi maalum ‘For GOV-TZ-NOT FOR SALE’ na nyingine zikiwa na nembo ya MSD.

Amebainisha katika oparesheni hiyo jumla ya bidhaa zenye thamani ya Tsh. Mil. 172 zilikamatwa na walibaini wachepushaji walikuwa wakifuta nembo za Serikali ili zisigundulike.

“Maboksi mengi yamefutwa maandishi yalisomeka GOT hizi wamezitoa kwenye mnyororo wa Serikali, zinauzwa maduka binafsi na nyingine tumezikuta zina nembo ya MSD,” amesema.

Amesema katika oparesheni hiyo pia wamekamata dawa bandia za mifugo, dawa na vifaa tiba duni, zilizoisha muda wa matumizi na visivyo na usajili au kutambuliwa na TMDA, zimekutwa zikiuzwa mtaani.

Amesema pia wamekuta dawa za TB zikiuzwa nje ya mfumo wakati haziruhusiwi kuuzwa, dawa za uzazi na zingine za kutibu fangasi na zile za oparesheni zinazotumika kwa nusu kaputi nazo zimekamatwa.

“Tumekamata dawa duni [zenye ubora hafifu], bandeji ambazo ukibandika hazishiki, gozi ambazo zinapukutika tu.

Amesema walikagua majengo 777 ya sehemu za biashara na kubaini 200 [25.7%] kati yake yalikuwa hayana usajili/ hayatambuliki kabisa.

“125 [16.1] yalikutwa na bidhaa zilizokwisha muda wa matumizi, 84 [10.8] hayakuwa na vibali vya biashara, 67 [8.6] hayakuwa na mtaalam, 66 [8.5] hayakuwa na nyaraka za manunuzi.

“64 [8.2] ambayo ni DLDM yalikutwa na dawa zilizoruhusiwa kuwepo katika DLDM, 36 [4.6] yalikutwa na dawa za Serikali, 20 [2.6] yalikutwa na bidhaa duni.

“5 [0.6] yalikutwa yanatoa huduma za kitabibu na 3 [0.4] yalikutwa na bidhaa bandia,” amebainisha.

Ameongeza “Kufuatia matokeo haya watuhumiwa wote waliokutwa na kuhusika moja kwa moja na kusambaza au kuuza dawa, vifaa tiba au vitendanishi vya Serikali na bandia wamefikishwa katika  vyombo vya Sheria.

“Jumla ya majalada 13 yamefunguliwa dhidi yao na taratibu za kuwafikisha mahakamani zinaendelea katika vituo vya Polisi, jumla ya faini Tsh. Mil. 100.8 zimetozwa .

Amesema bidhaa zote bandia, zisizo na usajili na zilizokwisha muda wa matumizi zimeondolewa sokoni kulinda afya ya jamii.

Msajili wa Baraza la Famasia Elizabeth Shekalaghe amesema wamekamata wauzaji wa dawa katika famasi na maduka ya dawa za binadamu na mifugo ambao hawana utaalamu.

“Kumekuwa na dhana potofu wananchi wengi wakidhani biashara ya dawa ni nyepesi kufanya kwa lengo la kujipatia kipato,” amesema.

Ameongeza “Dawa hizi zilizokamatwa inawezekana katika maeneo mengine ambayo hatujafika zipo, nitoe wito kwa wataalamu wote wa dawa tutumie weledi kufanya kazi zetu.

“Kwa waliobainika, taarifa itaebdelea kufanyiwa kazi na iwapo kuna mwana-taaluma wa famasi amejihusisha na uuzaji dawa za Serikali, duni, bandia hatua za ki-Sheria zitachukuliwa ikiwamo kufutiwa leseni.

Amesema kuna tabia pia ya baadhi ya wamiliki wa maduka kununua dawa mikononi na kuwataka waache mara moja.

“Natoa wito kwa wananchi kutupatia taarifa, kila mtu anatakiwa kuhakikisha analinda afya ya mwingine,” amesema.

Amesema kwa kipindi cha miaka mitatu wamekamata watoa dawa 3,000 ambao waliuza bila kuwa na sifa.

Kamishna wa Polisi, Daniel Nyambabe amesema tayari majalada 13 yamefunguliwa tayari kushughulikia kesi hizo za uuzaji dawa za Serikali, bandia, duni na zenye asili ya kulevya kinyume cha Sheria.

“Yapo hatua za upelelezi chini ya Ofisi ya Mkuu wa Mashtaka [DPP],” amebainisha.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement