Na Veronica Mrema
Dawa, vifaa tiba na vitendanishi vyenye nembo maalum ‘For GOV-TZ- NOT FOR SALE’ vimeibwa na kupelekwa kutumika, vituo binafsi vya kutolea huduma za afya na kuuzwa, maduka binafsi ya
dawa.
Bidhaa za dawa, vifaa tiba na vitendanishi vilivyoisha muda wa matumizi navyo vimekutwa vikiuzwa jambo ambalo ni kinyume na Sheria za
Nchi.
Dawa duni pamoja na vifaa tiba duni na vingine visivyo na
usajili/visivyotambuliwa na Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba Tanzania [TMDA] navyo
vimekutwa ndani ya soko.
Bidhaa zote hizo zimekamatwa katika oparesheni maalum ya
kukamata dawa, vifaa tiba na vitendanishi vya Serikali, bandia, duni, zisizo na
usajili na dawa za kulevya kipindi cha Novemba 20 hadi 24, 2023.
Oparesheni hiyo maalum imefanywa na TMDA ikishirikiana na Ofisi ya
Rais TAMISEMI, Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya [DCEA], Baraza
la Famasi na Jeshi la Polisi.
Ililenga kufanya ukaguzi na msako mkali wa bidhaa za afya
kwenye hospitali, vituo vya afya, zahanati, maghala, maduka ya jumla na
rejareja ya watu binafsi na maeneo mengine yasiyo rasmi.
“Dawa za Serikali zilikamatwa katika vituo binafsi vya
kutolea huduma za afya ni pamoja na dawa mseto ya kutibu malaria ya vidonge
aina ya ALU.
“Dawa mseto ya kutibu Kifua Kikuu yenye viambata hai vya Rifampicin
and Isoniazid, Phenoxymethyl Penicilin na dawa za uzazi wa mpango
[Medroprohesterone Acetate Injection],” ametaja Mkurugenzi Mkuu wa TMDA Adam.
Katika mkutano na waandishi wa habari, Fimbo ametaja
nyingine ni “Capsuli za Fluconazole na Lignocaine Injection, dawa hizi
zilikutwa Dar es Salaam, Lindi, Ruvuma na Simiyu.
Amesema vifaa tiba vya Serikali vinavyokadiriwa kuwa na
thamani ya Tsh. 11,297,500 vilikamatwa katika vituo na maduka binafsi.
“Baadhi ya vifaa tiba hivyo ni IV Cannula G21, G20, G22,
Bioline Malaria Ag, Bioline HIV ½ 3.0z, Hemocue Glucose 201, Microcuvettes na
Hemocue Hb2021 na Analyser, vilikutwa Kanda ya Mashariki na Kanda ya Kati.
Amesema dawa zilizokwisha muda wa matumizi zenye thamani ya
Tsh. 9,512,965 zilikamatwa zikiwa hazijatengwa kwa mujibu wa utaratibu.
“Sehemu kubwa ya dawa hizi zilikamatwa Kanda ya Kati, Kanda
ya Ziwa, Mashariki na Nyanda za Juu Kusini,” amesema na kuongeza,
“Vifaa tiba vilivyokwisha muda wa matumizi vyenye thamani
inayokadiriwa Tsh. 10,313,960 vilikamatwa pia vikiwa havijatengwa kwa mujibu wa
utaratibu.
“Sehemu kubwa ya vifaa tiba hivi vilikamatwa Kanda ya
Mashariki, Kanda ya Ziwa Mashariki na Nyanda za juu Kusini.
Kwa mujibu wa Fimbo, dawa bandia zenye thamani ya Tsh.
5,889,000 zilikamatwa Kanda ya Kaskazini, Nyanda za Juu Kusini na Kanda ya
Magharibi.
“Kanda ya Nyanda za Juu Kusini ndiyo inayoongoza ikifuatiwa
na Kanda ya Magharibi, dawa zote bandia zilizokamatwa zilikuwa za mifugo,”
amesema.
Ametaja dawa hizo “Ni Bupanor Injection, Homidium Chloride
250mg BP, Homidium Chloride 250mg, Ethidium Bromide, Samocare [Isometamidium
Chloride Hydrocloride 1g].
“Nyingine ni Bromidium na Veridum 1g [Isometamedium Chloride
Hydrochloride],” amebainisha.
Amesema dawa zenye ubora duni zenye thamani ya Tsh. 579,600 zilikamatwa Kanda ya Kaskazini, Kanda ya Mashariki na Kanda ya Kati.
“Sehemu kubwa ya uduni wa dawa ulibainika kusababishwa na
dawa husika kutokutuzwa kwa kuzingatia maelekezo ya mtengenezaji.
“Dawa duni zilizobainika ni pamoja na U-sol [Chlorinated Lime and Boric Acid], dawa za mifugo aina ya Bamisole 10% [Levamisole Injection] ambayo ilikutwa imebadilika rangi kutoka njano na kuwa nyeupe kama maji na Ibufen 200 [Ibuprofen].
Amesema vifaa tiba na vitendanishi duni vyenye thamani ya Tsh. 5,367,000 vilikamatwa Kanda ya Ziwa Mashariki na Kanda ya Mashariki.
"Ni pamoja na Stesthoscope za aina mbalimbali, Sphygmogram meter, Labouratory reagents, Immersion Oil for Microscopy, Sample Collection Tips, Wooden Applicators.
"Clinical Thermometer, Tongue Depressors, Thermohyglometer na Delivery Kits," amebainisha.
Amesema dawa ambazo hazijasajiliwa na kutambuliwa zenye thamani ya Tsh, 133,302,816 nazo zimekamatwa katika Kanda saba, kwa wingi Kanda ya Mashariki na Kanda ya Nyanda za Juu Kusini.
"Vifaa tiba na vitendanishi ambavyo havijasajiliwa na kutambuliwa vyenye thamani ya Tsh. 17,699,950 vilikamatwa kanda zote sabam hususan ya Mashariki na Kaskazini.
"Dawa zenye madhara ya kulevya aina ya Pethidine nazo zimekamatwa zikiuzwa kwa siri, mtandao wote umebainika na wahusika kufahamika," amesema.
Chapisha Maoni