Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement


Na Veronica Mrema - Dodoma

Huba alilokuwa nalo na mwenza wake, mahaba mazito waliyokuwa wakipeana, hakuwahi kufikiri hata siku moja, atamuingiza kwenye janga zito la matumizi ya dawa za kulevya.

Ni mwenyeji wa Morogoro, Fatuma James amelazimika kusafiri umbali mrefu na kuhamishia makazi hapa Dodoma akifuata tiba ya Methadone baada ya kuathiriwa na heroin.

“Wanaume..., hawala wangu ndiye alikuwa ananivutisha dawa za kulevya [lakini] mara ya kwanza aliniambia bangi tu, vuta mke wangu,” anasimulia.

Anasema jambo lililokuwa likishangaza ni pale alipokuwa akivuta bangi zingine hakuwa anapata hisia zile alizokuwa akizipata baada ya kuvuta bangi ya mpenzi wake huyo.

“Nilikuwa najiuliza hii bangi gani? Mbona nahisi alosto, akinivutisha ile yake najisikia vizuri, nikivuta bangi yangu maumivu yanaongezeka, nilikuwa najiuliza hii ni nini?,” anasema.

Anasema siku moja alimkuta mpenzi wake akisaga kitu kwenye jiwe, “Nilimkuta anasaga, nilimuuliza hii ndiyo bangi gani?, alinijibu kwani ulikuwa hujui hii ndiyo dawa ya kulevya.

‘PENZI LA UPOFU’

Anasema alihamaki na kujikuta akimuuliza mpenzi wake huyo… “Eh! Hivi wewe kaka ni mgonjwa wa akili?, kwanini unaniingiza kwenye hili? [naye] Akaniambia si ulinipenda?.

“.., na kweli yule kaka nilimpenda, alichokuwa ananiambia chochote, mimi nakubali ndiyo hapo aliingiza kwenye dawa za kulevya na mimi nikaujua ‘unga’.

Anaongeza “Niliishiwa nguvu, nilianza kulia, nilimuambia kwanini unaniingiza kwenye janga hilo.

“Nilikuwa sijui anayetumia dawa za kulevya yupoje, sijui hata nikutane naye niambiwe mteja nilikuwa sijui.

“Hadi nilivyotumia ndiyo nilijua aha kumbe ndiyo wanavyodhalilishwa hivi?,” anasema, tangu hapo maisha yake yalibadilika mno.

“Mwanangu roho ilikuwa inamuuma, alikuwa ananiambia shuleni wenzake walikuwa wanamcheka kweli mama yake anatumia ‘ma-unga’, analia.

‘KOVU LA MOYO’

Anaongeza “Nilishajutia mapenzi na nilisema sitakuja kupenda, nitakaa tu na mwanaume, basi kwa sababu mimi ni mwanamke, lakini huko kupenda hapana.

“Nimevuta unga bado mdogo sana, miaka 14, nyumbani sishikiki, yule jamaa kila akinitafuta. Shule niliishia darasa la nne, hata kusoma sijui, ndiyo uhuni au matatizo sijui.

“Nikaanza kutoka ‘road’ namtoroka… kwa sababu yeye akichelewa tu, naenda ‘road’ … natafuta fedha na mimi naenda kwa ‘mzungu’, nilishapajua.

Je kwenda ‘road’ maana yake nini? Fatuma anabainisha “Sisi wanawake ni kujiuza tu dada yangu, unaenda unajiuza.

“Ndiyo unapata hiyo hela, mwingine kuiba hawezi umeshazoea kujiuza, ndiyo hivyo unaenda kujiuza unapata hela.

“Unakuta li-baba lingine hujui lina Ukimwi, hujui lina nini.., likikuambia mimi nina 20,000 hii hapa, halafu na una ‘alosto’ ili ukidhi mahitaji yako utakubali tu.

Anaongeza “‘Alosto’ imeshaisha ndiyo unajuta, dah! Hivi mimi… yule m-baba kweli nimelala naye bila kondom?!.

“Yaani baadae ndiyo unaanza kujutia, ‘alosto’ hapo imeshaisha, tena ikianza wewe mwenyewe utaenda tu ‘road’.

MAJUTO NI MENGI

Fatuma anazikumbuka siku zake za kwanza kabla hajatumbukia kwenye janga hilo, anasema kabla ya mahusiano na mpenzi wake huyo alikuwa msusi mzuri mno.

“Dada yangu ndiye aliukuwa ananifundisha tulikuwa wote saluni, nilikuwa na chumba, godoro na kila kitu ndani.

“Ila nilipoanza kuvuta tu kila kitu niliuza ndani, hadi nguo za mwanangu niliiba na kuziuza, hadi mama yangu nilishamuibia sana.

“Nina mtoto mmoja na kijana mwengine naye [ni muathirika wa dawa za kulevya] nakunywa naye dawa hapa [Hospitali ya Taifa ya Afya ya Akili – Mirembe].

Anasema mwanamke anayetumia dawa za kulevya anadharaulika sana ndani ya jamii, jambo ambalo huwaumiza ‘moyo’ waraibu wengi.

“Wanasema lile si liteja tu, yaani ukipita mtaani, tu hadi mwenyewe unaona aibu. Sasa utafanyaje, umeshatumia dawa, wakisema linapitia huku linatokea huku.

“Utafanyaje?, kwa sababu umeshaingia kwenye lile janga, kwa sababu wenyewe hawajui wewe ndiye unayejua yale maumivu, nimeshaenda sana jela, nimeshakaa sana.

Je amepelekwa jela mara ngapi? Anabainisha “Mara tatu nimeenda kwa kesi za wizi, mara unaenda kulala na li-mwanaume unaliibia linakupeleka jela.

“Mama yangu, nilimuibia vitu vya ndani akanipeleka jela, alijua mwanangu ataacha unga lakini ni vile vile.

Anaongeza “Nia ile sikuwa nayo … kuacha dawa za kulevya, ila nilivyokuja kweny methadone naishukuru sana, ni mwaka wa pili sasa.

Anasema kwa kuwa Morogoro [kipindi hicho] hakukuwa na kliniki ya tiba ya methadone ndiyo maana aliamua kuhamia Dodoma kufuata tiba hiyo.

“Nakaa hapa hapa nimepanga chumba changu, nimefungua biashara yangu, nauza chai, uji, [lakini] kabla ya yote haya nilitamani niwe mtu mkubwa tu.

“Niwe na hela na heshima kubwa kwa jamii, kwenye ususi inategemea na mtindo niliweza kupata Tsh. 10,000 hadi 30,000, inategemea na mtu anavyokuja” anasema.

FUATILIENI NYENDO

Fatuma ni miongoni mwa wanawake 12 ambao wamejitokeza kupata tiba ya methadone kati ya waraibu 500 waliosajidiwa Mirembe.

“Sasa[wana-jamii] wanatukubali zamani walituita mteja sasa wanasema hatuna ‘neno’ [ni watu wema] tunatumia dawa,” anasema na kueleza jinsi alivyopata mtaji wake wa kuanzisha biashara.

“Nilimsiuka mtu yeboyebo alinilipa 15, 000 nikaanza kuuza chai, uji nikimaliza nakuja kwenye dawa. Hapa kliniki pia ni mnufaika wa mafunzo ya kilimo cha mbogamboga na nyanya.

Fatuma anashauri jamii hususan wazazi na walezi kuwa karibu na watoto na kuhakikisha wanafuatilia nyendo zao hatua kwa hatua kwani sasa ni kundi linalonyemelewa na ‘mapapa wa unga’.

Anawashauri pia vijana wale ambao hawajawahi kujihusisha na biashara na matumizi ya dawa hizo wasithubutu kabisa kwani ni janga lenye mateso mengi.

“Nawaambia majanga haya si mazuri, dawa za kulevya si nzuri waepuke kukaa kwenye vijiwe, marafiki waepuke waangalie wenye muelekeo, si wote wazuri

Anaongeza “Wapo wengine hawapendi maendeleo yako, sasa wanaopotea sana ni wenye hela. Ipo mara nyingi kwa sababu fulani ameathirika naye aje huku.

“Unaona tu yule nitamkomesha sisi msemo wetu adui yako usimuombee njaa muombee aingie kwenye unga. Mimi sijafanikiwa ila wapo wanaoingiza watu huku kwa sababu hiyo.

“Wazazi wawazingatie watoto wao, wawashikilie sana, hili janga bay asana, si umezaa ua uchungu mzingatie mwanao fuatilia nyendo zake asiingie pabaya. Sasa hivi watoto wanafuatiliwa sana.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement