Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement


Na Veronica Mrema  - Dodoma

Si kila aliye karibu nawe ana mapenzi ya dhati na anapenda maendeleo yako, wapo wanaoficha ukweli usoni mwaokwamba moyoni wanakuwazia mabaya na wanataka kukuangusha.

Fatuma James mmoja wa waraibu wanaotibiwa kwa methadone, Hospitali ya Taifa ya Afya ya Akili Mirembe – Dodoma, amesema katika mahojiano maalum na MATUKIO NA MAISHA BLOG.

Akiangua kilio, amesimulia alivyoanza kujihusisha kimapenzi akiwa na miaka 14 na mwanaume mmoja ambaye ndiye aliyemuingiza katika janga la matumizi ya ‘unga’ na kuishia darasa la nne.

Amesema mpenzi wake alimuingiza huko pasipo ridhaa yake na kusisitiza wazazi na walezi kufuatilia kwa ukaribu nyendo za watoto wao.

Amesema mwanaume aliyekuwa naye alianza kumshawishi kuvuta bangi aliyokuwa akiivuta yeye, hakumuambia imechanganywa na ‘unga’ aina ya heroin.

“Nawaambia majanga haya si mazuri, dawa za kulevya si nzuri waepuke kukaa kwenye vijiwe, marafiki waepuke waangalie wenye muelekeo, si wote wazuri,” ameshauri vijana.

Ameongeza “Wapo wengine hawapendi maendeleo yako, sasa wanaopotea sana ni wenye hela. Ipo mara nyingi kwa sababu fulani ameathirika naye aje huku,” amesema na kubainisha,

Baadhi ya watu walioathiriwa na ‘unga’ hutamani kuona wenzao ambao hawajaathirika nao wanaingia kwenye janga hilo.

“[Husema]  yule nitamkomesha sisi msemo wetu adui yako usimuombee njaa muombee aingie kwenye unga.

“Mimi sijafanikiwa [kuingiza maadui kwenye janga hili] ila wapo wanaoingiza watu huku kwa sababu hiyo.

“Wazazi wawazingatie watoto wao, wawashikilie sana, hili janga baya sana, si umezaa kwa uchungu mzingatie mwanao fuatilia nyendo zake asiingie pabaya, sasa hivi watoto wanafuatiliwa sana.

Hivi karibuni Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya [DCEA] ilitangaza kwa Umma namna ilivyoweza kubaini mtambo wa kutengeneza biskuti za bangi.

DCEA ilibaini na kumata pia bidhaa zilizozalishwa na kuchanganywa na bangi ikiwamo tomato sauce na juisi.

Kamishna Jenerali wa DCEA Aretas Lyimo alihimiza wazazi na walezi pia kuwa karibu na kufuatilia watoto wao kwani mtandao huo sasa unalenga watoto, kuwaingiza kwenye janga hilo.

Fatuma amesimulia mengi kuhusu maisha yake na namna anavyopambana kuacha matumizi ya dawa za kulevya, makala hayo tutakuletea hapa hapa MATUKIO NA MAISHA BLOG jumanne.

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement