Na Veronica Mrema
Sekta ya afya imedhamiria kugusa zaidi jamii katika ngazi ya msingi ambapo Wizara imeteua vipaumbele vinane mahususi vya utekelezwaji katika mwaka 2024.
Waziri wa Afya Ummy Mwalimu amebainisha vipaumbele hivyo mbele ya waandishi wa habari Dar es Salaam.
Ametaja kipaumbele cha kwanza ni
kuimarisha afua za Kinga ili kuwezesha wananchi kujikinga na magonjwa na pia
kuwezesha utambuzi wa mapema wa magonjwa
Amebainisha kipaumbele hiki
kitaangazia “Kuimarisha huduma za chanjo na Lishe hususani kwa watoto wa umri
chini ya miaka 5.
Ametaja pia Wizara itaanzisha huduma za watumishi wa afya ngazi ya jamii [CHW’s].
Amesema itaendelea kutoa elimu kwa umma kujikinga na magonjwa ya kuambukiza na magonjwa yasiyo ambukiza (MYA).
“Kwa upande wa MYA tutahimiza wananchi kubadili mtindo wa Maisha ikiwemo kuzingatia ulaji unaofaa wa vyakula, kufanya mazoezi nk,” amesema.
Ametaja kipaumbele cha pili ni kuendelea kuimarisha ubora wa huduma katika vituo vya umma vya kutolea huduma za afya katika ngazi zote.
“Ikiwemo zahanati, vituo vya afya, hospitali za wilaya/halmashauri, hospitali za rufaa za mikoa, hospitali za kanda na Hospitali ya Taifa kwa kufanya yafuatayo,
“Kuendelea kuwekeza kwenye Miundombinu ya kutolea huduma ikiwemo kukamilisha na kukarabati miradi ya ujenzi na kufanya matengenezo kinga kwa wakati.
“Kuhakikisha upatikanaji wa
dawa, vifaa na vifaa tiba hususani kwa ajili ya huduma za afya ya uzazi, mama
na mtoto,” amesema.
Ametaja jambo jingine ni “Kuimarisha
usimamizi wa utoaji huduma za afya katika ngazi ya vituo/hospitali, kata, halmashauri
na mikoa.
“Kuimarisha mifumo ya TEHAMA ili
kuwapunguzia wateja muda wa kusubiria huduma na kuimaisha mawasiliano kati ya kituo
kimoja na kingine katika mnyororo wa rufaa.
Ametaja kipaumbele cha tatu ni kuongeza
idadi ya watumishi wa afya katika ngazi zote sambamba na kuwajengea uwezo
watumishi wa afya walio kazini.
“Kwa kuwapeleka madaktari bingwa
walioko hospitali za rufaa za mikoa katika vituo vya afya na hospitali za
wilaya kutoa mafunzo kwa vitendo [mentorship].
“.., kuhusu kutoa huduma bora za
afya kwa wajawazito na watoto. kupitia utekelezaji wa kampeni ya madaktari
bingwa [Madaktari Bingwa wa Mama Samia] hadi katika ngazi ya afya ya msingi.
Waziri Ummy ametaja kipaumbele
cha tatu ni kutekeleza Sheria ya Bima ya Afya kwa wote ili kuwawezesha wananchi
wengi kupata huduma za afya bila ya kikwazo cha fedha.
“Kukamilisha Mwongozo wa gharama
wa utoaji huduma za afya kwenye vituo vya kutolea huduma za afya za umma ili
kuwa na uwiano sawa wa bei za utoaji wa huduma,” ni kipaumbele kingine.
Ametaja kingine ni “Kuimarisha
tija na kupunguza malalamiko yanayohusu matibabu ya makundi maalum ya wagonjwa
wanaostahili msamaha wa matibabu.
“Watoto walio na umri chini ya
miaka mitano, Wajawazito na Wazee wasio na uwezo.
Waziri Ummy amebainisha vipaumbele vingine ni kuongeza uwezo wa ndani wa kuzalisha vifaa, vifaa tiba na dawa na kuimarisha usimamizi wa weledi na maadili kwa wataalamu wa afya.
Awali amebainisha changamoto sita ambazo sekta ya afya ilikumbana nazo katika mwaka 2023 Tanzania, ni pamoja na upungufu wa watumishi katika sekta ya afya.
"Changamoto ya ubora wa huduma kwa baadhi ya maeneo ya utoaji wa huduma za afya kutokana na usimamizi usioridhisha kwa baadhi ya watumishi.
"Mwitikio mdogo wa Wananchi kujiunga na Mifuko wa bima ya Afya. Hivyo kushindwa kugharamia huduma mbalimbali wanazozihitaji.
Ameongeza "Kuongezeka kwa magonjwa yasiyo ya kuambukiza (NCDs) mfano ugonjwa wa kisukari sasa upo ndani ya magonjwa 10 ya OPD.
"Sekta ya afya ni jambo kubwa, pana na 'dynamic' [linalobadilika] mara kwa mara kutokana na sababu mbalimbali.
"Ikiwemo, ongezeko la idadi ya watu, ongezeko la magonjwa, mabadiliko ya tabia nchi, mabadiliko ya teknolojia ya tiba na uwepo wa uwazi katika utoaji huduma.
Amesema kuibuka kwa magonjwa ya Watoto yanayozuilika kwa chanjo kama vile surua, polio, tetekuwanga, hali ambayo ilisababishwa na watoto wengi kutokupata chanjo kwa wakati.
"Mfano mwaka 2023 kulitolewa taarifa ya ugonjwa wa Polio kwa mtoto katika Manispaa ya Mpanda ambapo kwa kipindi kirefu ugojwa huu ulikuwa umedhibitiwa hapa nchini," amebainisha.
Chapisha Maoni