Recent Post


 


moja

Responsive Advertisement


Na Veronica Mrema

Ulemavu wa kudumu atabaki nao maisha yake mwanamke mwenye busha nchini, hii ni kwa sababu hadi sasa bado hakuna teknolojia inayotumika Tanzania kwa upasuaji wa kuliondoa.

Hii ni tofauti na wanaume ambao ipo teknolojia ya kuwasaidia kufanya upasuaji na kuondoa busha.

Kwa wanawake ambao wamepata tatizo hili hali ni ngumu kwao kwani hali hiyo huwasababishia changamoto ndani ya mahusiano na ndoa zao.

Lakini pia imekuwa ngumu kwa wanawake wenye busha kujitokeza kutafuta tiba kwa kuhofia unyanyapaa watakaofanyiwa ndani ya jamii zao.

“Ugonjwa wa matende na mabusha unaenezwa na mbu aina zote na unaathiri watu wote ambao wanaishi kwenye maeneo ambayo yana maambukizi,” anasema Dkt. Clara Mwansasu.

Ni Afisa kutoka Mpango wa Taifa wa Kudhibiti Magonjwa Yaliyokuwa Hayapewi Kipaumbele [NTDCP] ulio chini ya Wizara ya Afya Tanzania.

Matende na mabusha si ugonjwa unaosababisha vifo moja kwa moja lakini madhara yake ni makubwa kwani husababisha ulemavu wa kudumu.

Dkt. Clara anaongeza “Unaposababisha ulemavu wa kudumu maana yake huyu mtu anaingia kwenye umaskini.

“Kwa sababu anakuwa hawezi tena kuzalisha mali kutokana na madhara anayoyapata. Ni ugonjwa unaosababishwa na minyoo midogo midogo ambayo inaathiri mfumo wa maji damu.

Anafafanya zaidi, “Ukishaathiri unapelekea maji kutokurudi kwenye mfumo wake wa kawaida hivyo kujaa kwenye sehemu za miguu na sehemu za siri.

“Wanaume kwa wanawake wote wapo kwenye uhatarishi sawia kwa sababu kwa wanawake akipata maambukizi anaweza kupata tende likaathiri titi au sehemu za siri.

“Anaweza kupata tende kwenye miguu au mkono, inategemea vile vimelea vimejikita zaidi sehemu gani,” anasema na kuongeza,

“Kwa wanaume kadhalika wanaweza kupata tende sehemu za miguu, mikono na wao pia wanaweza kupata madhara kwenye sehemu za siri na kupelekea ngirimaji au busha.

Anasema mtu anaweza kupata maambukizi ya ugonjwa huo katika umri mdogo ila madhara yake yakajitokeza baada ya miaka 10 au 15.

“Pale unapoanza kuzalisha uchumi athari zinajitokeza,” anasema.

Anasisitiza kutegemea na kiungo kilichoathirika, mathalani mtu akiathiriwa mguu au mkono hakuna namna yoyote ile ya kurekebisha uwe katika hali ya kawaida.

Mtu husika hupewa elimu jinsi ya kutunza tende alilopata ili asipate maambukizi na hii ni kwa wote wanaume na wanawake.

Anaongeza “Kwa wanawake ni tofauti wakipata sehemu za siri huwa hakuna namna ya kurekebisha,

“.., tofauti na wanaume wakipata busha huwa wanafanyiwa upasuaji kuondosha maji na anarudi kuwa kawaida.

“‘Advantage’ [kwa] mwanaume akipata sehemu za siri anafanyiwa upasuaji kurekebisha/kutoa busha kwenye mfuko wa korodani anarudi kawaida.

“Mwanamke akipata madhara inakuwa inampelekea ulemavu wa kudumu,” anasema.

Anaongeza “.., na wanawake wanapopata madhara haya mfano sehemu za siri mara nyingi huwa wanapata changamoto kwenye tendo la ndoa.

“[Ndoa] huvunjika na hupata unyanyapaa kwenye jamii, ni changamoto kwa kuwa hamna namna ya kurekebisha, ataishi na ulemavu huo wa kudumu.

Je wanawake wangapi hujitokeza kutafuta tiba? Anafafanua ni wanawake wachache mno hufika vituo vya huduma za afya kutafuta tiba.

“Hatuna suluhisho lakini pia bado wanaogopa kujitokeza kwa sababu ya unyanyapaa," anabainisha na kwamba huishi wakiwa na msongo wa mawazo.

Je, Wizara ya Afya inafanya nini kuokoa jamii yake,? Dkt. Clara anabainisha,

“Inatekeleza mpango/program ya kupambana na magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele ikiwa mojawapo ni matende na mabusha.

“Lakini afua tunayoitekeleza sasa ni umezeshaji wa dawa kinga kwenye jamii zilizoathirika.

Anasema ili tuitekeleze program hiyo Wizara ilifanya tathmini nchi nzima na kujua halmashauri 119 kati ya 184 zilizopo Tanzania Bara zilikuwa zimeathiriwa na matende na mabusha.

“Baada ya kuainisha ukubwa wa tatizo kwa nchi nzima hizo halmashauri zote ziliingia kwenye program ya kumezesha dawa mara moja kwa mwaka.

“Kwa mwongozo wa WHO dawa zinapaswa kumezeshwa angalau mara moja kwa miaka mitano mpaka sita na ukifikia walengwa wote ambao ni miaka mitano kwenye jamii,” anasema.

Anaongeza “Ukishafanya hivyo unafanya tathimini kuangalia ukubwa wa tatizo.

“Mwaka huu tumekuwa tukifanya na sasa hizo 199 zilizokuwa zimeathirika maambukizi yameshuka.

“Tumebaki na halmashauri saba ikiwamo Kinondoni, Lindi MC, Mtwara Mikindani, Mafia na Pangani, tunaenelea na umezeshaji dawakinga, wasipate maambukizi.

“Tunafanya ‘mass program’ [kampeni kubwa kwa jamii kubwa zaidi],” anabainisha.

Anaongeza “Wito wangu kwa wakina mama na jamii kwa ujumla maeneo ambako bado yana maambukizi wanajitokeza, tunaomba wajitokeze kwa wingi wapate dawa

“Ikizingatiwa madhara uya ugonjwa huu hujitokeza baada ya muda, wahimize pia watoto wafike dawa hizi ni salama hazina madhara yoyote.

“Wanaume pia washiriki kwa sababu pamoja tukiungana tunaweza kutokomeza magonjwa haya yaliyokuwa hayapewi kipaumbele,” ametoa rai.

Januari 30, 2024 Tanzania itaungana na nchi nyingine duniani kuadhimisha Siku ya Kupambana na Magonjwa Yaliyokuwa Hayapewi Kipaumbele [NTD's].

Kauli mbiu ya mwaka huu inasema 'Tuungane, Tuchukua Hatua kutokomeza Magonjwa Yaliyokuwa Hayapewi Kipaumbele'..

Post a Comment

saba

nane


 


sita

Responsive Advertisement