Na Veronica Mrema
'Nuru' inazidi kuangaza nchini Tanzania, ikiwa ni miaka ipatayo 20 sasa tangu iingie 'vitani' dhidi ya Magonjwa Yaliyokuwa Hayapewi Kipaumbele [NTD's], hatua kubwa imefikiwa kuyatokomeza.
Jamii ikiwa imewekwa mstari wa mbele ili kufikia hilo, pia ni lengo la dunia katika Malengo Endelevu [SDG's] ifikapo 2030 kila nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa [UN] kutokomeza NTD's.
Elimu sahihi imeendelea kupelekwa kwa jamii na umezeshaji dawakinga katika program za Mpango wa Taifa wa Kudhibiti Magonjwa yaliyokuwa Hayapewi Kipaumbele [NTDCP], Wizaya ya Afya.
Magonjwa ambayo Tanzania imeyaweka kipaumbele zaidi ni matano ikiwamo Matende na Mabusha, Usubi, Trakoma, Kichocho na Minyoo ya tumbo.
Afisa Program wa NTDCP Isaac Njau amesema hayo kwa niaba ya Meneja wa Mpango huo, katika semina ya siku moja kwa waandishi wa habari Dar es Salaam.
Semina hiyo ililenga kuwajengea uelewa wanahabari hao kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Magonjwa yaliyokuwa Hayapewi Kipaumbele Duniani inayotarajiwa kufanyika Januari 30, mwaka huu.
“Mwaka huu tumejipanga kuadhimisha Siku ya Magonjwa yaliyokuwa Hayapewi Kipaumbele, maadhimisho yatafanyika ngazi za mikoa na halmashauri.
“Kwa kutoa
elimu na hamasa juu ya magonjwa haya katika jamii, tuungane, tuchukue hatua
kutokomeza magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele,” amesema.
Ameongeza “Tunalenga
jamii ziwe na uelewa, taasisi mbalimbali na viongozi mbalimbali katika jamii
waungane ili tuweze kutokomeza haya magonjwa.
“Ni mikakati
yetu kwamba itakapofika 2030 sawa na malengo yale makubwa duniani [SDG’s].
“Sisi
Tanzania tumeazimia maazimio mengi ya kupambana na NTD’s tutakuwa tumepunguza
maambukizi mengi katika jamii,” amesema.
Dkt.
Clara Mwansasu kutoka NTDCP amesema Tanzania imekuwa ikitekeleza afua za
kutokomeza NTD’s baada ya kuwa imefanya tathmini ya kina.
“Tunatekeleza
afua za kutokomeza kwa mfumo wa kingatiba, matende na mabusha, usubi, kichocho,
minyoo ya tumbo na trakoma.
Ameongeza “Kabla
ya kuanza utekelezaji wa afua za kutokomeza ugonjwa huu, Wizara ilifanya
taythmini na kuainisha magonjwa haya yameambukizwa katika maeneo husika.
Amesema awali
kulikuwa na halmashauri 119 zilizoathiriwa na matende na mabusha kufikia 2023 zimesalia
halmashauri 7.
“Usubi kuliwa
na halmashauri 28 zenye ukanda wa milima zenye vyanzo vya maji ambavyo vina-support
mazalia ya nzi waenezao ugonjwa huu.
“Tumeendelea
kufanya tathmini na maambukizi yameshuka ila bado hatujatokomeza, kichocho na
minyoo ya tumbo halmashauri 184 hadi sasa tumefikia kushusha ukubwa wa tatizo.
“Lakini bado
tunaendelea kufanya afua za umezeshaji dawakinga kwa rika la shule, trakoma
halmashauri 77 zilikuwa na maambukizi 2023 tumeweza kushusha mambukizi zimesalia
9.
Amesisitiza “Tunapoelekea
kuadhimisha siku ya kupambana na NTD’s, tunaomba wananchi wanaoishi kwenye
mazingira yenye maambukizi washiriki kumeza ili tutokomeze.,
Amehimiza wananchi
pia kuendelea kushiriki katika utekelezaji wa afua nyinginezo ikiwamo usafi wa
mazingira na mwili.
“Ili ifike
mahala tuweze kutokomeza haya magonjwa na tuweze kuinua pato la Taifa,” ametoa
rai.
Chapisha Maoni