Na Veronica Mrema
Afya ni mtaji bora zaidi duniani, ni muhimu kuwekeza katika kuilinda na kuitunza afya yake kwa kuepuka mtindo mbovu wa maisha kwani kwa
kiwango kikubwa huchangia janga la magonjwa yasiyoambukiza [NCD's].
Rai hiyo imetolewa na Waziri wa Afya Ummy Mwalimu mapema leo punde baada
ya kuhitimika kwa matembezi ya hisani [Walk the Talk] yaliyoandaliwa na Shirika
la Afya Duniani [WHO Tanzania].
“Tutaendelea kuwekeza katika elimu ya afya kwa Umma, [kuhimiza jamii] ilinde
afya zao ili kuepuka magonjwa yasiyoambukiza…, kinga ni bora kuliko tiba,”
amesema na kuongeza,
“Tumeona wagonjwa wengi wenye Shinikizo la Juu la Damu na Kisukari.
“Kama kweli tunataka Afya zetu ziwe salama lazima kila mmoja aanze kuchukua
hatua ili tuepuke magonjwa yasiyoambukiza,”.
Takwimu za mwaka 2023 za Wizara ya Afya Tanzania zinaonesha magonjwa hayo
mawili yaliyo katika kundi la magonjwa yasiyoambukiza yanazidi kushika kasi kwa
idadi kubwa ya wagonjwa.
Kulingana na ripoti hiyo, magonjwa hayo kwa mara ya kwanza yameingia katika orodha ya magonjwa 10 yanayoongoza kwa rekodi ya idadi kubwa ya wagonjwa katika vituo vya kutolea huduma za afya.
Waziri Ummy ameihimiza jamii kuepuka tabia bwete na mtindo mbovu wa
maisha ili kuepukana na magonjwa hayo.
“Tunahitaji kuwekeza katika afya, vijana zingatieni mtindo bora wa maisha,
ulaji unaofaa na kujenga desturi ya kufanya mazoezi,” amesema.
Amesisitiza ni muhimu kuwekeza katika afya kwani magonjwa yasiyoambukiza
yana gharimu uchumi katika kuyagharamia, yakiathiri wengi na hata kusababisha
vifo.
Pamoja na hayo amesema Serikali itaendelea kuchukua hatua za makusudi za kuwekeza kwenye miundombinu ya kutoa huduma za Afya.
“Ikiwemo kujenga Zahanati, Vituo vya Afya, Hospitali za ngazi zote na kuimarisha
upatikanaji wa huduma za uchunguzi ikiwemo huduma za maabara,” amesema.
Amesisitiza “Serikali inaendelea kuwekeza katika upatikanaji wa
rasilimali watu wa Afya kwa ngazi zote kuanzia huduma za Afya za msingi hadi
huduma za ubingwa na ubingwa bobezi.
Amesema pia inaendelea kuimarisha upatikanaji wa dawa pamoja na kuwekeza
kwenye elimu ya Afya kwa Umma.
Amehimiza Watanzania kuendelea kukata/kujiunga na mifuko ya bima ya afya ajili waweze kupata huduma wakati wowote pale wanapohitaji, bila kikwazo cha
fedha.
Chapisha Maoni